Programu Mpya ya Kusanyiko la Mzunguko
Maana moja ya neno hofu ni kuwa na “staha nyingi na kicho, hasa kumwelekea Mungu.” Hiyo ni hofu inayofaa inayotajwa katika Maandiko kuwa “mwanzo wa hekima.” (Zab. 111:10) Kinyume cha hofu hiyo, aina nyingine ya hofu hutawala ulimwengu wa Shetani unaotuzunguka. Twawezaje kuepuka hofu hiyo isiyofaa huku tukisitawisha hofu yenye staha nyingi kwa Yehova? Programu mpya ya kusanyiko la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2002 yajibu swali hilo. Kichwa cha kusanyiko ni “Hofuni Mungu na Kumpa Utukufu.” (Ufu. 14:7) Tutaelewa jinsi ambavyo kumhofu Yehova hutufaidi tukiwa watu mmoja-mmoja na tukiwa tengenezo pia.
Ingawa hofu yaweza kuonyesha kwamba mtu ana wasiwasi au anakosa ujasiri na kusitasita anapokabili hali ngumu, Biblia husema hivi: “Heri kila mtu amchaye [amhofuye, NW] BWANA.” (Zab. 128:1) Programu ya kusanyiko itatuonyesha jinsi ya kukabiliana kwa mafanikio na vipingamizi vya ibada ya kweli. Tutaona jinsi ya kuwasaidia wapya wasitawishe hofu inayofaa kwa Mungu, ambayo itawachochea watake kumtumikia yeye kwa moyo wao wote, nafsi yao yote, akili zao zote, na nguvu zao zote. (Mr. 12:30) Siku ya kwanza itamalizika kwa hotuba ya mwangalizi wa wilaya yenye kichwa “Na Uwe na Uhusiano wa Karibu Zaidi na Wale Unaowapenda.” Ataeleza jinsi tunavyoweza kuwa macho kutambua jitihada za Ibilisi za kututenga mbali na Yehova, familia yetu, na ndugu zetu Wakristo.
“Hofuni Mungu, Wala Si Wanadamu” ndicho kichwa cha mfululizo wa hotuba nne siku ya pili. Zitaeleza kwa nini na ni jinsi gani tunavyoweza kuishinda hofu inayotuzuia kutimiza huduma yetu kikamili, au kudumisha uaminifu wetu na kuwa na dhamiri njema shuleni na kazini. Hotuba ya watu wote yenye kichwa “Hofuni Mungu na Mshike Amri Zake” itategemea mfululizo wa matukio yanayofafanuliwa kwenye Ufunuo sura ya 14. Kusanyiko la mzunguko litamalizika kwa kitia-moyo hiki, “Endeleeni Kutembea kwa Kumhofu Yehova.”
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi wa kigezo, hotuba ya ubatizo, na muhtasari wa Funzo la Mnara wa Mlinzi ni mambo makuu ya ziada ya programu hiyo ambayo haingefaa tukose. Alika wanafunzi wako wa Biblia wahudhurie pamoja nawe. Yeyote anayetaka kubatizwa apaswa kumjulisha mwangalizi-msimamizi bila kukawia. Sisi sote twataka kuonyesha hofu yetu ifaayo kwa Yehova na kumtukuza yeye kwa kutokosa sehemu yoyote ya programu hiyo yenye kutokeza!