Onyesha “Huruma Nyororo”
1. Watu wanahitaji nini sana leo?
1 Hakuna wakati mwingine wowote katika historia ambapo watu wamehitaji sana kusaidiwa kwa huruma kama wakati huu. Hali za ulimwengu zinazoendelea kuzorota zimewafanya wengi wakose furaha, washuke moyo, na kukosa tumaini. Mamilioni wanahitaji msaada, nasi tukiwa Wakristo tunaweza kuonyesha kwamba tunawahangaikia jirani zetu kikweli. (Mt. 22:39; Gal. 6:10) Tunaweza kufanyaje hivyo?
2. Ni njia gani iliyo bora kwetu kuonyesha huruma?
2 Kazi Inayohusisha Sifa ya Huruma: Mungu ndiye chanzo pekee cha faraja ya kweli na ya kudumu. (2 Kor. 1:3, 4) Yehova anatuhimiza tumwige kwa kuwa wenye “huruma nyororo,” na ametupa kazi ya kuwatembelea jirani zetu tukiwa na habari njema ya Ufalme. (1 Pet. 3:8) Kushiriki kwa bidii katika kazi hii ndiyo njia bora tunayotumia kuwafariji “waliovunjika moyo,” kwa sababu Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la kweli kwa wanadamu wanaoteseka. (Isa. 61:1) Kwa sababu ya huruma zake kwa watu wake, hivi karibuni Yehova atachukua hatua ya kuondolea mbali uovu na kufanyiza ulimwengu mpya wenye uadilifu.—2 Pet. 3:13.
3. Ni kwa njia gani tunaweza kuwaona watu kama Yesu alivyowaona?
3 Waone Watu Kama Yesu Alivyowaona: Hata alipokuwa akihubiria umati mkubwa wa watu, Yesu hakuwaona kuwa kikundi tu. Aliwaona wakiwa watu mmoja-mmoja waliokuwa na uhitaji wa kiroho. Walikuwa kama kondoo bila mchungaji wa kuwaongoza. Mambo aliyoyaona yalimgusa Yesu moyo, naye akachochewa kuwafundisha kwa subira. (Marko 6:34) Tukiwaona watu kama Yesu alivyowaona, tutachochewa kuwaonyesha huruma ya kweli wakiwa mtu mmoja-mmoja. Hilo litaonekana wazi katika njia yetu ya kuongea na ishara zetu za uso. Tutatanguliza kazi ya kuhubiri, na kubadili maneno yetu yafaane na mahangaiko ya kila mmoja.—1 Kor. 9:19-23.
4. Kwa nini tunapaswa kujivika sifa ya huruma?
4 Umati mkubwa wa watu kutoka katika mataifa yote wanaukubali ujumbe wa Ufalme na hangaiko lenye upendo wanaloonyeshwa. Tunapoendelea kujivika sifa ya huruma, tunamheshimu na kumfurahisha Yehova, Mungu wetu mwenye huruma.—Kol. 3:12.