Watu wa Namna Zote Wataokolewa
1 Mapenzi ya Yehova ni “kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4, NW) Ingawa watu wanaathiriwa kwa kadiri fulani na urithi, malezi, na mazingira, wana hiari ya kuchagua nao waweza kuchagua wakiwa mtu mmoja-mmoja jinsi watakavyotumia maisha zao. Wanaweza kufanya yaliyo mema waishi, au wanaweza kufanya yaliyo mabaya waangamie. (Mt. 7:13, 14) Uelewevu huu unaathirije maoni yetu kuhusu watu tunaowafikia tukiwa na habari njema za Ufalme?
2 Tusidhanie tu kwamba kupendezwa kwa mtu katika kweli kwaamuliwa na mambo kama vile taifa au malezi ya kitamaduni au na hali ya kijamii. Kweli yaweza kuvutia wale walio na ama elimu ndogo au kubwa, wale wanaohusika na ufuatiaji wa mambo ya kisiasa, na wataalamu, waatheisti (wasioamini kuwako kwa Mungu), waagnosti (waaminio kwamba ya Mungu hayawezi kujulikana), na hata kwa wakosaji wenye sifa mbaya sana. Watu kutoka malezi yote na viwango vyote vya kijamii wamebadilika kutoka mwenendo wao wa zamani nao sasa wako katika hali ya kupata uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Mit. 11:19) Kwa hiyo, hatupaswi kusitasita kuwafikia watu wa aina zote tukiwa na ujumbe wa Ufalme.
3 Fikiria Vielelezo Hivi: Mwanamume mmoja alikuwa amepanga kumwua baba yake wa kambo lakini hakufanya hivyo. Baadaye aliamua kujiua lakini hakufanya hivyo. Baada ya kutiwa gerezani kwa sababu ya kuiba na kufanya ulanguzi wa dawa za kulevya, ndoa yake ilivunjika. Leo mtu huyu anaishi kwa kufuatia haki na anafurahia ndoa yenye furaha na pia uhusiano bora pamoja na baba yake wa kambo. Badiliko hilo lilitokana na nini? Alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova naye akatumia aliyojifunza. Yehova hakumwona kuwa asiyeweza kukombolewa.
4 Umaarufu wa mwanamke mmoja mchanga akiwa mwigizaji wa kike katika televisheni haukumletea furaha. Lakini alipopata kuvutiwa na mwenendo mwema wa adili wa Mashahidi, alikubali funzo la Biblia, naye upesi alikuwa anasaidia wengine kujifunza juu ya habari njema za Ufalme. Popote alipoenda katika huduma ya mlango hadi mlango alitambuliwa, lakini kwa furaha alieleza kwamba yeye alitaka kujulikana kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova badala ya mwigizaji wa kike.
5 Shahidi mmoja alipopanga funzo la Biblia na mwandikishaji mmoja wa gazeti Mnara wa Mlinzi, jirani alisikia kuhusu hilo na akahudhuria funzo. Jirani huyo alitambua kweli aliyokuwa akitafuta mara moja! Yeye na mume wake walivunja agizo la talaka ambalo walikuwa wamepewa na walifanya maafikiano. Mwanamke huyo alikuwa amehusika sana na unajimu naye alikuwa ameshikamana na madhehebu ya uasiliani-roho, lakini alitupa vitabu vyake vya bei ghali na kila kitu alichokuwa nacho ambacho kilihusiana na ibada ya roho waovu. Upesi alianza kuhudhuria mikutano na kuongea na watu wa ukoo na marafiki kuhusu imani yake mpya. Sasa yeye hutolea wengine ushahidi kwa idili.
6 Hatupaswi kumhukumu mtu yeyote kimbele. Badala ya hivyo, na tushiriki kwa bidii habari njema na watu kila mahali. Tuna kila sababu ya kuwa na uhakika kwamba Yehova, ambaye “huutazama moyo,” atakuwa “Mwokozi wa namna zote za watu.”—1 Sam. 16:7; 1 Tim. 4:10, NW.