Watumishi wa Huduma Hutoa Utumishi Wenye Thamani
1 “Wamejionyesha kuwa wanaume walio wakfu kweli kweli ambao imani yao imeonyeshwa kwa utumishi wenye bidii wa Ufalme na katika kusaidia wengine wawe imara katika imani.” Ndivyo kinavyosema kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, kwenye ukurasa wa 57, kuhusu watumishi wa huduma. Kwa kweli, kielelezo cha kiroho kinachowekwa na watumishi wetu wa huduma chastahili kuigwa. Kufanya kazi pamoja nao na pamoja na wazee “hutokeza ukuzi wa mwili ili kujijenga huo wenyewe katika upendo.”—Efe. 4:16.
2 Watumishi wa huduma hutimiza sehemu ya maana sana kutanikoni. Ebu fikiria utumishi wao wote wenye thamani! Wao hushughulikia hesabu, fasihi, magazeti, maandikisho, na maeneo; wao hutumikia wakiwa wakaribishaji, hushughulikia vifaa vya sauti, na kusaidia kudumisha Jumba la Ufalme. Wao hushiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Baadhi yao huenda wakatoa hotuba za watu wote au kuongoza mikutano fulani ya kutaniko. Wakiwa kama viungo vya mwili wa asili, watumishi wa huduma hutimiza utumishi mbalimbali tunaohitaji.—1 Kor. 12:12-26.
3 Kuwaona watumishi wa huduma wakishirikiana na wazee kwa upatano wakiwa sehemu ya baraza moja la utumishi kwa kustahiana na kuelewana hutia moyo wengine wafanye vivyo hivyo. (Kol. 2:19) Kwa kutimiza madaraka yao juma baada ya juma na kwa kuonyesha wanapendezwa na wengine kibinafsi, wao huchangia maendeleo ya kiroho ya kutaniko.
4 Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha uthamini wetu kwa kazi ngumu ya watumishi wa huduma? Twahitaji kufahamu wajibu wao waliogawiwa na kuwa tayari kushirikiana nao wanapohitaji msaada wetu. Kwa maneno na matendo, tunaweza kuwajulisha kwamba kazi yao inathaminiwa sana. (Mit. 15:23) Wale wanaofanya kazi kwa bidii kwa niaba yetu wanastahili kuonyeshwa wanatambuliwa kwa moyo mweupe.—1 The. 5:12, 13.
5 Neno la Mungu huweka kiwango cha daraka na sifa za watumishi wa huduma. (1 Tim. 3:8-10, 12, 13) Utumishi wao mtakatifu wenye thamani ni wa lazima ili kutaniko liendelee. Wanaume hao hustahili kitia-moyo chetu chenye kuendelea, wanapokuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Kor. 15:58.