‘Iweni Wakarimu, Tayari Kushiriki’
1 Karne kadhaa zilizopita Mtume Paulo alimwagiza Timotheo atie moyo waamini wenzake “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Tim. 6:18) Paulo pia aliwakumbusha Wakristo Waebrania wasisahau “kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine.” (Ebr. 13:16) Kwa nini aliandika maagizo hayo? Kwa sababu alijua kwamba kungekuwako “utukufu na heshima na amani kwa kila mtu afanyaye lililo jema.”—Rom. 2:10.
2 Kwa sababu yeye ni Muumba, Yehova Mungu ndiye Mwenye Kumiliki vitu vyote. (Ufu. 4:11) Kwa kweli twathamini yale anayotufanyia kwa mali zake. Ujapokuwa mtazamo usio wa shukrani wa wanadamu wengi, Aliye Juu Zaidi huendelea kuruhusu wote wanufaike na maandalizi yake ya ukarimu ya kuendeleza uhai. (Mt. 5:45) Hata alitoa Mwanawe mpendwa zaidi awe dhabihu ili tuweze kupata uhai wa milele. Je, upendo ambao tumeonyeshwa haupaswi kutuchochea tuwe wenye shukrani kwa kuwa wakarimu kwa wanadamu wenzetu?—2 Kor. 5:14, 15.
3 Twaweza Kuwapa Nini? Inafaa kutumia mali zozote tulizo nazo kwa njia inayompendeza Mungu. Kwa kweli, twataka kutegemeza kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote kwa njia ya kimwili na kiroho. Bila shaka, habari njema ni hazina yenye thamani zaidi ambayo mtu anaweza kuwa nayo, kwa kuwa hiyo ni “nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu.” (Rom. 1:16) Kwa kutumia wakati wetu na mali zetu kwa ukarimu kila mwezi ili kushiriki katika kuhubiri na kufundisha, twaweza kuwapa wengine hazina hii ya kiroho, iwaongozayo kupata uhai wa milele.
4 Yehova hupendezwa sana tunaposaidia wale wenye mali chache. Yeye anaahidi kutubariki, na pia hutukumbusha hivi: “Mali hazifai kitu siku ya ghadhabu; bali haki huokoa na mauti.” (Mit. 11:4; 19:17) Kutegemeza kazi ya Ufalme kimwili na kushiriki kikamili katika kuhubiri habari njema ni njia nzuri ajabu tunazoweza kuonyesha kwamba sisi tu wakarimu, tayari kushiriki.