Msaidie Mwangalizi Wenu wa Funzo la Kitabu la Kutaniko
1 Kila mmoja wetu hufaidika sana na Funzo la Kitabu la Kutaniko. Mwezi uliopita tulizungumzia jinsi mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko anavyotimiza daraka lake. Lakini twaweza kufanya nini ili sisi wenyewe pamoja na wengine tunufaike?
2 Hudhuria Kila Juma: Kwa sababu vikundi vya funzo la kitabu huwa vidogo, ni muhimu uhudhurie. Weka mradi wa kuhudhuria kila juma. Pia unaweza kusaidia kwa kufika kwa wakati ili mwangalizi aanze mkutano huo kwa utaratibu.—1 Kor. 14:40.
3 Maelezo Yenye Kujenga: Njia nyingine unayoweza kusaidia ni kwa kujitayarisha na kutoa maelezo yenye kujenga. Maelezo yanayokazia jambo moja huwa bora zaidi, na pia huwatia moyo wengine watoe maelezo. Epuka kujaribu kujibu kila kitu katika fungu. Jambo fulani katika habari mnayozungumzia likikugusa moyo, toa maelezo zaidi juu yalo.—1 Pet. 4:10.
4 Ikiwa una pendeleo la kusoma mafungu kwa manufaa ya funzo la kitabu, timiza mgao wako kwa bidii. Usomaji mzuri hufanya funzo lifurahishe.—1 Tim. 4:13.
5 Mahubiri ya Kikundi: Mikutano ya utumishi wa shambani hufanywa katika sehemu nyingi za mafunzo ya kitabu, na kuunga mkono mipango hii humsaidia mwangalizi anapoongoza katika kazi ya kueneza injili. Ione mipango hii kuwa fursa za kuwa na uhusiano wa karibu na ndugu zako na kuwatia moyo.
6 Ripoti za Utumishi wa Shambani: Kutoa ripoti yako bila kukawia mwishoni mwa kila mwezi ni njia nyingine ya kumsaidia mwangalizi wenu. Unaweza kumpa ripoti yako moja kwa moja au kuiweka kwenye kisanduku kilichowekwa kwa ajili ya ripoti za shambani kwenye Jumba la Ufalme. Mwandishi anaweza kutumia kisanduku hicho kukusanya ripoti za utumishi wa shambani zinazoletwa na waangalizi wa funzo la kitabu.
7 Jitihada zako za kushirikiana na mwangalizi wenu wa Funzo la Kitabu la Kutaniko zitathaminiwa sana. Zaidi ya yote, uwe na hakika kwamba Yehova ‘atakuwa na roho unayoonyesha.’—Flp. 4:23.