Endelea Kutambua Uharaka wa Nyakati Hizi!
1 Yesu alijua kwamba alikuwa na wakati mfupi wa kutimiza kazi ya Baba yake. (Yoh. 9:4) Kwa hiyo, alitimiza huduma yake kwa kutambua uharaka wa nyakati alimoishi, naye akawazoeza wanafunzi wake kufanya hivyo. (Luka 4:42-44; 8:1; 10:2-4) Hakutanguliza mambo ya kimwili. (Mt. 8:20) Kwa hiyo, aliweza kumaliza kazi aliyopewa na Yehova.—Yoh. 17:4.
2 Wakati Ni Mfupi: Wakati wa kuhubiri habari njema katika “dunia yote inayokaliwa” ni mfupi pia. (Mt. 24:14) Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi kwenye umalizio wa siku za mwisho. Hivi karibuni “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu . . . watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.” (2 The. 1:6-9) Hukumu hiyo itafika kwa ghafula sana. (Luka 21:34, 35; 1 The. 5:2, 3) Watu wanahitaji kutambua kwamba wako katika hali ya hatari sana. Ni daraka letu kuwasaidia watafute kibali cha Yehova maadamu kungali na wakati.—Sef. 2:2, 3.
3 Kufanya Yote Tuwezayo: Watumishi wa Mungu hutanguliza kazi ya kuhubiri wakitambua kwamba “wakati uliobaki umepungua.” (1 Kor. 7:29-31; Mt. 6:33) Baadhi yao wameacha fursa za kujiendeleza kiuchumi au kufuatilia mambo mengine ya kibinafsi ili kupanua huduma yao. (Marko 10:29, 30) Wengine wameendelea kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana” licha ya majaribu yenye kudumu. (1 Kor. 15:58) Wengi wametangaza habari njema kwa miaka mingi bila kuacha. (Ebr. 10:23) Yehova huthamini sana jitihada zote wanazofanya ili kuunga mkono Ufalme.—Ebr. 6:10.
4 Kutanguliza ibada ya Yehova, ambayo inatia ndani kuhubiri, hutusaidia kuweka karibu akilini siku ya Yehova. Jambo hilo hufanya tusikengeushwe na ulimwengu wa Shetani na huimarisha azimio letu la kudumisha mwenendo mtakatifu. (2 Pet. 3:11-14) Naam, tunaweza kuokoa uhai wetu na wa wale wanaotusikiliza tukitimiza huduma yetu kwa kutambua uharaka wa nyakati tunamoishi.—1 Tim. 4:16.