Jinsi ya Kuwazoeza Wahubiri Wapya Katika Utumishi
1. Ulihisije uliposhiriki katika huduma kwa mara ya kwanza?
1 Je, unakumbuka ulipoenda nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza? Yaelekea ulikuwa na wasiwasi mwingi. Iwapo ulihubiri pamoja na mwalimu wako wa Biblia au mhubiri mwingine, bila shaka ulithamini msaada wake. Sasa umepata uzoefu fulani katika huduma, kwa hiyo, unaweza kusaidia kuwazoeza wahubiri wapya.
2. Wahubiri wapya wanahitaji kufunzwa nini?
2 Wahubiri wapya wanahitaji kufunzwa jinsi ya kuanzisha mazungumzo pamoja na wenye nyumba, kutumia Biblia wanapohubiri nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia, na kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Wanapaswa pia kufunzwa jinsi ya kutoa ushahidi kwa njia mbalimbali, kama vile kuwahubiria watu katika maeneo ya biashara na barabarani. Unaweza kuwasaidia kufanya maendeleo kwa mfano wako mzuri, na kwa kuwapa mapendekezo.
3. Tunaweza kuwasaidia wengine jinsi gani kwa mfano wetu mzuri?
3 Wafundishe kwa Mfano Wako: Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake jinsi ya kuhubiri. (Luka 8:1; 1 Pet. 2:21) Unapopanga kuhubiri pamoja na mhubiri mpya, tayarisha maelezo rahisi ambayo anaweza kuiga. Labda unaweza kutumia pendekezo moja katika vitabu vyetu. Kisha, ujitolee kuhubiri kwenye mlango wa kwanza, au kwenye milango kadhaa, ili mhubiri huyo mpya asikie mambo unayoyasema. Mnapoondoka kwenye nyumba moja na kuelekea nyumba nyingine, unaweza kumwuliza maoni yake kuhusu njia yako ya kuhubiri. Hili litamsaidia kuona umuhimu wa kushiriki katika huduma pamoja na wahubiri wengine, na kumsaidia pia kukubali mapendekezo yoyote yale ambayo utampa baada ya yeye kumhubiria mwenye nyumba.
4. Tunaweza kumsaidia mhubiri mpya jinsi gani baada ya kumsikiliza akimhubiria mwenye nyumba?
4 Wape Mapendekezo: Yesu aliwapa pia wanafunzi wake maagizo kuhusu jinsi ya kuhubiri. (Mt. 10:5-14) Wewe unaweza kuwasaidia wahubiri wapya kwa njia kama hiyo. Sikiliza kwa makini anapozungumza na mwenye nyumba. Halafu, mnapoondoka na kuelekea nyumba nyingine, mpongeze kwa moyo mweupe na utaje mambo hususa aliyofanya vizuri, hata kama umetambua kwamba anahitaji kuboresha sehemu fulani za mazungumzo yake. Kabla ya kumpa pendekezo lolote, huenda ikawa jambo la hekima kungoja ili kuona kama ameboresha mazungumzo yake kwenye mlango unaofuata. Labda alishikwa na wasiwasi tu. Kumbuka pia kwamba wahubiri wana vipawa tofauti-tofauti, na mara nyingi kuna njia zaidi ya moja za kufanya jambo.—1 Kor. 12:4-7.
5. Tunaweza kusema nini tunapochukua hatua ya kumpa mhubiri mpya mapendekezo?
5 Nyakati nyingine, mhubiri mpya ataomba mapendekezo. Lakini asipofanya hivyo, chukua hatua ya kumsaidia. Unawezaje kufanya hivyo kwa busara? Baadhi ya wahubiri wenye uzoefu huuliza, “Ungependa nikupe pendekezo?” au, “Unaonaje mazungumzo yako katika nyumba hiyo?” Ama unaweza kusema, “Nilipokuwa mhubiri mpya, ilikuwa vigumu sana kwangu ku- . . . , lakini jambo hili lilinisaidia sana. . . . ” Nyakati nyingine inafaa kuchunguza kitabu Kutoa Sababu pamoja. Mpe mapendekezo kuhusu jambo moja tu ili asilemewe.
6. Maneno “chuma hunolewa kwa chuma” yanahusisha huduma yetu kwa njia gani?
6 Chuma Hunolewa kwa Chuma: Timotheo, ambaye alikuwa mhubiri stadi, alitiwa moyo na Paulo kufanya maendeleo ya kiroho na kuendelea kufundisha kwa bidii. (1 Tim. 4:13, 15) Hata ingawa miaka mingi imepita tangu ulipoenda nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza, hupaswi kamwe kuacha kuboresha uwezo wako wa kuhubiri. Jifunze kutokana na wahubiri wenzako, hata wale wasio na uzoefu mwingi, na uwe macho kuwasaidia wengine kwa fadhili, hasa wahubiri wapya, ili wawe wahudumu stadi wa habari njema.—Met. 27:17.