Je, Utaiga Bidii ya Yehova na Yesu Katika Majira Haya ya Ukumbusho?
1. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya nini katika majira ya Ukumbusho?
1 Yehova ana bidii katika kutimiza kusudi lake. Andiko la Isaya 9:7 linasema hivi kuhusu baadhi ya baraka za Ufalme wa Mungu: “Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.” Vivyo hivyo, katika huduma yake hapa duniani Mwana wa Mungu alikuwa na bidii sana katika ibada ya kweli. (Yoh. 2:13-17; 4:34) Kila mwaka katika majira ya Ukumbusho, mamilioni ya wahubiri ulimwenguni pote hujitahidi sana kuiga bidii ya Yehova na Yesu kwa kuongeza utendaji wao katika huduma. Je, utakuwa mmoja wao?
2. Bidii itatuchochea kufanya nini kuanzia Machi 7?
2 Kampeni ya Ukumbusho: Mwaka huu kampeni ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho itaanza Jumamosi, Machi 7. Panga sasa kushiriki kwa bidii katika huduma. Wahubiri watafurahia kuwaalika kwa bidii watu wengi iwezekanavyo katika eneo. Jitahidi kuwaalika wanafunzi wa Biblia, watu wanaopendezwa, wafanyakazi wenzako, watu wako wa ukoo, na wanafunzi wenzako, kwa kuwapa mwaliko au kwa kutumia Tovuti yetu ya jw.org/sw.
3. Tunaweza kupanuaje huduma yetu katika mwezi wa Machi na Aprili?
3 Fanya Upainia Msaidizi: Bidii itatuchochea pia kupanua huduma yetu. Bila shaka wahubiri wengi wataweza kufanya upainia msaidizi katika miezi ya Machi na Aprili, kwa sababu tutakuwa na nafasi ya kuchagua takwa la saa 30. Katika ibada yenu ya familia au funzo la kibinafsi, sali kuhusu jinsi ya kutimiza jambo hilo. (Met. 15:22) Wengine watachochewa kushiriki kwa bidii katika kampeni hiyo ikiwa tuna bidii ya kuwaalika watu. Ukifanya mabadiliko ili utimize mengi zaidi katika huduma yako, utakuwa unaiga bidii ya Yesu.—Marko 6:31-34.
4. Tutapata baraka gani tukiiga bidii ya Yehova na Yesu?
4 Tukiiga bidii ya Yehova na Yesu katika majira haya ya Ukumbusho tutapata baraka nyingi. Watu wengi zaidi katika eneo letu watahubiriwa. Tutapata shangwe na uradhi kwa kumtumikia Yehova na kuwasaidia wengine. (Mdo. 20:35) Zaidi ya yote, tutamfurahisha Mungu wetu mwenye bidii na Mwana wake.