DEA/G. Dagli Orti/De Agostini via Getty Images
Jitihada ya Huldrych Zwingli ya Kutafuta Kweli ya Biblia
Leo watu wengi wanyoofu wanaopenda dini wanaweza kujichunguzia ikiwa mambo wanayoamini yanategemea mafundisho ya Biblia au la. Hali haikuwa hivyo mwanzoni mwa karne ya 16. Kwa nini? Kwa sababu watu wengi hawangeweza kupata Biblia katika lugha yao wenyewe. Hivyo, ni waumini wachache sana katika makanisa ambao wangeweza kulinganisha mambo ambayo Kanisa lilifundisha na kile hasa ambacho Biblia inasema. Na viongozi wa dini hawakutoa msaada wowote. Kitabu kinachozungumzia historia ya kanisa la Kikristo (History of the Christian Church) kinasema hivi: “Kanisa nchini Uswisi lilikuwa limepotoka. Viongozi wa dini hawakuwa na ujuzi, walitegemea ushirikina, na walikuwa na maadili mapotovu.”
Katika kipindi hicho, Huldrych Zwingli alianza kutafuta kweli ya Biblia. Aligundua nini? Alitumia njia gani kuwaeleza wengine mambo aliyojifunza? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na maisha yake na mambo aliyoamini?
Zwingli Anaanza Uchunguzi
Alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, Zwingli alikusudia kuwa kasisi wa Kanisa Katoliki. Wakati huo, mtu yeyote aliyetaka kuwa kasisi alipaswa kujifunza falsafa, mapokeo ya kanisa, na maandishi mengine ya “Mababa wa Kanisa”—lakini si Biblia.
Zwingli alianzaje kutafuta kweli ya Biblia? Alipokuwa chuo kikuu huko Basel, Uswisi, alihudhuria mihadhara ya Thomas Wyttenbach, ambaye alishutumu mfumo wa Kanisa wa kudai malipo kwa ajili ya msamaha wa dhambi.a Mwandishi mmoja wa maisha ya Zwingli anasema kwamba Zwingli “alijifunza kutoka [kwa Wyttenbach] kwamba kifo cha Kristo kilitolewa mara moja kulipia dhambi zetu.” (1 Petro 3:18) Alipoelewa kwamba fidia ya Yesu ndiyo msingi pekee wa kupata msamaha wa dhambi, Zwingli alikataa fundisho la kwamba viongozi wa dini wangetoa msamaha wa dhambi baada ya kupokea malipo. (Matendo 8:20) Hata hivyo, Zwingli aliendelea na masomo yake na akawa kasisi wa Kanisa Katoliki akiwa na umri wa miaka 22.
Katika miaka hiyo, Zwingli alijifunza Kigiriki ili aelewe lugha ya awali iliyotumiwa kuandika sehemu ya Biblia ambayo kwa kawaida inajulikana kama Agano Jipya. Pia, alichunguza maandishi ya Erasmus na akagundua kwamba kama Biblia inavyofundisha, Yesu ndiye Mpatanishi pekee kati ya Mungu na wanadamu. (1 Timotheo 2:5) Kwa sababu hiyo, Zwingli alianza kutilia shaka fundisho la Kanisa Katoliki kwamba mtu anaweza kuwatumia watakatifu kuzungumza na Mungu.
Zwingli aliongeza jitihada zake za kutafuta kweli alipokuwa na umri wa zaidi ya miaka 30. Hata hivyo, wakati huo alitumikia pia akiwa kasisi wa jeshi katika vita mbalimbali zilizopiganwa kotekote barani Ulaya ili kuidhibiti Italia. Mwaka wa 1515, wakati wa vita vya Marignano, alijionea Wakatoliki wakiwaua maelfu ya Wakatoliki wenzao. Miaka kadhaa baadaye, Zwingli alinakili kwa mkono na hata akakariri sehemu kubwa ya Maandiko ya Kigiriki. Kufikia mwaka wa 1519, alikuwa akiishi jijini Zurich, kituo cha mamlaka ya kisiasa nchini Uswisi. Akiwa huko, alikuja kuamini kwamba Kanisa linapaswa kuacha kabisa kufundisha mafundisho yoyote ambayo hayawezi kuthibitishwa na Maandiko. Lakini angewasaidiaje wengine kufikia mkataa huo?
“Hatujawahi Kamwe Kusikia Mahubiri Kama Hayo”
Zwingli aliamini kwamba watu wangekataa uwongo wa kidini mara tu baada ya kusikia kweli ya Biblia. Kwa hiyo, alipochaguliwa kuwa kasisi wa kanisa maarufu la Zurich lililoitwa Grossmünster, alitangaza mpango wenye kushangaza alipoanza kuhubiri: Hatasoma tena kutoka kwenye mkusanyo wa maandiko ya Kilatinib ambayo viongozi wa dini walikuwa wametumia kidesturi kwa karne nyingi. Badala yake angehubiri Injili moja kwa moja kutoka kwenye Biblia, sura baada ya sura, kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Badala ya kutumia mawazo ya Mababa wa Kanisa kuelezea Maandiko, angetumia Maandiko kueleza Maandiko. Alifanya hivyo kwa kuzungumzia masimulizi rahisi na kuyatumia kufafanua mafundisho yaliyokuwa magumu kueleweka.—2 Timotheo 3:16.
Sergio Azenha/Alamy Stock Photo
Kanisa la Grossmünster jijini Zurich
Alipohubiri, Zwingli aliwasaidia watu kuona jinsi ambavyo Biblia ingewasaidia katika maisha yao ya kila siku. Alifundisha kuhusu viwango vya maadili vya Biblia, na akashutumu ibada inayotolewa kwa Maria, mama ya Yesu, kusali kwa watakatifu, kudai malipo ya msamaha wa dhambi, na upotovu wa maadili wa viongozi wa dini. Watu waliitikiaje? Baada ya mahubiri yake ya kwanza, baadhi ya watu walisema hivi: “Hatujawahi kamwe kusikia mahubiri kama hayo.” Na mwanahistoria mmoja alisema hivi kuhusu waumini wa Kanisa Katoliki ambalo Zwingli alifundisha: “Watu ambao walikuwa wameacha kuhudhuria Misa kwa sababu ya kuchukizwa na ujinga na maisha mapotovu ya makasisi, sasa walianza kurudi.”
Katika mwaka wa 1522, viongozi wa dini walijaribu kuwachochea wanasiasa wa Zurich wawazuie watu wasifanye chochote kinachopinga mafundisho ya Kanisa. Matokeo ni kwamba Zwingli alishtakiwa kuwa mwasi wa kidini. Kwa kuwa alikataa kukana imani zake, alijiuzulu na kuacha kuwa kasisi wa Kanisa Katoliki.
Zwingli Alifanya Nini?
Ingawa Zwingli hakuwa kasisi tena, bado aliendelea kuhubiri, naye alijaribu kuwasadikisha wengine kuhusu mambo ambayo aliamini. Kuhubiri kwake kulimfanya kuwa maarufu, na hilo likamfanya awe na uvutano mkubwa miongoni mwa wanasiasa wa Zurich. Kwa sababu ya uvutano huo, alijaribu kuchochea marekebisho ya kidini jijini Zurich. Kwa mfano, mwaka wa 1523, alisadikisha mahakama za jiji la Zurich zitangaze kwamba ni kinyume cha sheria kufundisha mafundisho ya kidini ambayo hayawezi kuthibitishwa na Maandiko. Katika mwaka wa 1524, aliwasadikisha kutangaza kwamba ni kinyume cha sheria kuabudu sanamu. Mahakimu walisimamia kuharibiwa kwa madhabahu, sanamu, picha, na mabaki ya vitu vya kale vya kidini. Walifanya hivyo kwa kushirikiana na wahubiri wengine wa eneo hilo na kwa idhini ya watu. Kitabu kinachomrejelea Zwingli kuwa nabii mwenye silaha wa Mungu (Zwingli—God’s Armed Prophet) kinasema hivi: “Mbali na uporaji wa makanisa uliofanywa na maharamia kutoka Skandinavia, Kanisa halijawahi kushuhudia uharibifu mkubwa kama huo wa kimakusudi.” Kufikia mwaka wa 1525, alikuwa pia amewashawishi wenye mamlaka kubadili majengo ya makanisa kuwa hospitali na kuwaruhusu watawa wa kiume na wa kike kufunga ndoa. Pia, alipendekeza kwamba Misa ibadilishwe na sherehe rahisi iliyotegemea kielelezo kilicho kwenye Biblia. (1 Wakorintho 11:23-25) Wanahistoria wanasema kwamba jitihada za Zwingli zilitokeza umoja kati ya viongozi wa dini na wanasiasa jijini Zurich na kuweka msingi wa yale Marekebisho Makubwa ya Kidini na wa dini mpya ya Kiprotestanti.
Toleo la 1536 la Biblia ya Zurich, kwenye Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova, Warwick, New York
Kazi muhimu zaidi ambayo Zwingli alifanya ni kutafsiri Biblia. Katika miaka ya 1520, aliongoza kikundi cha wasomi kutafsiri Biblia wakitumia mbinu rahisi. Walisoma kila mstari kutoka kwenye maandishi ya awali ya Kiebrania na ya Kigiriki na pia kutoka kwenye tafsiri zilizoheshimika, kutia ndani Septuajinti ya Kigiriki na Vulgate ya Kilatini. Kisha wangezungumzia maana ya mstari na kuandika maamuzi yao. Walifafanua na kutafsiri Neno la Mungu, na hatimaye katika mwaka wa 1531 wakatokeza buku moja linaloitwa Biblia ya Zurich.
Ingawa Zwingli alikuwa mnyoofu, hakuheshimu imani za wengine, naye alikuwa mkatili. Kwa mfano, mwaka wa 1525, alishiriki katika kesi dhidi ya Wanabaptisti, ambao walipinga imani ya kwamba watoto wanapaswa kubatizwa. Baadaye mahakama zilipotangaza hukumu ya kifo dhidi ya mtu yeyote aliyeendelea kupinga kwamba watoto wanapaswa kubatizwa, Zwingli hakupinga uamuzi huo wa kikatili. Pia, aliwachochea viongozi wa kisiasa watumie nguvu za kijeshi kueneza marekebisho ya kidini. Hata hivyo, maeneo kadhaa nchini Uswisi yaliyokuwa na Wakatoliki wenye msimamo mkali yalipinga marekebisho yake. Hilo lilitokeza vita vya wenyewe kwa wenyewe. Zwingli alienda kwenye uwanja wa vita pamoja na wanajeshi kutoka Zurich, ambako aliuawa akiwa na umri wa miaka 47.
Urithi Ambao Zwingli Aliacha
Kwa kweli, Huldrych Zwingli ana sehemu muhimu katika historia, ingawa yeye si maarufu kama Martin Luther na John Calvin ambao wanajulikana sana kwa sababu ya yale Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti. Zwingli alipinga mafundisho ya Kanisa Katoliki la Roma kwa njia kubwa zaidi kuliko Martin Luther. Nazo jitihada za Zwingli zilifanya iwe rahisi zaidi kwa watu kukubali maoni ya John Calvin. Kwa sababu hiyo amekuja kujulikana kama Mtu wa Tatu wa Yale Marekebisho Makubwa ya Kidini.
Kazi ambazo Zwingli alifanya zilitokeza faida na madhara. Ili kueneza maoni yake, alijihusisha sana katika siasa na vita. Kwa kufanya hivyo, alikosa kufuata mfano wa Yesu Kristo, ambaye alikataa kujihusisha na siasa, na ambaye aliwafundisha wanafunzi wake kuwapenda adui zao, badala ya kuwaua.—Mathayo 5:43, 44; Yohana 6:14, 15.
Wakati huohuo, Zwingli anakumbukwa kwa sababu alikuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii aliyeazimia kuwaeleza wengine mambo ambayo alijifunza. Aligundua kweli nyingi za Biblia na akawasaidia wengine kufanya hivyo pia.
a Malipo kwa ajili ya msamaha wa dhambi (ghofira), yalikuwa maagizo yaliyotolewa na viongozi wa kanisa ambayo yalisemekana kupunguza au hata kufuta adhabu ambayo watu hupata wakiwa toharani(purgatori) baada ya kufa.
b Mkusanyo wa maandiko hayo ya Kilatini ni kitabu kilicho na mistari ya Biblia iliyochaguliwa mapema ambayo husomwa mwaka mzima.