Saidia Wasio na Uzoefu Waelewe
1 Kupitia kazi ya kufanya wanafunzi, twafundisha wengine yale ambayo Mungu anataka wafanye. (Mt. 28:19, 20) Jitihada kubwa ya kufanya hivyo inakaziwa ulimwenguni pote na Mashahidi zaidi ya milioni tano. Mafanikio hayapimwi kwa kiwango cha saa zinazotumiwa, fasihi inayoangushwa, au mafunzo ya Biblia yanayoanzishwa. Twafikia lengo letu watu wanapoelewa na kutenda kulingana na yale wanayojifunza.
2 Kusaidia wengine kiroho hutia ndani ‘kuwapa ufahamu wasiojua kitu.’ (Zab. 119:130, Habari Njema kwa Watu Wote) Mioyo inaguswa na watu wanachochewa tu ‘wanapopata maana.’ (Mt. 15:10) Kazi yetu ipanukapo na kuongezeka, twapata kung’amua zaidi uhitaji wa kusema na kufundisha kwa usahili. Ndiyo sababu Sosaiti imechapisha broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Ina mtaala wa funzo wenye mapana unaoshughulikia mafundisho ya msingi ya Biblia. Masomo ni mafupi, maneno si magumu, na mafundisho ni rahisi kuelewa, yakiipa broshua hiyo uvutio mkubwa.
3 Broshua hii itatolewa pamoja na magazeti miezi ya Aprili na Mei. Inapendekezwa kwamba unapopangia utendaji wako wa utumishi wa kila juma, upange kutoa magazeti Jumamosi lakini utoe broshua katika huduma yako siku nyingine za juma. Wapelekee broshua watu ambao wamekubali fasihi kwa utayari wakati uliopita. Kumbuka kwamba inaweza kusaidia hasa kufundisha watoto, watu wanaosema lugha ya kigeni, na wale walio na uwezo mdogo wa kusoma.
4 Tumia Mfikio Sahili: Unapotoa broshua Anataka, rejezea ukurasa wa 2, inapoeleza kwamba “kusudi la broshua hii ni ili kujifunza Biblia.” Elekeza kwenye fungu la 3 ukurasa wa 3 kuonyesha sababu kwa nini mtu huyo anahitaji kujifunza Biblia. Amsha kupendezwa kwake na baadhi ya vichwa vya masomo vinavyofunua kweli sahili za Biblia. Onyesha jinsi broshua hii hufanya kujifunza kupendeze, na ujitolee kumsaidia binafsi.
5 Ongoza Funzo Lenye Maendeleo: Mradi wetu si kuongoza mafunzo tu—twataka kufanya wanafunzi ambao watakuwa waungaji-mkono imara wa ibada ya kweli. Broshua hii yaweza kumalizwa kwa majuma kadhaa nayo yapaswa kuongoza hadi kwenye funzo la kitabu Ujuzi. (Ona kielezi-chini kwenye ukurasa wa 31.) Kuanzia mwanzo, saidia mwanafunzi atambue tengenezo la Yehova. (Ona kitabu Kutoa Sababu, ukurasa wa 314-315.) Kazia thamani ya mikutano ya kutaniko, na ueleze kwamba kuihudhuria huandaa uelewevu mpana wa jinsi ya kudhihirisha ibada ya kweli.—Ebr. 10:24, 25.
6 Ushiriki kamili katika kazi hii ya pekee katika miezi ya Aprili na Mei kwa hakika utatuletea shangwe inayotokana na kusaidia watu wenye mioyo myeupe ‘wajipatie ufahamu’ unaoongoza kwenye uhai.—Mit. 4:5.