KICHWA CHA MWEZI HUU: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.”—2 Tim. 4:2.
Tumia Fursa Unazopata Kueneza Ujumbe wa Ufalme!
1. Tunajifunza somo gani kutokana na mfano wa Daudi?
1 Mfalme Daudi hakuruhusu hali alizokabili zimzuie kutenda. Kwa mfano, Daudi alitaka kujenga nyumba ya Yehova. Alipozuiwa kufanya hivyo, Daudi alibadili miradi yake na kufanya matayarisho ili Sulemani ajenge hekalu. (1 Fal. 8:17-19; 1 Nya. 29:3-9) Badala ya kuhangaikia jambo ambalo hangeweza kufanya, Daudi alikazia fikira kile alichoweza kufanya. Tunawezaje kuiga mfano wa Daudi tunapotafuta njia za kueneza ujumbe wa Ufalme?
2. Tunaweza kujichunguza jinsi gani?
2 Fanya Yote Uwezayo: Wengi wamerahisisha maisha yao ili wawe mapainia wasaidizi au wa kawaida. (Mt. 6:22) Je, unaweza kuwaunga mkono? Ukisali na kuchunguza hali zako, unaweza kuona “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” umefunguliwa. Ikiwa ndivyo, tumia fursa hiyo!—1 Kor. 16:8, 9.
3. Tunaweza kutumia fursa zipi kutoa ushahidi hata kama hali zetu hazituruhusu kuwa mapainia?
3 Namna gani ikiwa hali zako hazikuruhusu kuwa painia? Usipuuze fursa nyingine zinazojitokeza. Kwa mfano, ikiwa unakutana na watu mbalimbali katika kazi yako, kwa nini usitumie fursa hiyo kuwahubiria? Au ikiwa una tatizo la afya, je, unaweza kutumia nafasi hiyo kuwahubiria wahudumu wako wa afya? Kumbuka kwamba wale ambao hawawezi kabisa kufanya mengi katika huduma kwa sababu ya umri au tatizo kubwa la afya, wanaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, au 45. Unapojaza ripoti yako ya utumishi kila mwezi, usisahau kuripoti wakati uliotumia kuhubiri isivyo rasmi pamoja na machapisho yoyote uliyotoa, kutia ndani trakti, na mialiko ya Ukumbusho na makusanyiko. Unaweza kushangaa kuona jinsi wakati huo, unaoonekana kuwa mdogo, unapojumlishwa pamoja huwa mwingi!
4. Umeazimia kufanya nini?
4 Katika hali zozote tulizo nazo, acheni tutumie kila fursa tunayopata kueneza ujumbe wa Ufalme. Tukifanya hivyo, tutapata uradhi kwa sababu tunafanya yote tuwezayo kwa ajili ya Ufalme.—Marko 14:8; Luka 21:2-4.