Programu Mpya ya Siku ya Kusanyiko la Pekee
Kichwa cha programu ya siku ya kusanyiko la pekee la mwaka mpya wa utumishi kina msingi imara wa Kimaandiko: “Jitiisheni Wenyewe kwa Mungu—Mpingeni Ibilisi.” (Yak. 4:7) Huo ni mwongozo wa maana sana katika hizi nyakati zenye magumu! Kwa kuwa tunatii amri za Mungu, sisi hushambuliwa moja kwa moja na Shetani. Programu hiyo itatufundisha jinsi ya kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi za kuharibu imani yetu. Ni zipi baadhi ya hazina za kiroho tutakazopokea kwenye kusanyiko hilo?
Mwangalizi wa mzunguko ataonyesha jinsi “Kudhihirisha Ujitiisho kwa Mungu Mkiwa Washiriki wa Familia” kunavyoimarisha familia zishinde msongo wa ulimwengu. Hotuba ya kwanza ya msemaji anayezuru yenye kichwa “Kinachomaanishwa na Kumpinga Ibilisi,” itaeleza ni kwa nini na ni jinsi gani tunahitaji kuchukua hatua madhubuti kukinza malengo ya Shetani ya kuharibu hali yetu ya kiroho. Sehemu mbili zitaelekezewa vijana ambao lazima pia wawe macho kuona mbinu za Ibilisi. Wakristo wengi ambao sasa ni watu wazima walikataa kufuata tamaa za ulimwengu walipokuwa wachanga. Tutafurahia kusikia baadhi ya mambo yao ya kibinafsi yaliyoonwa.
Wanadamu wote wapaswa kunyenyekea mamlaka. Kwa hiyo, hotuba ya kumalizia ya msemaji anayezuru itakazia sehemu nne ambazo ujitiisho wetu wa kimungu lazima uonyeshwe: (1) kwa serikali, (2) katika kutaniko, (3) kazini, na (4) katika familia. Hiyo ni programu yenye manufaa kama nini!
Wale ambao wangependa kubatizwa katika siku ya kusanyiko la pekee wanahitaji kujulisha mwangalizi-msimamizi bila kukawia. Sisi sote twapaswa kutia alama tarehe katika kalenda zetu na kupanga kuhudhuria programu yote. Baraka tutakazopokea zitadumu milele twendeleapo kujitiisha kwa Yehova milele.