Ridhika na Yale Uliyo Nayo
1 Maandiko hutuagiza tuiruzuku familia yetu kimwili, lakini hilo halipasi kuwa jambo kuu maishani. Lazima tutangulize mambo ya kiroho. (Mt. 6:33; 1 Tim. 5:8) Kuwa na usawaziko ni jambo gumu katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?
2 Uwe na Maoni Yanayopatana na Biblia: Neno la Mungu latuonya kwamba kufuatia sana utajiri kwaweza kusababisha madhara ya kiroho. (Mhu. 5:10; Mt. 13:22; 1 Tim. 6:9, 10) Wakati huu ulio muhimu, lingekuwa jambo la hatari kwetu kujiingiza zaidi katika kazi ya kuajiriwa au mahangaiko ya kifedha hivi kwamba tukose kutanguliza mambo ya kiroho kama vile, mikutano, funzo, na utumishi. (Luka 21:34-36) Biblia hushauri hivi: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.”—1 Tim. 6:7, 8.
3 Hii haimaanishi kwamba Wakristo wanatakiwa kuishi maisha ya umaskini wa kujilazimisha. Lakini hutusaidia kutambua mahitaji yetu ya kimwili ni yapi—chakula, mavazi, na makao yanayofaana na mahali tunapoishi. Ikiwa tuna mahitaji ya lazima ya maisha, hatupaswi kufuatia kupita kiasi maisha ya hali ya juu zaidi. Tunapofikiria kununua kitu au kufanya kazi ya ziada, itafaa tujiulize, ‘Je, kweli hii ni ya lazima?’ Kujiuliza hivyo kutatusaidia tutii shauri hili lililopuliziwa na roho ya Mungu: “Acheni namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo.”—Ebr. 13:5.
4 Tukimtumaini Yehova, atatubariki. (Mit. 3:5, 6) Ingawa lazima tufanye kazi kwa bidii ili tupate mahitaji ya kila siku, hatutazingatia kupita kiasi mambo hayo maishani. Iwe tuna vitu vichache au vingi, twamtegemea Yehova atosheleze mahitaji yetu. (Flp. 4:11-13) Matokeo ni kwamba twafurahia uradhi wa kimungu pamoja na baraka nyingine nyingi.
5 Iga Imani ya Wengine: Mzazi mmoja aliye peke yake ambaye alikuwa akimlea binti yake katika kweli alifanya maisha yake yawe sahili hatua kwa hatua. Ijapokuwa alifurahia vitu alivyokuwa navyo nyumbani kwake, alihamia kwenye nyumba ndogo na baadaye kwenye nyumba ya kukodisha. Hilo lilimwezesha kupunguza muda aliokuwa akifanya kazi ili aweze kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma. Baada ya binti yake kukua na kuolewa, mama huyo alistaafu mapema, ingawa hilo lingepunguza zaidi mapato yake. Dada yetu sasa amekuwa painia wa kawaida kwa miaka saba na hana masikitiko yoyote kuhusu vitu vya kimwili ambavyo amejinyima ili kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwake.
6 Mzee mmoja na mke wake walifanya upainia kwa miaka mingi huku wakilea watoto watatu. Wakiwa familia, walijifunza kuridhika na mahitaji yao badala ya kuhangaikia vitu wasivyokuwa navyo. Ndugu huyo anaeleza hivi: “Ilitubidi tuishi maisha sahili kabisa. Ingawa tumekuwa na magumu, Yehova ametuandalia mahitaji yetu sikuzote. . . . Ninapoona jinsi ambavyo familia yangu inatanguliza masilahi ya kiroho, nahisi kwamba mambo ni sawa, na naona nimefanikiwa.” Mke wake aongezea kusema: “Ninapoona [mume wangu] akiwa mwenye shughuli katika mambo ya kiroho, ninaridhika kabisa.” Pia watoto wamefurahi kwamba wazazi wao waliamua kumtumikia Yehova wakiwa watumishi wa wakati wote.
7 Wale wote ambao wamechagua mwendo huo wa ujitoaji kimungu badala ya kufuatia vitu vya kimwili, Biblia inawaahidi baraka tele sasa na katika wakati ujao.—1 Tim. 4:8.