Tenda kwa Uharaka
Tangu kuboreshwa kwa Tovuti yetu, kumekuwa na ongezeko kubwa sana la wanaotumia Tovuti hiyo kuomba kujifunza Biblia. Pia, kupitia njia nyinginezo za kutoa ushahidi hadharani, wengi wameomba kujifunza Biblia. Ofisi ya tawi hushughulikia maombi hayo mara tu baada ya kuyapokea. Kwa mfano, ikiwa ombi limefanywa kupitia Tovuti yetu ya jw.org, wazee katika eneo la anayependezwa hupokea taarifa kutoka ofisi ya tawi siku mbili tu baadaye. Hata hivyo, ripoti kutoka kwenye maeneo zinaonyesha kwamba, baadhi ya watu wanaoomba kujifunza Biblia hawajafikiwa kwa majuma kadhaa. Tunawezaje kuhakikisha kwamba tunawasaidia watu hao kabla hamu yao ya kujifunza haijaanza kupungua?—Marko 4:14, 15.
Ikiwa mtu anayependezwa haishi katika eneo lako, bila kukawia jaza fomu Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) na umpe mwandishi katika mkutano unaofuata. Kisha mwandishi anapaswa kuwasilisha habari hizo kwenye ofisi ya tawi ndani ya siku moja au mbili kwa kutumia tabo ya Kutaniko kwenye jw.org. Wazee wanapaswa kuangalia Tovuti yetu kila wakati. Wakipokea taarifa kwamba mtu fulani katika eneo anapendezwa, wanapaswa kumfuatilia haraka. Mhubiri yeyote anayeombwa kumtembelea anapaswa kutanguliza jambo hilo. Ikiwa hampati mtu huyo nyumbani, mhubiri anaweza kumwachia ujumbe mfupi unaoonyesha jinsi aliyependezwa anavyoweza kuwasiliana naye.