Kazi Ambayo Huburudisha
1 Ujumbe wa Biblia huburudisha wote ambao huukubali na kuutumia maishani mwao. (Zab. 19:7, 8) Ujumbe huo huwasaidia kuacha mafundisho ya uwongo na mazoea yenye kudhuru na hutoa tumaini lenye kutegemeka la wakati ujao. Hata hivyo, wale ambao hufaidika na habari njema si wale tu wanaozipokea. Wale ambao huwatangazia wengine kweli za Biblia zenye kuburudisha, huburudishwa pia.—Mit. 11:25.
2 Kutiwa Nguvu na Huduma: Yesu alisema kwamba wale wanaokubali kubeba nira ya kuwa wanafunzi wa Kristo, ambayo inatia ndani kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, ‘wangepata burudisho kwa ajili ya nafsi zao.’ (Mt. 11:29) Yeye mwenyewe alitiwa nguvu kwa kuwahubiria wengine. Kufanya hivyo kulikuwa kama chakula kwake. (Yoh. 4:34) Alipowatuma wanafunzi 70 kuhubiri, walifurahi walipoona Yehova akiunga mkono jitihada zao.—Luka 10:17.
3 Wakristo wengi leo hutiwa nguvu pia wanaposhiriki katika kazi ya kuhubiri. Dada mmoja alisema: “Huduma inaburudisha kwa sababu huyafanya maisha yangu yawe na kusudi. Matatizo ya kibinafsi na mikazo ya kila siku hupungua ninaposhiriki katika utumishi.” Mhudumu mwingine mwenye bidii alisema: “Huduma . . . humfanya Yehova awe halisi kwangu kila siku na hunipa amani na furaha moyoni ambazo haziwezi kupatikana vinginevyo.” Tuna pendeleo lililoje la kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”!—1 Kor. 3:9.
4 Nira ya Kristo Ni Yenye Fadhili: Ingawa Wakristo wanahimizwa ‘wajikakamue wenyewe kisulubu,’ Yesu hadai mengi kuliko yale tunayoweza kufanya. (Luka 13:24) Kwa kweli, yeye hutualika kwa upendo ‘tuchukue nira yake.’ (Mt. 11:29) Wale ambao lazima wakabiliane na magumu wanaweza kuwa na hakika kwamba utumishi wao wa nafsi yote, hata ukiwa mdogo, unampendeza Mungu.—Marko 14:6-8; Kol. 3:23.
5 Ni jambo lenye kuburudisha kama nini kumtumikia Mungu ambaye anathamini lolote tunalofanya kwa ajili ya jina lake! (Ebr. 6:10) Na tujitahidi sikuzote kumpa yaliyo bora.