Ndugu Zaidi Wanahitajiwa Katika Utumishi wa Painia
1 Paulo alitusihi ‘sikuzote tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Kor. 15:58, NW) Kwa wengi, kufanya hivyo kwamaanisha kuchukua utumishi wa painia. Septemba huu uliopita, zaidi ya 200 walijiunga na mapainia!
2 Kwa sasa idadi kubwa ya wale wanaotumikia wakiwa mapainia katika Afrika Mashariki ni akina dada. (Zab. 68:11) Ingekuwa shangwe kama nini kwa makutaniko ikiwa ndugu zaidi wangejiunga na watumishi wa wakati wote! (Zab. 110:3) Ni jambo lenye kueleweka kwamba ndugu wengi wanalazimika kutunza wajibu mbalimbali wa maana na wa familia. Wengine pia hufanya bidii kutunza mahitaji ya kiroho ya kutaniko. Twathamini wanaume hawa wenye kujitahidi kwa ajili ya Ufalme.—1 Tim. 4:10.
3 Lakini, je, wengi wenu akina ndugu mngeweza kuchukua utumishi wa painia? Ikiwa mke wako anapainia, je, waweza kujiunga naye? Ikiwa umestaafu, hukubali kwamba hakuna njia bora zaidi yenye kuleta uradhi ya kutumia wakati wako kuliko kuutumia katika huduma ya wakati wote? Ikiwa unamaliza tu shule, umefikiria kwa bidii na kwa sala kuchukua pendeleo la utumishi wa painia kuwa njia ya kukufungulia mapendeleo zaidi ya utumishi?—Efe. 5:15-17.
4 Ndugu mmoja aliuza biashara yake yenye mafanikio na kuchukua kazi isiyo ya wakati wote ili aweze kupainia. Kwa uongozi wake mzuri, watatu kati ya watoto wake wanne wakawa mapainia upesi walipomaliza shule. Yule wa nne alikuwa na hamu ya kujiunga nao. Ndugu huyu na familia yake wamebarikiwa vilivyo.
5 Mlango Mkubwa Umefunguliwa: Utumishi wa painia waweza kufungua ‘mlango mkubwa ufaao [“uongozao kwenye utendaji,” NW].’ (1 Kor. 16:9) Akina ndugu walio mapainia wanaweza kutumiwa zaidi katika kutaniko. Utendaji wenye bidii wa shambani huongezea hali yao ya kiroho na huchangia maendeleo ya kitheokrasi. Kupainia kwaweza kufungua njia ya kupata mapendeleo ya ziada ya utumishi. Baada ya mwaka wa kwanza wa kupainia, kuna baraka ya kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Watumishi wa huduma na wazee walio waseja wanaweza kufikia mradi wa kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Akina ndugu hatimaye wanaweza kustahili kwa kazi ya kusafiri. Naam, huduma ya painia hufungua mlango wa mapendeleo haya makubwa ya utumishi katika tengenezo la Yehova.
6 Akina ndugu wanaoweza kupanga mambo yao ili kushiriki utumishi wa painia wa kawaida wanaweza kupata furaha kubwa zaidi inayotokana na kutoa kwingi.—Mdo. 20:35.