Tutaanza Kujifunza Kitabu Mkaribie Yehova Juma Linaloanza Januari 6
1. Kuanzia juma la Januari 6, tutapata fursa gani za kumkaribia Yehova?
1 Yehova anataka tumkaribie. (Yak. 4:8) Ili kutusaidia kufanya hivyo, kuanzia juma linaloanza Januari 6, tutajifunza kitabu Mkaribie Yehova katika funzo la Biblia la Kutaniko. Kuhusu kusudi la kitabu hicho, maneno ya utangulizi yanasema: “Tukitafakari juu ya jinsi Yehova anavyodhihirisha kila mojawapo ya sifa zake, jinsi Yesu Kristo alivyodhihirisha sifa hizo kikamili, na kufahamu jinsi sisi pia tunavyoweza kusitawisha sifa hizo, tutamkaribia Mungu zaidi.” Mara ya kwanza kitabu hicho kilizungumziwa makutanikoni mwaka wa 2004 na 2005. Hata hivyo, kwa walio wengi kati ya wahubiri milioni mbili hivi ambao wamebatizwa tangu wakati huo, itakuwa mara yao ya kwanza kuona sifa za Yehova zikizungumziwa kwa kina. Kwa wale ambao walijifunza kitabu hicho, kujifunza tena, kutawasaidia wathamini zaidi sifa za Yehova.—Zab. 119:14.
2. Tutatumia utaratibu gani kujifunza kitabu Mkaribie Yehova?
2 Utaratibu wa Kujifunza: Ndugu anayeongoza ataanza kwa utangulizi mfupi, labda sentensi moja au mbili. Kitabu hakionyeshi maandiko hususa yanayopaswa kusomwa, hivyo ndugu anayeongoza atachagua maandiko yanayopaswa kusomwa. Kupitia mambo makuu, ndugu anayeongoza anaweza kuuliza swali moja au mawili mwishoni mwa kila somo. Ikiwa habari itatia ndani sanduku “Maswali ya Kutafakari,” maswali hayo yatatumiwa kukazia mambo makuu. Wakati ukiruhusu, ndugu anayeongoza anaweza kuwaomba wasikilizaji wasome maandiko yaliyoonyeshwa kwenye sanduku na kisha aulize maswali ya ziada.
3. Tunapojifunza kitabu hicho, tunapaswa kufanya nini na kwa nini?
3 Faidika Kikamili: Jitayarishe mapema hata kama umewahi kujifunza kitabu hicho. Shiriki kutoa maelezo, kwani kufanya hivyo kutamletea Yehova sifa, kutakusaidia kukumbuka habari hiyo, na kuwanufaisha wahudhuriaji wengine. (Zab. 35:18; Ebr. 10:24, 25) Unapotafakari sifa za Yehova zisizo na kifani, utamkaribia zaidi. (Zab. 77:11-13) Matokeo ni kwamba, utaazimia kabisa kutii amri za Yehova na utachochewa zaidi kuwaambia wengine kuhusu sifa zake.—Zab. 150:1-6.