Kukusanyika Ili Tumsifu Yehova
1 Yehova ni mwenye nguvu zote, hekima yake haichunguziki, ana haki kamilifu, na yeye ni upendo. Yeye peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa kwa sababu yeye ni Muumba, Mpaji-Uhai, na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu. (Zab. 36:9; Ufu. 4:11; 15:3, 4) Kusanyiko la Wilaya la mwaka huu la “Mtukuzeni Mungu” litaimarisha azimio letu la kumsifu yeye akiwa Mungu wa pekee wa kweli.—Zab. 86:8-10.
2 Tunahitaji Kufanya Mipango Mizuri: Ni muhimu tufanye mipango mizuri ili tufaidike kabisa na karamu ya kiroho ambayo Yehova ameandaa. (Efe. 5:15, 16) Je, umekamilisha mipango yako ya kupata mahali pa kulala, usafiri, na kuomba ruhusa kazini au shuleni? Usingoje kushughulikia mambo hayo muhimu dakika ya mwisho. Ukichelewa kuomba ruhusa, huenda ukakosa sehemu fulani ya pindi hiyo yenye shangwe. Sisi sote twapaswa kuhudhuria kila kipindi.
3 Uwe na mradi wa kufika kusanyikoni mapema kila siku. Hiyo itakusaidia kutulia kitini kabla ya wimbo wa kwanza na utaweza kuwa makini ili kupokea mafundisho yatakayotolewa. Tafadhali hifadhi viti kwa ajili tu ya familia yako au wale unaosafiri nao.
4 Wote wanaombwa wabebe chakula cha mchana badala ya kuondoka kusanyikoni na kwenda kununua chakula wakati wa mapumziko. Kufuata mpango huo kunachangia hali yenye utulivu na hufanya kuwe na wakati zaidi wa kushirikiana na waamini wenzako. (Zab. 133:1-3) Tafadhali kumbuka kwamba pombe hairuhusiwi kwenye kusanyiko.
5 Sikiliza na Ujifunze: Ezra aliutayarisha moyo wake kwa sala ili kupokea neno la Mungu. (Ezra 7:10) Aliuelekeza moyo wake ili kupokea mafundisho ya Yehova. (Mit. 2:2) Tunaweza kuanza kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya kusanyiko hata kabla ya kuondoka nyumbani kwa kutafakari kichwa cha kusanyiko na kukizungumzia na familia yetu.
6 Kwenye ukumbi mkubwa au uwanja wa kusanyiko kwaweza kuwa na vikengeusha-fikira vingi. Vikengeusha-fikira hivyo vyaweza kugeuza fikira zetu kutoka kwa msemaji, na kutufanya tukose habari muhimu. Madokezo yaliyo kwenye sanduku lililoonyeshwa hapa yanaweza kutusaidia tuboreshe uwezo wetu wa kukaza fikira.
7 Wajali Wengine: Kamera na kamera za video zaweza kutumiwa wakati wa programu, lakini ili kuepuka kuwakengeusha wengine, zitumie tu mahali unapoketi. Simu za mkononi na peja hazipaswi kuwasumbua wengine. Vifaa vya kibinafsi havipaswi kuunganishwa kwenye mfumo wa kusanyiko wa umeme au sauti.
8 Tuna hamu kubwa kama nini ya kukusanyika ili tumsifu Yehova! Na tuazimie kumtukuza Yehova kwa kuhudhuria kila kipindi, kusikiliza kwa makini, na kutumia yale tunayojifunza.—Kum. 31:12.
[Maswali ya Funzo]
1. Kichwa cha kusanyiko ni kipi, na kwa nini Yehova anastahili sifa zetu?
2, 3. Mipango mizuri itatusaidiaje kufaidika kabisa?
4. Kwa nini wote wanaombwa wabebe chakula cha mchana kusanyikoni?
5. Tunawezaje kuanza kuitayarisha mioyo yetu kwa ajili ya kusanyiko?
6. Ni nini kinachoweza kutusaidia tukazie fikira programu? (Ona Sanduku.)
7, 8. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali wengine?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Kusikiliza Kwenye Kusanyiko
▪ Tafakari vichwa vya hotuba
▪ Fungua maandiko
▪ Andika maandishi machache
▪ Andika mambo makuu ya kutumia
▪ Rudia mambo unayojifunza