Sanduku La Swali
◼ Watoto wanapaswa kujifunza nini ili wafikie ukomavu wa kiroho?
Wazazi Wakristo hujitahidi kuwalea watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Kwa mfano, wazazi wameona kwamba kuna manufaa ya kuchunguza andiko la siku pamoja na watoto wao kila asubuhi. Wanapofanya ibada ya familia au katika pindi nyingine, familia zinaweza kuangalia video pamoja, kuzungumzia habari hususa kutoka kwenye makala za Vijana Huuliza, kuigiza masimulizi ya Biblia, au kufanya mazoezi kuhusu hali ambazo huenda wakakabili. Hata hivyo, ili watoto waweze ‘kusonga mbele kufikia ukomavu,’ ni lazima wafundishwe Biblia kwa kina zaidi.—Ebr. 6:1.
Fikiria mambo tunayowafundisha watu katika eneo letu. Kwa kawaida sisi hujitahidi kuanzisha funzo la Biblia katika ziara ya kwanza au katika ziara ya kurudia, kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Baada ya kumaliza kitabu hicho, tunatumia kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu.” Kwa nini? Kwa sababu kitabu Biblia Inafundisha huwapa wanafunzi ujuzi wa msingi wa Maandiko. Kitabu “Upendo wa Mungu” huwafundisha jinsi ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha yao ya kila siku. Kujifunza vitabu hivyo viwili huwasaidia wapya ‘watie mizizi’ katika Kristo na “kuimarishwa katika imani.” (Kol. 2:6, 7) Bila shaka watoto wako pia watanufaika wakijifunza vitabu hivyo. Wanapaswa kufundishwa kuhusu fidia, Ufalme, na hali ya wafu. Wanapaswa kujua kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na jinsi ya kutambua siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Ni lazima wasadiki kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofundisha kweli. Pia, watoto wanapaswa kuelewa kanuni za Biblia na jinsi ya kuzoeza “nguvu zao za ufahamu.” (Ebr. 5:14) Bila shaka, wazazi wanapaswa kuzingatia umri na uwezo wa watoto wao wa kuelewa mambo. Hata hivyo, watoto wengi wanaweza kujifunza Biblia kwa kina hata wanapokuwa wenye umri mdogo sana.—Luka 2:42, 46, 47.
Ili kuwasaidia wazazi, Tovuti ya jw.org/sw itakuwa na miongozo inayotegemea kitabu Biblia Inafundisha. Familia zinaweza kupata miongozo hiyo kwenye Tovuti yetu kwa kutazama chini ya MAFUNDISHO YA BIBLIA > MATINEJA. Wakati ujao, miongozo zaidi ya kujifunza inayotegemea kitabu “Upendo wa Mungu” itaandaliwa. Bila shaka, nakala zilizochapwa za vitabu hivyo zinaweza kutumiwa. Wazazi wanaweza kuamua ikiwa watatumia habari hizo katika Ibada yao ya Familia, wanapojifunza Biblia na mmoja wa watoto wao, au wanapomzoeza mtoto wao kufanya funzo la kibinafsi.