Aprili—Wakati wa Kuwa Wenye Bidii kwa Kazi Zilizo Bora!
1 Kimbunga kinapokaribia sehemu yenye watu, kunakuwa na uhitaji wa hima wa kuonya watu juu ya hatari inayokaribia. Kadiri kimbunga kikaribiavyo, ndivyo mkazo wa kutoa onyo uzidivyo. Kwa nini? Kwa sababu uhai umo hatarini! Huenda ikawa watu fulani hawakusikia maonyo yaliyotolewa awali. Huenda ikawa wengine walisikia lakini wakapuuza kuchukua hatua. Ndivyo ilivyo na onyo la kimungu ambalo tumeagizwa kutoa kabla “kisulisuli” cha hasira yenye uadilifu ya Mungu hakijapulizia mbali masazo ya mfumo huu mbovu wa mambo. (Mit. 10:25) Uhai wa milele wa mabilioni ya watu umo hatarini! Lazima onyo litolewe. Lazima tuwe “wenye bidii kwa kazi zilizo bora.”—Tito 2:11-14.
2 Kwa miongo kadhaa, watu wa Yehova wamechochewa kufanya majira ya Ukumbusho kuwa wakati wa bidii ya pekee katika huduma. Katika masika ya 1939, Informant, ambayo ilikuja kuwa Huduma ya Ufalme Yetu, iliandaa kitia-moyo hiki: “Masika yakaribiapo, na hali ya hewa yenye kupendeza, twatazamia muda wa saa za utumishi za wahubiri wa [kutaniko] utakuwa maradufu na wakati wa mapainia uongezeke zaidi. Mwezi wa Aprili una Jumapili tano. Pia una Jumamosi tano. Fanya kila Jumamosi na Jumapili za mwezi wa Aprili . . . kuwa wakati wa kutoa ushahidi kipekee.” Huo ulikuwa mradi uliowekewa akina ndugu miaka 60 iliyopita! Mwaka huu, sawa na mwaka wa 1939, mwezi wa Aprili una miisho-juma mitano kamili. Mipango yako ni ipi mwezi huu? Umeandika nini kwenye kalenda yako ya mwezi wa Aprili 2000? Panga ushiriki kikamili katika kazi zilizo bora na watu wengine wa Yehova wakati wa mwezi huu wa pekee wa utendaji wa kiroho uliozidishwa.
3 Tunayotazamia Kutimiza: Siku ya maana zaidi ya mwaka wa 2000 itakuwa mwezi huu. Ni Aprili 19, ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu. Na tufanye jitihada ya pekee kualika watu wengi iwezekanavyo kwenye Ukumbusho. Kama ilivyodokezwa mwezi uliopita, andika orodha ya wale wote wanaotazamiwa kuhudhuria Ukumbusho na uangalie kwamba hakuna anayesahauliwa. Wale wanaoalikwa wapaswa kutia ndani wahubiri wasiotenda, wanafunzi wa Biblia, ziara za kurudia, wale waliokuwa wakijifunza hapo zamani, wafanyakazi wenzi, wanashule wenzi, majirani, watu wa jamaa, na watu wengine unaowajua. Je, wale wanaotaka kuhudhuria wana namna ya kusafiria? Ikiwa hawana, je, waweza kusaidia kwa upendo? Usiku wa Ukumbusho huo, sisi sote tutakuwa na pendeleo la kufanya wale watakaohudhuria wahisi wamekaribishwa. Baada ya Ukumbusho, twaweza kuwatolea msaada wa ziada wa kiroho watu hao wenye kupendezwa.
4 Kuwa “wenye bidii kwa kazi zilizo bora” siku za kabla na baada ya Ukumbusho ni njia bora ya kumwonyesha Yehova kwamba twathamini kikweli yale yote ambayo ametufanyia. Wengi wetu tutaweza kuongeza jitihada zetu katika kazi ya kueneza evanjeli. Ikiwa unafanya upainia-msaidizi, ungependa kufanya kadiri uwezavyo kutumia muda wa saa 50 au zaidi katika huduma. (Mt. 5:37) Shikamana kabisa na ratiba uliyotayarisha mwanzoni mwa mwezi. (Mhu. 3:1; 1 Kor. 14:40) Sisi sote na tufanye yote tuwezayo kuunga mkono mapainia wote, tukiwatia moyo na kuhubiri nao katika utumishi. (Linganisha 2 Wafalme 10:15, 16.) Tukipanda kwa bidii mwezi wa Aprili, twaweza kutazamia shangwe kubwa na baraka kutoka kwa Yehova. (Mal. 3:10) Labda hiyo itakuwa njia fulani ya kuendelea kuwa painia-msaidizi au painia wa kawaida. Mwendo huo wa kiroho tupatao Aprili na uendelee katika miezi inayofuata tuendeleapo kuwa wahubiri wa kawaida wa Ufalme.
5 Bila shaka, maelfu ya watu wa Yehova wataanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani mwezi huu. Je, ungependa kuanzisha moja? Sali hasa upate funzo, na utende kupatana na sala zako. Waweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atathamini maombi yako ya unyenyekevu ya kutaka msaada wa kupata mtu mwenye moyo wa haki ili kumfundisha.—1 Yh. 3:22.
6 Ufuatao ni mfikio wa utumishi uliojaribiwa ambao umetumiwa kwa mafanikio kuanzisha mazungumzo. Waanza kwa kuuliza: “Je, wafikiri kwamba jeuri yote katika shule za umma husababishwa na utendaji wa roho waovu, au inatokana na ukosefu wa mazoezi ya mzazi?” Ngoja jibu. Mtu akisema “utendaji wa roho waovu,” soma Ufunuo 12:9, 12, na ukazie fungu la Ibilisi katika kuchochea msukosuko ulimwenguni. Kisha fungua broshua Anataka somo la 4, na umwulize mtu huyo kama amepata kujiuliza Ibilisi alitoka wapi. Endelea kusoma na kuzungumzia mafungu mawili ya kwanza. Mtu akichagua “ukosefu wa mazoezi ya mzazi” kuwa sababu ya jeuri katika shule, soma 2 Timotheo 3:1-3 na utaje tabia ambazo kwa wazi husababisha tatizo hilo. Kisha fungua broshua Anataka somo la 8, soma fungu la 5, na uendelee na mazungumzo. Ukiweza kufanya mpango wa kurudi, labda utakuwa unaanzisha funzo la kawaida la Biblia na mtu huyo. Wakati wa ziara inayofuata, mwulize kama anajua yeyote ambaye huenda akapendezwa kusikia yale anayojifunza.
7 Njia nyingine ya kuwa “wenye bidii kwa kazi zilizo bora” mwezi wa Aprili ni kushiriki njia mbalimbali za kuhubiri. Je, umekuwa ukifikiria kutoa ushahidi kwenye bustani au kwenye maegesho ya gari? Kwenye kituo cha basi au stesheni ya garimoshi? Au je, ungependa kujaribu kutoa ushahidi kwa simu, au barabarani, au kwenye eneo la biashara? Kwa nini usitumie mawazo hayo kihalisi mwezi huu? Yehova atakusaidia ujipatie ujasiri unaohitajiwa. (Mdo. 4:31; 1 The. 2:2b) Labda unaweza kufanya mpango uhubiri na painia au mhubiri aliye na uzoefu katika sehemu hizi za huduma.
8 Mtu yeyote aliye na tamaa ya kuongeza utendaji wake katika kazi ya kutoa ushahidi atataka kushiriki katika ushahidi wa vivi hivi. Mara nyingi kile kinachohitajiwa tu ni kumhusisha mtu katika mazungumzo ya kirafiki. Tokeza tu jambo linalowapendeza watu kwa kawaida, labda kwa kutumia mfikio unaokaziwa katika fungu la 6. Jitahidi kutumia ifaavyo sehemu ndogo za wakati ambao huenda ungepotezwa. Sisi hatutupi ndururu, peni moja, au thumni kwa sababu tu sio shilingi nzimanzima. Kwa nini usitumie kwa faida hata dakika tano, kumi, au robo saa kutoa ushahidi wa vivi hivi?
9 Wakati wa Kufikiria Yaliyotokea: Fikiria mambo ya maana yaliyotajwa katika drama kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka jana wa “Neno la Mungu la Kiunabii.” Drama hiyo, yenye kichwa Kuthamini Urithi Wetu wa Kiroho, ilitufanya tufikirie kwa uangalifu tofauti kati ya Yakobo na Esau. Esau alisema kwamba alipendezwa na mambo ya kiroho kama Yakobo, lakini matendo ya Esau hayakuonyesha hivyo. (Mwa. 25:29-34) Hilo lilikuwa onyo kali sana kwetu kama nini! Kama Yakobo, na tuwe tayari kung’ang’ana, hata kushindana mwereka, ili kupata baraka za Yehova. (Mwa. 32:24-29) Kwa nini tusitumie Aprili na miezi yote inayokuja kufanya upya bidii yetu, kutochukulia hivihivi kamwe urithi wetu bora wa kiroho?
10 “Siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana.” (Sef. 1:14) Lazima habari njema za Ufalme zitangazwe. Uhai umo hatarini! Mwezi huu na uthibitike kuwa uliobarikiwa hasa kwa watu wote wa Yehova tuonyeshapo kwa muungano kwamba tu wenye “bidii kwa kazi zilizo bora.”
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Vikumbusha vya Ukumbusho
Sherehe ya Ukumbusho mwaka huu itakuwa Jumatano, Aprili 19. Wazee wapaswa kukazia uangalifu mambo yafuatayo:
◼ Mnapoweka saa za mkutano, hakikisheni kwamba mifano haitapitishwa mpaka baada ya jua kushuka.
◼ Kila mtu, kutia na msemaji, apasa kujulishwa wakati hasa na mahali pa sherehe.
◼ Mkate na divai inayofaa yapaswa kupatikana na kuwa tayari.—Ona Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 1985, ukurasa wa 17.
◼ Sahani, bilauri, meza, na kitambaa cha meza kifaacho vyapasa kuletwa kwenye jumba na kuwekwa mahali pake mapema.
◼ Jumba la Ufalme au mahali pengine pa mkutano papasa kusafishwa kikamili mapema kabla ya wakati.
◼ Wakaribishaji na wapitishaji wa mifano wapasa kuteuliwa na kuagizwa mapema juu ya utaratibu unaofaa na wajibu wao.
◼ Mipango yapasa kufanywa kuwatumikia wowote kati ya watiwa-mafuta walio dhaifu na wale ambao hawawezi kuwapo.
◼ Makutaniko zaidi ya moja yanaporatibiwa kutumia Jumba la Ufalme lilelile, kwapaswa kuwe na makubaliano mazuri miongoni mwa makutaniko ili kuepuka msongamano usio wa lazima kwenye sebule, mahali pa kuingilia, vijia vya kando ya barabara vya watu wote, na maegesho ya magari.