Barua ya Ofisi ya Tawi
Wahubiri wa Ufalme Wapendwa:
Mwanzoni mwa mwaka mpya wa utumishi, mizunguko mitatu ilianzishwa nchini Kenya, mitatu nchini Tanzania, na mmoja nchini Burundi. Sasa eneo la Afrika Mashariki lina mizunguko 67 na wilaya 7.
Tangu mwaka wa 2000, Majumba ya Ufalme 237 yamejengwa nchini Tanzania. Mipango ya ujenzi wa ofisi ya tawi inaendelea vizuri na inatarajiwa kwamba ujenzi utaanza kabla ya mwaka huu kumalizika. Huenda Ujenzi wa ofisi ya tawi ya Burundi na ya Uganda ukamalizika mwishoni mwa mwaka huu. Tangu mwaka wa 1999, Majumba ya Ufalme 276 nchini Kenya na 20 nchini Sudan yamejengwa.
Jitihada fulani zinafanywa ili kuwahubiria viziwi habari njema. Mapainia wa pekee kadhaa wanaojua Lugha ya Ishara wametumwa katika maeneo fulani yaliyo na viziwi wengi.
Tungependa kuwashukuru ndugu na dada wengi ambao wametegemeza mipango ya kuandaa msaada mwaka huu. Wengi walisaidia kurekebisha Jumba la Ufalme la kutaniko la Juba West na kujenga nyumba ya dada fulani baada ya mlipuko huko Juba, Sudan. Pia, msaada uliandaliwa katika maeneo fulani yaliyokumbwa na ukame au mafuriko. Tuna pendeleo kubwa sana la kuwa sehemu ya tengenezo lenye upendo la akina ndugu!—1 Pet. 2:17.
Tunawapongeza sana kwa kuwa wenye bidii katika kuendeleza mambo ya Ufalme. Pia, tunawashukuru sana kwa michango ambayo mnatoa kwa ukarimu. (Met. 3:9, 10) Yehova na aendelee kubariki jitihada zetu tunapotumikia kwa umoja “kwa ajili ya sifa ya utukufu wake.”—Efe. 1:12.
Ndugu zenu,
Ofisi ya Tawi ya Burundi, Kenya, Tanzania, na Uganda