Dumisha Mwenendo Mzuri Unaomtukuza Mungu
1 Popote tulipo, mwenendo wetu, mavazi na mapambo yetu hutoa ushahidi kutuhusu na vilevile kuhusu Mungu tunayeabudu. Hilo huonekana waziwazi hasa kwenye mikusanyiko mikubwa ya watu wa Mungu, mahali ambapo watu wengi hututazama. Tunapoweka kielelezo, jina la Yehova hutukuzwa. (1 Pet. 2:12) Hata hivyo, tabia mbaya au matendo yasiyofaa ya wachache yanaweza kuletea suto jina la Mungu na watu wake. (Mhu. 9:18b) Tunapokumbuka kwamba kwa mwenendo wetu watu wa nje huhukumu tengenezo letu na Mungu tunayeabudu twapaswa kudhamiria ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’—1 Kor. 10:31.
2 Mwenendo Mzuri Hotelini: Katika visa vingi, wafanyakazi wa hoteli au wa mabweni huvutiwa sana na utaratibu, tabia njema, na usafi wa Mashahidi wa Yehova. Alipokuwa akizungumza kuhusu familia za Mashahidi zilizokaa hotelini mwake, meneja mmoja alisema: “Watoto wa Mashahidi wa Yehova ndio watoto bora kabisa niliopata kuwaona! Wamevaa kama mabibi na mabwana, ni wapole, wenye adabu nzuri, na tabia njema, na hawajatokeza tatizo lolote. Mwapaswa kusifiwa kweli kwa ajili ya vijana wenu. Tumefurahi kuwa na watoto wenu hapa.” Tunapokea maelezo kama hayo kwa sababu wale wanaoshughulika nasi wanaweza kuona upendo na staha iliyopo miongoni mwa watu wa Yehova.
3 Kwa upande mwingine, maelezo kutoka kwa wafanyakazi wa hoteli au wa mabweni yaonyesha kwamba bado wengine wana tatizo katika mwenendo wao au hutumia vibaya hoteli au mabweni. Hilo hutokeza matatizo na kufanya tuchambuliwe isivyo lazima. Mameneja fulani hulalamika kwamba watoto na matineja wana kelele na ni watukutu, huku wakiachwa bila mwongozo na wazazi wao wanapotembea kwenye ua.
4 Hoteli na shule nyingi zina sheria ambazo wageni wanatarajiwa kufuata. Ndugu wengine wamevunja sheria hizo kuhusu kelele au kupika katika vyumba vyao. Kupikia mahali usiporuhusiwa, ni kutumia vibaya mahali hapo.
5 Jitihada halisi yapasa kufanywa ili kushirikiana kikamili na wasimamizi. Kwa hakika, hatutaki kuacha wazo lisilofaa kuhusu watu wa Yehova. Tukiwa Wakristo lazima tujiendeshe vyema nyakati zote. Hatupaswi kuchukua matandiko au “tunu” kutoka mahali tunapolala, kwa kuwa huo ni wizi; wala hatupaswi kusema uwongo tunaporipoti ni watu wangapi tunaopanga kuwatafutia mahali pa kulala au idadi ya watakaokuwa katika chumba tunapoweka nafasi au tunapojiandikisha.
6 Mwenendo Unaofaa Mkusanyikoni: Bila kujali ni jengo la aina gani tunalotumia, linakuwa Jumba kubwa la Ufalme wakati wa mkusanyiko. Twapaswa kuvalia mavazi na mapambo yanayofaa kama tufanyavyo wakati tunapohudhuria mikutano ya kutaniko letu. Wakati na baada ya vipindi vya mkusanyiko, twapaswa kuepuka kuvalia mavazi yasiyo na kiasi au ya kimtindo, yanayodhihirisha roho ya ulimwengu na kufanya iwe vigumu kututambulisha kuwa tofauti. Akina dada wapaswa kuwa waangalifu kwamba mtindo na urefu wa skati na nguo zao ni wa kiasi kinachofaa. (1 Tim. 2:9, 10) Tuwe tunahudhuria mkusanyiko, tunakaa kwenye hoteli, tunakula kwenye mkahawa, au kununua vitu dukani, nyakati zote tabia zetu zapasa kuonyesha kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu, tukiepuka sababu yoyote ya kukwaza.—2 Kor. 6:3.
7 Ubatizo utafanywa Jumamosi asubuhi kwenye mkusanyiko. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1995, ukurasa wa 30 laeleza mtazamo tunaopaswa kuwa nao kwenye pindi hiyo. Linasema kwamba “twapaswa kuona ubatizo kwa uzito ufaao. Huo si wakati wa kupaaza sauti kwa hisiamoyo, wa kufanya karamu, au wa kushangilia kwa kelele nyingi. Wala huo si wakati wa mtu kukosa uchangamshi au furaha.” Haingefaa hata kidogo wale wanaobatizwa kuvalia mavazi yanayobana au mavazi ya kuoga yasiyo marefu vya kutosha, wawe ni wanaume au wanawake. Hivyo, wote wapaswa kuonyesha uzito na shangwe ya ubatizo wa Kikristo.
8 Petro atukumbusha ‘twapaswa kuwa watu wa aina gani katika matendo matakatifu na mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.’ (2 Pet. 3:11) Maneno na matendo yetu mwaka huu kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu” na yasaidie watu wenye moyo mweupe wamjue na kumwabudu Mungu wetu mkuu, anayestahili heshima yote na utukufu.—1 Kor. 14:24, 25.