Muziki Unaoburudisha
1 Muziki ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli. Katika Israeli la kale, Asafu na ndugu zake waliimba: “Mshukuruni Yehova. . . . Mwimbieni, mpigieni muziki, jishughulisheni na matendo yake yote ya ajabu.” (1 Nya. 16:8, 9) Leo sisi humwimbia Yehova kwenye mikutano yetu ya kutaniko ya kila juma. (Efe. 5:19) Hiyo ni fursa nzuri sana ya kulisifu jina la Yehova!—Zab. 69:30.
2 Kusikiliza Kingdom Melodies, nyimbo za Ufalme zilizorekodiwa kwa ala peke yake, kunaweza kujaza akili zetu mambo ya kiroho. Dada mmoja alisema hivi: “Nyimbo hizo zinapopigwa, mimi huanza kukumbuka maneno yake. Hiyo ni njia bora sana ya kumkumbuka Yehova huku nikifurahia muziki!”—Flp. 4:8.
3 Pindi za Kuufurahia: Kupiga Kingdom Melodies nyumbani hutokeza hali nzuri ya kiroho ambayo huchangia amani ya familia. Familia moja iliandika hivi: “Sisi husikiliza [muziki] huo mara nyingi tukiwa nyumbani na kwenye gari, nao hautuchoshi kamwe. Mara nyingi Kingdom Melodies hututuliza akili tunapojitayarisha kwenda kwenye mikutano ya Kikristo au tunaposafiri kwenda kusanyikoni.” Dada mmoja alisema hivi: “Kusikiliza muziki huo ninapofanya kazi za nyumbani hunichangamsha kweli. Huo hunichangamsha sana ninapokunja nguo. Mimi husikiliza muziki huo ninaposhuka moyo. Lo! muziki huo huniburudisha kama nini! . . . Kila wimbo hunifanya nifurahi sana.” Je, kuna pindi ambazo muziki huo wenye kuburudisha hukusaidia?
4 Mara nyingi muziki wa leo huonyesha roho ya ulimwengu. Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wapendezwe na muziki mzuri kwa kusikiliza Kingdom Melodies. Wanafunzi wengi wa Biblia na watu wanaopendezwa watafurahi pia kujua kuhusu nyimbo hizi nzuri za kiroho ambazo humtukuza Yehova na kuchangamsha moyo.—Zab. 47:1, 2, 6, 7.