Sanduku la Swali
◼ Ikiwa ndugu na dada wanataka kufanya arusi yao katika Jumba la Ufalme, wanapaswa kuzungumzia mambo gani pamoja na wazee?
Yehova anaheshimiwa arusi zinapopangwa kupatana na kanuni za Biblia. Arusi zinazofanywa katika Jumba la Ufalme hasa zinamletea Yehova heshima kwa sababu kupitia matukio kama haya, watu katika ujirani hujionea jinsi tengenezo la Yehova lilivyo. Ili ‘mambo yote yatendeke kwa adabu na kwa mpango,’ inafaa wazee wa kutaniko linalohusika wazungumzie mambo yanayohusu mipango ya arusi pamoja na wale ambao wameomba kufanya arusi yao katika Jumba la Ufalme.—1 Kor. 14:40.
Ndugu na dada wanaotaka kufanya arusi yao katika Jumba la Ufalme wanapaswa kuandika barua ya ombi. Barua hii inapaswa kupewa ndugu katika halmashauri ya utumishi ya mojawapo ya makutaniko yanayofanya mikutano katika jumba wanalotaka kutumia. Ni lazima wazee wapate barua hii mapema, nayo inapaswa kuonyesha tarehe na wakati wanapotaka kutumia Jumba la Ufalme. Inafaa wakumbuke kwamba wazee hawatabadili saa za mikutano kwa sababu ya arusi. Isitoshe, ni lazima bibi arusi na bwana arusi wawe wenye msimamo mzuri, yaani, ni lazima wawe wakiishi kupatana na kanuni za Biblia na sheria za uadilifu za Yehova.
Ili arusi imletee heshima Mungu wetu mtukufu, ndugu na dada wanaotaka kufunga ndoa wanapaswa kuzungumzia mipango ya arusi yao pamoja na ndugu wa halmashauri ya utumishi kabla ya kuikamilisha. Wazee hawatawalazimisha wale wanaotaka kufunga ndoa wafuate mapendezi yao ya kibinafsi, hata hivyo, ikiwa jambo lisilofaa limepangwa, marekebisho yanapaswa kufanywa. Nyimbo zilizoteuliwa katika Kingdom Melodies au zilizo katika kitabu chetu cha nyimbo ndizo tu zinazopaswa kutumiwa. Ni lazima pia wale wanaotaka kufunga ndoa waombe ruhusa wakitaka kupamba Jumba la Ufalme au kupanga viti kwa njia tofauti. Kupiga picha au kurekodi video hakupasi kuvuruga utaratibu wa arusi. Wazee wanaweza kuruhusu mazoezi ya arusi yafanywe katika Jumba la Ufalme maadamu hayaingilii mipango ya kutaniko. Kadi za mwaliko hazipaswi kubandikwa kwenye ubao wa matangazo. Hata hivyo, wazee wanaweza kutoa tangazo fupi katika Mkutano wa Utumishi kwamba kutakuwa na arusi katika Jumba la Ufalme.
Si lazima waandamani wote wa bwana na bibi arusi wawe Mashahidi waliobatizwa, hata hivyo, watu wenye mwenendo unaovunja kabisa kanuni za Biblia, au watu ambao mwenendo wao unatiliwa shaka, hawafai kuchaguliwa kuwa waandamani. Ikiwezekana, mzee Mkristo anapaswa kutoa hotuba ya arusi. Wazee Wakristo ni walimu stadi wa Neno la Mungu, kwa hiyo wao wanaweza kukazia ifaavyo kanuni za Maandiko zinazohusika katika tukio hili muhimu. (1 Tim. 3:2) Kwa kawaida nadhiri za ndoa zinashughulikiwa na ndugu ambaye amepewa mamlaka kisheria kuandikisha ndoa.
Kwa kuwa, sifa ya mzee Mkristo anayetoa hotuba inaweza kuathiriwa, mzee huyo anapaswa pia kuelezwa mapema kuhusu mipango ya arusi. Atazungumza na ndugu na dada wanaotaka kufunga ndoa na kuwauliza kuhusu mwenendo wao wa maadili wakati wa uchumba, nao wanapaswa kumjibu waziwazi na kwa unyofu. Ni lazima bibi arusi au bwana arusi aliyekuwa amefunga ndoa hapo awali athibitishe kwamba yuko huru, Kimaandiko na kisheria, kufunga ndoa. (Mt. 19:9) Kati ya mambo mengine, anapaswa kumwonyesha yule mzee nakala ya hati ya talaka.
Arusi itakuwa pindi ya furaha kwa wote, ikiwa ndugu na dada wanaotaka kufunga ndoa watawasiliana waziwazi na wazee, na kushirikiana nao kikamili.—Met. 15:22; Ebr. 13:17.