Kampeni ya Pekee ya Kutangaza Ukumbusho!
1. Wahubiri wa Ufalme watafanya nini ulimwenguni pote kuanzia Machi 21, 2009, na kwa nini?
1 Waabudu wa Yehova Mungu ulimwenguni pote watakusanyika siku ya Alhamisi, Aprili 9, 2009 kutafakari tendo kuu linaloonyesha upendo wake kwa wanadamu. (Rom. 5:6-8) Tunatazamia kwa hamu kuwa pamoja na mamilioni ya watu wanaopendezwa tunapoadhimisha kifo cha Yesu. Mwaliko wa pekee wa Ukumbusho utasambazwa duniani kote kuanzia Machi 21.
2. Unapaswa kukumbuka mambo gani unapotoa mwaliko?
2 Mambo ya Kukumbuka: Tumia kikamili picha, maswali, na maandiko yanayoonyeshwa kwenye mwaliko. Kwa mfano, unaweza kuonyesha picha kwenye ukurasa wa kwanza na kusema: “Ningependa kukualika uadhimishe pamoja nasi kifo cha Yesu siku ya Alhamisi, Aprili 9, 2009.” Kisha umwonyeshe kichwa cha mwaliko na maswali ambayo yameorodheshwa. Usikose kukazia kwamba mwenye nyumba anaweza kuwaalika watu wa familia yake na mtu mwingine yeyote ambaye angependa kuja naye.
3. Unaweza kufanya nini ili uhakikishe kwamba watu uliowaalika mwanzoni mwa kampeni hawasahau mwaliko huo?
3 Ikiwa kutaniko lenu lina eneo kubwa, wazee wanaweza kuwaambia mwache mialiko kwenye nyumba zisizo na watu. Jumamosi na Jumapili, toeni magazeti pamoja na mialiko hiyo. Uwe na lengo la kualika watu unaowarudia, mafunzo ya Biblia, watu wa ukoo, wanafunzi wenzako, wafanyakazi wenzako, majirani, na watu wengine unaojuana nao. Mwaka uliopita, dada mmoja aliwaalika watu wake wa ukoo 30 kwenye Ukumbusho, kisha akawakumbusha mara kwa mara umuhimu wa tukio hilo. Alifurahi kama nini watu 25 walipohudhuria, na baadaye 4 kati yao wakakubali kujifunza Biblia!
4. Tunapaswa kufanya mipango gani sasa, na kwa nini?
4 Fanya Mipango Sasa: Wahubiri wengi wanaweza kupanua utumishi wao katika miezi ya Machi na Aprili. Ikiwa una watoto au wanafunzi wa Biblia ambao wanafanya maendeleo, huu ni wakati mzuri wa kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Sasa ndio wakati wa kuanza kujitayarisha kushiriki kikamili katika kampeni hii inayotangaza maadhimisho ya kukumbuka wonyesho mkuu zaidi wa upendo kutoka kwa Yehova na Yesu.—Yoh. 3:16; 15:13.