Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya Mwaka wa 2004
1 Yehova huwazoeza watu wa kawaida kutimiza kazi iliyo muhimu ulimwenguni. Njia moja anayotumia kufanya hivyo ni kupitia mafundisho yanayotolewa kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma. Je, unashiriki kwa kadiri uwezavyo? Kuanzia Januari, mabadiliko machache yatafanywa ili kuwasaidia wanafunzi wanufaike zaidi na mpango huo.
2 Kazi ya Mshauri Msaidizi Itafanywa kwa Zamu: Ndugu wanaotoa hotuba za maagizo na mambo makuu ya usomaji wa Biblia wamethamini madokezo ya mshauri msaidizi. Katika makutaniko yenye wazee wengi wanaostahili, kazi ya mshauri msaidizi inaweza kufanywa kwa zamu kila mwaka. Kwa njia hiyo, wengine wanaweza kushiriki daraka hilo, na jambo muhimu zaidi ni kwamba wazee na watumishi wa huduma wanaostahili watanufaika na ujuzi wa wasemaji na walimu mbalimbali stadi.
3 Ratiba ya Pitio la Maswali na Majibu: Ikiwa kutaniko lenu lina kusanyiko la mzunguko juma la pitio, basi pitio hilo (na ratiba yote ya juma hilo) litafanywa juma linalofuata, na ratiba ya juma linalofuata itafanywa juma la kusanyiko la mzunguko. Hata hivyo, si lazima mbadili ratiba ya majuma hayo mawili ikiwa pitio linaangukia juma la ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Wimbo, hotuba ya sifa ya usemi, na mambo makuu ya usomaji wa Biblia yatafanywa kulingana na ratiba ya juma hilo. Hotuba ya maagizo (inayotolewa baada ya hotuba ya sifa ya usemi) itatoka kwenye ratiba ya juma linalofuata. Baada ya mambo makuu ya usomaji wa Biblia, Mkutano wa Utumishi utafanywa kwa nusu saa. Mkutano huo unaweza kurekebishwa ili uwe na sehemu tatu za dakika 10 kila moja au sehemu mbili za dakika 15 kila moja. (Hakupaswi kuwa na matangazo mwanzoni mwa mkutano huo.) Baada ya Mkutano wa Utumishi kutakuwa na wimbo na sehemu ya dakika 30 itakayoshughulikiwa na mwangalizi wa mzunguko. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya juma linalofuata itaanza na hotuba ya sifa ya usemi na mambo makuu ya usomaji wa Biblia kama ilivyoratibiwa, kisha kutakuwa na pitio la maswali na majibu.
4 Tumia kila fursa kufanya maendeleo ya kiroho. Unapoendelea kufaidika na elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, unawatia moyo washiriki wa kutaniko lenu, unachangia utimizo wa unabii wa Biblia, na unamletea sifa Mwanzilishi wa ujumbe mzuri ambao ni lazima tuutangaze.—Isa. 32:3, 4; Ufu. 9:19.