Mahubiri ya Vikundi Huleta Shangwe
1 Alipokuwa akiwatuma wale wanafunzi 70 kuhubiri, Yesu aliwafundisha mambo ya kusema, akawapanga wawili-wawili na kuwaambia maeneo ambayo walipaswa kuhubiri. Hiyo iliwaletea shangwe. (Luka 10:1-17) Vivyo hivyo leo, mahubiri ya vikundi husaidia kuwatayarisha, kuwapanga, na kuwatia moyo watu wa Mungu wahubiri.
2 Wazee Huongoza: Wazee hutimiza sehemu muhimu katika kuwasaidia wote washiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri. Mwangalizi wa utumishi huongoza katika kufanya mipango ya utumishi katikati ya juma. Kila mwangalizi wa funzo la kitabu ana daraka la kupanga mahubiri ya kikundi chake, hasa mwishoni mwa juma. Mara kwa mara wakati kutaniko lote linapokutana kwa ajili ya utumishi wa shambani, kama vile baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi, kila mwangalizi wa funzo la kitabu anapaswa kushughulikia kikundi chake.
3 “Kwa Adabu na kwa Mpango”: Yule aliyepewa mgawo wa kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani anapaswa kuanza kwa wakati na kuongoza mkutano huo kwa muda wa dakika 10 au 15 tu. Ingefaa apange vikundi vya kuhubiri na kuwapa maeneo (isipokuwa waangalizi wa mafunzo ya kitabu washughulikie jambo hilo, kama ilivyotajwa mapema) kabla ya kumalizia kwa sala. Kufanya hivyo kutapunguza uhitaji wa wahubiri kukusanyika katika eneo, jambo ambalo linaweza kushusha heshima ya kazi yetu. Pia kufanya hivyo kunapatana na shauri hili la Paulo: “Acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Wote wanaohudhuria mikutano hiyo wanapaswa kufanikisha mpango huo kwa kufika kwa wakati, kushirikiana kikamili na yule anayeongoza na kuelekea kwenye eneo mara moja.
4 Kuunganishwa kwa Umoja: Mipango ya mahubiri ya vikundi hutupa fursa bora ya kuwajua wengine kutanikoni. Ijapokuwa si vibaya kupanga mapema kuhubiri na mtu mwingine, tunaweza kufaidika pia kwa kuhudhuria mikutano ya utumishi bila kupanga mapema na mtu mwingine. Huenda tukaombwa tuhubiri na mtu fulani tusiyemjua vyema, na hilo hutuwezesha ‘kupanuka’ katika upendo wetu.—2 Kor. 6:11-13.
5 Mahubiri ya vikundi hututia moyo na kutuunganisha tukiwa “wafanyakazi wenzi katika kweli.” (3 Yoh. 8) Na tushiriki kikamili katika mahubiri ya vikundi!