Barua Kutoka kwa Ofisi ya Tawi
Wahubiri wa Ufalme Wapendwa:
Tunafurahi kuona maendeleo katika eneo la Afrika Mashariki katika mwaka wa utumishi wa 2007! Mapainia wengi wa pekee na wa kawaida wamepewa migawo katika eneo letu, nao wanasaidia sana katika kazi ya kuhubiri. Ujenzi wa ofisi ya tawi nchini Tanzania unaendelea vizuri. Ilikuwa shangwe kubwa kuona ofisi mbalimbali za tawi zikiwekwa wakfu. Ofisi ya Burundi iliwekwa wakfu Novemba 25, 2006, Rwanda Desemba 2, 2006, na ile ya Uganda Januari 20, 2007. Sudan ilikuwa na kilele kipya cha wahubiri 1,508 katika mwezi wa Aprili. Tunahitaji kuendelea kuwakumbuka katika sala ndugu zetu nchini Eritrea. Kwa sasa ndugu 23 wako gerezani huko Eritrea na wengine kati yao wamekuwa huko kwa zaidi ya miaka 12.
Mamilioni ya nakala za trakti ya Habari za Ufalme Na. 37, “Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia!” ziligawanywa kotekote katika eneo letu. Baada ya kupokea na kusoma nakala moja, dada asiyetenda nchini Marekani alishindwa kulala. Jumapili iliyofuata, alihudhuria mkutano na kuomba funzo la Biblia. Watu wanaopendezwa walitumia sehemu iliyo nyuma ya trakti hiyo Habari za Ufalme kuomba nakala za broshua Endeleeni Kukesha! na vilevile wakaomba kufundishwa Biblia.
Kusudi la kampeni kama hizo ni kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu wajifunze kile ambacho Biblia inafundisha hasa. (Mt. 28:19, 20) Unapohubiri kumbuka kutambua upendezi wowote unaoonyeshwa, na urudi ukiwa na lengo la kuanzisha funzo la Biblia. Tunafurahi kufanya kazi bega kwa bega pamoja nanyi katika kazi hii muhimu, na tunawatumia upendo wetu mchangamfu wa Kikristo.
Ndugu zenu,
Ofisi za Tawi za Burundi, Kenya, Tanzania, na Uganda