Je, Jicho Lako Ni Rahisi?
1. Inamaanisha nini kuwa na ‘jicho rahisi’?
1 Matendo yetu yanaongozwa na mambo ambayo macho yetu yanakazia. Hivyo, maneno haya ya Yesu yanafaa sana: “Basi, ikiwa jicho lako ni rahisi, mwili wako wote utakuwa mwangavu”! (Mt. 6:22) Tunapokuwa na jicho “rahisi,” kulingana na maneno ya Yesu, tunazingatia kusudi moja maishani, yaani, kufanya mapenzi ya Mungu. Tunatanguliza Ufalme maishani na hatukengeushwi na vitu vya kimwili visivyo vya lazima wala shughuli nyingine ambazo huvuruga utumishi wetu.
2. Maoni yetu yanaweza kupotoshwa na nini, lakini nini kinachoweza kutusaidia?
2 Uhitaji wa Kujichunguza: Mtazamo wetu wa vitu tunavyohitaji unaweza kupotoshwa na matangazo ya vyombo vya habari, au tamaa ya kuwa na vitu ambavyo wengine wanavyo. Kabla ya kununua kitu chochote au kufanya jambo lolote ambalo linahitaji wakati mwingi, pesa nyingi, au nguvu nyingi, ni vizuri “kuhesabu gharama” kwa kujiuliza, ‘Je, kitu hiki au jambo hili litaboresha huduma yangu kwa Yehova au litanizuia nisitimize huduma hiyo kikamili?’ (Luka 14:28; Flp. 1:9-11) Pia, ni jambo la hekima kuchunguza mara kwa mara jinsi tunavyoweza kurahisisha maisha yetu ili tufanye mengi zaidi katika huduma.—2 Kor. 13:5; Efe. 5:10.
3. Tunajifunza nini kutokana na dada ambaye alifanya mabadiliko na kurahisisha maisha yake?
3 Wakati dada fulani alipoanza upainia wa kawaida, aliamua kuendelea na kazi yake ya wakati wote ingawa angeweza kujikimu kwa kufanya kazi ya muda. Mwishowe, alikata kauli hii: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili. Ilibidi nijinyime vitu visivyo vya lazima na kuridhika na mahitaji ya lazima tu. Nilitambua kuwa tamaa yetu ya vitu vya kimwili huisha baada ya kuvipata vitu hivyo na kuvifuatia wakati wote kungenichosha sana.” Hali zake zilimruhusu kufanya mabadiliko na kurahisisha maisha yake. Alibadili kazi yake pia, na hivyo, akaweza kuendelea na upainia.
4. Kwa nini ni muhimu sana kwetu kudumisha jicho rahisi?
4 Kwa kuwa mwisho unakaribia sana, ni muhimu sana kwetu kudumisha jicho rahisi. Kadiri siku zinavyopita, ndivyo tunavyokaribia mwisho wa ulimwengu huu na mwanzo wa ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Kor. 7:29, 31) Kwa kuzingatia kazi yetu ya kuhubiri, tunaweza kujiokoa sisi wenyewe, na wale wanaotusikiliza.—1 Tim. 4:16.