Sisi Ni Mashahidi Wakati Wote
1. Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi kumhusu Yesu akimhubiria mwanamke kisimani?
1 Yesu alikuwa ametembea kwa muda wa saa nyingi. Alikuwa amechoka na mwenye kiu. Wanafunzi wake walipoenda kununua chakula, aliketi kwenye kisima nje ya jiji la Samaria ili apumzike. Yesu hakuwa ameenda Samaria kuhubiri; alipita tu katika eneo hilo akiwa safarini kwenda Galilaya ili kuendelea na huduma yake huko. Hata hivyo, alitumia fursa hiyo kumhubiria mwanamke aliyekuja kuteka maji. (Yoh. 4:5-14) Kwa nini Yesu alifanya hivyo? Kwa sababu nyakati zote Yesu alikuwa “shahidi mwaminifu na wa kweli” wa Yehova. (Ufu. 3:14) Tunamwiga Yesu kwa kuendelea kuwa Mashahidi wa Yehova wakati wote.—1 Pet. 2:21.
2. Tunaweza kujitayarishaje kuhubiri isivyo rasmi?
2 Jitayarishe: Tunaweza kujitayarisha kuhubiri isivyo rasmi kwa kubeba vitabu, magazeti, trakti, na kadhalika. Wahubiri wengi hubeba trakti na huwaachia wahudumu wa maduka na wa vituo vya mafuta, au watu wengine wanaokutana nao katika shughuli zao za kila siku. (Mhu. 11:6) Dada ambaye anasafiri mara nyingi huhakikisha kwamba amebeba Biblia ndogo na kitabu Biblia Inafundisha katika kibeti chake, naye hujaribu kuanzisha mazungumzo na wale walioketi karibu naye.
3. Tunaweza kuanzishaje mazungumzo?
3 Kuanzisha Mazungumzo: Tunapohubiri isivyo rasmi, si lazima tuanzishe mazungumzo kwa kutaja jambo fulani katika Biblia. Yesu hakuanzisha mazungumzo na yule mwanamke kwenye kisima kwa kujitambulisha kuwa Masihi. Alimwomba tu ampe maji ya kunywa, na kwa njia hiyo akaanzisha mazungumzo pamoja na mwanamke huyo. (Yoh. 4:7-9) Dada mmoja ameona kwamba kutumia njia kama hiyo humwezesha kuanzisha mazungumzo anapoulizwa kama alisherehekea sikukuu fulani. Badala ya kusema hakusherehekea kwa sababu yeye ni Shahidi wa Yehova, yeye husema, “Mimi binafsi niliamua nisisherehekee.” Aliyeuliza swali hilo hutaka kujua sababu, na dada huyo hupata nafasi ya kumtolea ushahidi.
4. Kwa nini andiko la Mathayo 28:18-20 linakuchochea?
4 Ingawa Yesu alimaliza huduma yake ya bidii duniani, bado anapendezwa sana na kazi ya kuhubiri inayofanywa jinsi alivyoifanya. (Mt. 28:18-20) Kwa hiyo, kwa kuiga kielelezo cha Yesu, sisi ni Mashahidi walio tayari kutangaza hadharani imani yetu wakati wowote.—Ebr. 10:23.