Kazi Inayotegemezwa na Mungu
1 Kati ya watumishi wa Mungu leo, ni wachache walio na elimu ya pekee, mali, na umaarufu katika mfumo wa sasa wa mambo. Kwa sababu hiyo, watu fulani huidharau huduma yetu. (Isa. 53:3) Hata hivyo, kazi ya elimu ya Biblia tunayofanya imewaletea mamilioni ya watu ulimwenguni pote faraja na tumaini. Watu wa kawaida wamewezaje kupata matokeo hayo makubwa? Ni kwa kutegemezwa na Mungu. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) “Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu,” akaeleza mtume Paulo, “ili aviaibishe vitu vyenye nguvu.”—1 Kor. 1:26-29.
2 Wengi kati ya mitume na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Hata hivyo, walitimiza kwa ujasiri utume wao wa kuhubiri habari njema, na Yehova alibariki jitihada zao. Licha ya vizuizi na upinzani, ‘neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi katika njia yenye nguvu.’ Kazi hiyo haingeweza kuzuiwa kwa sababu ilitegemezwa na Mungu. (Mdo. 5:38, 39; 19:20) Mambo yamekuwa vivyo hivyo siku zetu. Hata upinzani mkali kutoka kwa watawala wenye nguvu haujaweza kuzuia habari njema zisiendelee kusitawi na kukua.—Isa. 54:17.
3 Mungu Ndiye Anayestahili Sifa: Je, tujivune kwa sababu ya pendeleo letu la kuwa wahudumu wa Mungu? Sivyo hata kidogo. Akirejelea huduma ya Kikristo, Paulo alisema: “Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.” (2 Kor. 4:7) Paulo alitambua kwamba angeweza kutimiza huduma yake kwa kuwa alikuwa na nguvu kutoka kwa Mungu.—Efe. 6:19, 20; Flp. 4:13.
4 Sisi pia hutambua kwamba tunatimiza kazi ya kuhubiri kwa sababu tu ‘tumeupata msaada kutoka kwa Mungu.’ (Mdo. 26:22) Kupitia tangazo hilo la ulimwenguni pote, Yehova anatutumia kwa njia ya pekee kuyatikisa mataifa—ishara ya hukumu itakayotekelezwa karibuni. (Hag. 2:7) Tuna pendeleo kubwa kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” katika kazi kuu ya mavuno ya kiroho!—1 Kor. 3:6-9.