Wasaidie Watoto Wako Wafanye Maendeleo Katika Huduma
1 Wazazi Wakristo wana wajibu mzito wa kuwazoeza watoto wao kuhubiri tangu wakiwa wachanga. Wanaweza kutimiza wajibu huo kwa njia mbalimbali. Baadhi ya watoto wanaweza kukariri andiko fulani la Biblia hata kabla hawajajua kusoma. Hilo linaweza kuwavutia sana wasikilizaji. Kadiri watoto wanavyokua, ndivyo wanavyoweza kushiriki zaidi katika huduma. Ninyi wazazi, mnaweza kuwasaidiaje watoto wenu wahubiri? Mapendekezo yafuatayo yanaweza kuwasaidia.
2 Baada ya kumsalimu mwenye nyumba, unaweza kusema hivi:
◼ “Mwana wangu, [taja jina lake], ana andiko muhimu ambalo angependa ulisikie.” Mtoto wako anaweza kusema: “Andiko hili la Zaburi lilinijulisha jina la Mungu. [Mtoto asome au akariri Zaburi 83:18.] Magazeti haya yanazungumzia yale ambayo Yehova Mungu atatufanyia. Ninaweza kukuachia magazeti haya?” Unaweza kumalizia mazungumzo kwa kueleza jinsi kazi ya ulimwenguni pote inavyotegemezwa.
3 Au unaweza kujaribu njia hii:
◼ “Hujambo. Ninamzoeza binti yangu, [taja jina lake], kuwajali watu wengine katika jamii. Angependa kukupa ujumbe mfupi kutoka katika Biblia.” Binti yako anaweza kusema: “Njia moja ninayotumia kuwasaidia watu ni kuwaonyesha tumaini letu la wakati ujao ambalo linategemea Biblia. [Mtoto asome au akariri Ufunuo 21:4.] Magazeti haya yanaeleza mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatufanyia. Natumaini utafurahia kuyasoma.”
4 Kutumia utangulizi rahisi bila kuubadili-badili huwafanya watoto wawe na uhakika kwamba wanaweza kuhubiri ujumbe wa Ufalme vizuri. Mkiwa na vipindi vya mazoezi ya kusema kwa njia inayoeleweka wazi na kwa kiasi kinachofaa cha sauti, watoto wataweza kuhubiri chini ya hali mbalimbali. Kuwatayarisha vizuri na mapema, na pia kuwapongeza kwa unyoofu kutawachochea watoto wawaeleza wengine mambo wanayoamini.
5 Watoto wengi ambao wamesaidiwa jinsi hiyo wamestahili kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Tunashangilia jinsi gani kuwaona watoto wetu wakifanya maendeleo katika huduma ya Kikristo!—Zab. 148:12, 13.