Lazima Turudi Tena na Tena
1 Je, uliitikia vizuri mara ya kwanza mtu fulani alipokwambia habari njema? Ikiwa sivyo, lazima ushukuru kwamba Mashahidi wa Yehova walirudi tena na tena hadi ulipokubali funzo la Biblia hatimaye. Inafaa kufikiria hilo unapohubiri kwa kurudia eneo lako ulilogawiwa.
2 Maisha za watu zabadilika kila mara. Wao hukabili matatizo mapya au hali mpya, husikia matukio yenye kuudhi katika jumuiya au ulimwenguni, hupatwa na mshuko wa kiuchumi, au huwa wagonjwa au hupatwa na kifo katika familia. Huenda mambo hayo yakawafanya watake kujifunza sababu ya taabu zote hizo. Lazima tufahamu mambo yanayowavunja watu moyo kisha tuitikie tukiwa na ujumbe wenye kufariji.
3 Hii Ni Kazi ya Kuokoa: Wafikirie wafanyakazi wenye kuokoa mahali palipotokea msiba. Hata ingawa huenda wengine wakawa wanatafuta mahali palipo na waokokaji wachache, huwa hawajilegezi na kuacha kwa sababu wafanyakazi wenzao wanapata waokokaji wengi mahali kwingineko. Kazi yetu ya kuokoa haijaisha bado. Kila mwaka, mamia ya maelfu ambao wanataka kuokoka “dhiki kubwa” wanapatikana.—Ufu. 7:9, 14.
4 “Kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa.” (Rom. 10:13-15) Maneno hayo yanapaswa kukazia kila mmoja wetu uhitaji wa kuendelea kuhubiri. Tangu eneo letu lianze kuhubiriwa, watoto wamekua na sasa ni wakubwa kuweza kufikiria kwa uzito kuhusu wakati wao ujao na kusudi la uhai. Hatuwezi kujua ni nani ambaye mwishowe atasikiliza. (Mhu. 11:6) Wapinzani wengi wa zamani wamekubali kweli. Kazi yetu si kuhukumu watu, bali kuendelea kuwapa fursa ya kusikia na kuokolewa kutoka katika ulimwengu huu wa kale. Kama vile wanafunzi wa mapema wa Yesu walivyofanya, lazima ‘tuwaendee watu kwa kuendelea’ na kujaribu kuchochea kupendezwa kwao katika ujumbe wa Ufalme.—Mt. 10:6, 7.
5 Uhakika wa kwamba bado kuna fursa ya sisi kuhubiri ni wonyesho wa rehema ya Yehova. (2 Pet. 3:9) Tunapowaruhusu wengine wasikie ujumbe tena na tena, twakazia upendo wa Mungu, na kwa njia hiyo twamsifu yeye.