“Wakeni Roho”
1. Tunapaswa kuwa na sifa gani tunapohubiri?
1 Tunapaswa kuwa na bidii katika sehemu zote za utumishi wetu wa Kikristo. Kwa hiyo, tunahimizwa ‘kuwaka roho’ na ‘kumtumikia Yehova.’ (Rom. 12:11) Hata hivyo, kuna mambo mengi yanayoweza kupunguza bidii yetu katika utumishi. Tunawezaje ‘kuichochea kama moto’ bidii na shauku yetu ya kuhubiri Ufalme?—2 Tim. 1:6, 7.
2. Kuna uhusiano gani kati ya funzo la kibinafsi la Biblia na bidii katika huduma?
2 Funzo la Kibinafsi la Biblia: Mhubiri wa Ufalme mwenye mafanikio anapenda sheria ya Mungu na anaguswa moyoni na kweli zinazopatikana humo. (Zab. 119:97) Tunapojifunza kweli za Biblia wakati wa funzo letu la kibinafsi, moyo wetu unachochewa na bidii yetu inaongezeka. Upendo kwa Yehova anayetuandalia kweli hizo na tamaa yetu ya kuwahubiria wengine habari njema, inatusukuma tumsifu na tutangaze jina lake hadharani. (Ebr. 13:15) Tunapohubiri habari njema kwa bidii tunaonyesha kwamba tunaithamini sana.
3. Roho ya Mungu inaweza kutusaidiaje katika huduma?
3 Mwombe Mungu Akupe Roho Takatifu: Mafanikio katika huduma hayatokani na jitihada zetu tu. Bidii katika utumishi inatokana na roho ya Mungu inapofanya kazi bila kuzuiwa. (1 Pet. 4:11) Kwa kumkaribia Mungu aliye Chanzo cha nguvu zote, tunaimarishwa kiroho ili tuhubiri kwa ujasiri. (Isa. 40:26, 29-31) Mtume Paulo alipokabili uhasama katika huduma yake, alipata “msaada kutoka kwa Mungu.” (Mdo. 26:21, 22) Roho ya Yehova yenye kutia nguvu inaweza kutusaidia kuwa na bidii katika huduma, kwa hiyo, tunapaswa kumwomba atupe roho yake.—Luka 11:9-13.
4. Bidii inaweza kuwa na matokeo gani mazuri, lakini tunatahadharishwa kuhusu nini?
4 Mkristo anapokuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme, mara nyingi Wakristo wenzake huchochewa wawe na bidii vilevile. (2 Kor. 9:2) Yamkini watu wengi zaidi katika eneo watakuwa tayari kusikiliza ujumbe unaotolewa kwa shauku na kwa usadikisho. Hata hivyo, mbali na kuhubiri kwa bidii tunapaswa pia kuwa wapole na wenye busara. (Tito 3:2) Nyakati zote tunapaswa kumheshimu mwenye nyumba na hiari yake ya kuchagua.
5. Katika Neno la Mungu tunahimizwa tufanye nini?
5 Tuwe wenye ‘kuwaka roho’ sikuzote tunapotangaza Ufalme. Na tuchochee bidii yetu kwa kujifunza Biblia na kwa kutoa sala ya moyoni kwa Yehova, ambaye anaweza kutupa roho yake takatifu inayotia nguvu. Tunapofanya hivyo, tunaweza kutimiza huduma yetu kwa bidii na “kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu.”—1 The. 1:5.