Je, Uko Tayari Kubadilika Kulingana na Hali?
1. Mabadiliko yanayotukia ulimwenguni yanatulazimu tufanye marekebisho gani?
1 Kwenye andiko la 1 Wakorintho 7:31, Biblia inalinganisha ulimwengu na jukwaa lenye tamasha na waigizaji wanaobadilika badilika. Mabadiliko yanayotukia ulimwenguni yanatulazimu turekebishe mara kwa mara njia zetu za kuhubiri, ratiba yetu, na njia yetu ya kuwafikia watu. Je, uko tayari kubadilika kulingana na hali?
2. Kwa nini tunapaswa kubadilika kulingana na hali ili twende sambamba na tengenezo?
2 Njia Zako za Kuhubiri: Sikuzote kutaniko la Kikristo limekuwa likibadilika kulingana na hali. Mwanzoni Yesu alipowatuma wanafunzi wake, aliwaambia wasichukue mfuko wa chakula au pesa kwa ajili ya mikoba yao. (Mt. 10:9, 10) Hata hivyo, baadaye alirudia maagizo hayo akitarajia kuwa wakati ujao wanafunzi wake wangetendewa kwa ukatili na kazi ya kuhubiri ingeenea katika maeneo mengine. (Luka 22:36) Katika karne iliyopita, tengenezo la Yehova lilitumia njia mbalimbali za kuhubiri kulingana na mahitaji ya wakati huo. Njia hizo ni kama vile kadi za kutoa ushahidi, matangazo ya redio, na magari yenye vikuza-sauti. Leo, mbali na huduma yetu ya nyumba kwa nyumba, tumetiwa moyo kuhubiri zaidi hadharani na isivyo rasmi kwa sababu watu katika maeneo mengi hawapatikani sana nyumbani. Pia, tumetiwa moyo kuhubiri nyumba kwa nyumba jioni ikiwa watu hawapatikani nyumbani wakati wa mchana. Gari la kimbingu la Yehova linapobadili mwendo wake, je, wewe unaenda sambamba na gari hilo?—Eze. 1:20, 21.
3. Kubadilika kulingana na hali hutusaidiaje kupata matokeo mazuri zaidi kwenye eneo letu?
3 Jambo Utakalozungumzia: Watu katika eneo lenu wanahangaishwa na nini? Uchumi? Familia? Vita? Ni vizuri tujue matatizo na hali za sasa zilizo katika eneo letu ili tuweze kutayarisha jambo linalofaa la kuzungumzia. (1 Kor. 9:20-23) Wenye nyumba wanapojieleza, badala ya kuwaitikia kidesturi na kuendelea kuzungumzia jambo tulilopanga kuwaeleza, ni afadhali zaidi kubadilika kulingana na hali na kuzungumzia mambo yanayowahangaisha.
4. Kwa nini tunapaswa kuwa wepesi wa kubadilika kulingana na hali?
4 Hivi karibuni “tamasha” ya mwisho ya ulimwengu huu itafikia mwisho, na dhiki kuu itaanza. “Wakati uliobaki umepungua.” (1 Kor. 7:29) Hivyo, ni muhimu sana tubadilike kulingana na hali bila kukawia, ili tuweze kutimiza mambo mengi zaidi katika muda mchache uliobaki!