Sarafu Mbili Zenye Thamani Ndogo
Njia moja muhimu ya kutegemeza mambo ya Ufalme ni kwa kutoa michango kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote. Namna gani ikiwa hatuna pesa nyingi?
Pindi moja, Yesu alimwona mjane mmoja maskini akitoa mchango wa sarafu mbili zenye thamani ndogo katika sanduku la hazina hekaluni. Upendo kwa Yehova ulimsukuma mjane huyo kutoa “kutokana na uhitaji wake, . . . vyote alivyokuwa navyo, riziki yake yote.” (Marko 12:41-44) Kwa kuwa Yesu alitambua jambo hilo, ni wazi kwamba mchango wa mjane huyo ulikuwa wenye thamani kubwa machoni pa Mungu. Vivyo hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza hawakuona daraka la kuitegemeza kifedha huduma kuwa pendeleo la Wakristo matajiri tu. Mtume Paulo alitaja mfano wa ndugu wa Makedonia ambao licha ya ‘umaskini mkubwa, waliendelea kuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili.’—2 Kor. 8:1-4.
Hivyo basi, ikiwa tunaweza tu kutoa mchango wa ‘sarafu mbili zenye thamani ndogo,’ tunapaswa kukumbuka kwamba mchango huo mdogo ukijumlishwa na mwingine unaweza kuwa kiasi kikubwa. Tunapotoa kutoka moyoni, tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni aliye mkarimu, kwa kuwa “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Kor. 9:7.