Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • lfs makala 9
  • Maisha Yenye Kuridhisha ya Umishonari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maisha Yenye Kuridhisha ya Umishonari
  • Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tunasikia Kweli ya Biblia kwa Mara ya Kwanza
  • Najiwekea Mradi
  • Kufikia Mradi Wangu
  • Umishonari Katika Nyakati za Taabu
  • Kufukuzwa!
  • Kutumikia Nchini Honduras
  • Kufikia Miradi ya Kiroho Huleta Furaha ya Kweli
  • Wamishonari Wasukuma Mpanuko wa Ulimwenguni Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Bidii ya Umisionari—Alama ya Wakristo wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • ‘Mkono wa Yehova Ulikuwa Pamoja Nao’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Jinsi Siku Ilivyo Katika Maisha ya Misionari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
lfs makala 9
Elfriede Urban.

ELFRIEDE URBAN | SIMULIZI LA MAISHA

Maisha Yenye Kuridhisha ya Umishonari

Miaka ya kwanza ya maisha yangu ilikuwa yenye taabu. Nilizaliwa Desemba 11, 1939, nchini Chekoslovakia, miezi mitatu tu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza. Majuma mawili baadaye, mama yangu alikufa kutokana na matatizo ya kiafya aliyopata baada ya kujifungua. Kabla ya hayo, baba yangu alikuwa amehamia nchini Ujerumani ili kutafuta kazi. Ninafurahi kwamba wazazi wa mama yangu walinichukua na kunitunza. Wakati huo, bado walikuwa wakiwalea mabinti wao watatu ambao walikuwa wadogo kuliko mama.

Nikiwa na babu na nyanya

Vita viliisha mwaka wa 1945, lakini maisha yaliendelea kuwa magumu sana. Tulifukuzwa Chekoslovakia kwa sababu tulikuwa Wajerumani, basi tukarudi Ujerumani. Tuliporudi, miji ilikuwa imeharibiwa kabisa, na watu wengi walikuwa maskini hohehahe. Wakati mwingine wadogo wa mama wangesubiri kwenye foleni ya chakula usiku mzima, ili kupata tu chakula kidogo. Pindi nyingine, tulienda msituni kutafuta uyoga na matunda madogo meusi yanayoitwa blackberries, kisha tungebadilishana vitu hivyo na wengine ili tupate mkate. Ilikuwa vigumu sana kupata chakula hivi kwamba watu walikuwa wakiiba wanyama-vipenzi na kuwala. Mara nyingi tulilala njaa.

Tunasikia Kweli ya Biblia kwa Mara ya Kwanza

Babu na nyanya walikuwa Wakatoliki lakini hatukuwa na Biblia. Babu alitaka kununua Biblia lakini kasisi alikataa kumuuzia na akamwambia kwamba washiriki wa kanisa wanahitaji tu kusikiliza Misa. Kwa hiyo, babu alibaki na maswali mengi kumhusu Mungu.

Nilikuwa na umri wa miaka saba Mashahidi wa Yehova walipotutembelea nyumbani. Walitumia Biblia kujibu maswali ya babu kuhusu mambo kama vile Utatu, moto wa mateso, na hali ya wafu. Babu aliridhika na majibu ya wazi ambayo alipata kwenye Biblia. Alikuwa na uhakika kabisa kwamba ameipata kweli. Baada ya hapo, tulianza kujifunza Biblia kwa ukawaida tukiwa familia nzima.

Najiwekea Mradi

Hata ingawa nilikuwa msichana mdogo, nilimpenda Yehova kutoka moyoni. Nilipenda kusoma masimulizi kuhusu wamishonari ambao walimtumikia Yehova katika nchi za mbali. Nilijiuliza, “Maisha yao yakoje? Wanahisije wanapowahubiria watu ambao hawajawahi kusikia jina la Yehova?’

Elfriede akiwa kwenye dawati lake shuleni.

Muda mfupi kabla ya kujiwekea mradi wa kuwa mmishonari

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, niliamua kwamba ningependa kuwa mmishonari na nikaanza kufanya mambo ambayo yangenisaidia kufikia mradi huo. Kwanza, nilijitahidi kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii. Kisha, nikabatizwa Desemba 12, 1954, na baada ya muda nikawa painia. Sasa nilikuwa nikikaribia mradi wangu!

Nilijua kwamba ili kuhudhuria Shule ya Gileadi ya wamishonari, nilihitaji kujua Kiingereza, basi nilijifunza lugha hiyo kwa bidii. Wakati huo, nchini Ujerumani kulikuwa na wanajeshi kutoka Marekani. Niliwaza kwamba ningefanya mazoezi ya kuzungumza Kiingereza kwa kuongea nao. Kwa hiyo, siku moja nilimkaribia mwanajeshi mmoja na kumwambia hivi kwa Kiingereza, “I am Christ.” (“Mimi ni Kristo.”) Alinitazama kisha akanijibu kwa fadhili, “I think you mean to say ‘I am a Christian.’” (“Nafikiri unataka kusema ‘Mimi ni Mkristo.’”) Kumbe bado nilikuwa na kazi kubwa ya kuboresha Kiingereza changu!

Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, nilihamia Uingereza. Saa za asubuhi nilifanya kazi ya kutunza watoto wa familia moja ya Mashahidi. Saa za mchana nilishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, na hiyo ilikuwa fursa nzuri sana ya kufanya mazoezi ya kuzungumza Kiingereza. Baada ya kukaa Uingereza kwa mwaka mmoja, nilizungumza Kiingereza vizuri zaidi.

Nilirudi Ujerumani, na mwezi wa Oktoba 1966, nilialikwa kutumikia nikiwa painia wa pekee huko Mechernich. Kulikuwa na baridi kali katika eneo hilo, na watu vilevile walionyesha ubaridi mwingi kuelekea ujumbe wetu. Hawakutualika kuingia nyumbani kwao hata baridi kali iliposhuka kufikia chini ya sufuri Selsiasi. Mara nyingi nilisali na kumsihi Yehova hivi, “Ikiwa siku moja utaniruhusu niwe mmishonari, tafadhali nitume kwenye nchi yenye joto.”

Kufikia Mradi Wangu

Baada ya kutumikia nikiwa painia wa pekee kwa miezi michache, Yehova alitimiza tamaa ya moyo wangu! Nilipata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 44 la Shule ya Gileadi, na tulihitimu Septemba 10, 1967. Nilipewa mgawo wa kwenda wapi? Kwenye nchi maridadi ya kitropiki inayoitwa Nikaragua, iliyoko Amerika ya Kati! Kulikuwa na wamishonari wengine tayari na walinikaribisha mimi na waandamani wenzangu watatu kwa mikono miwili. Nilihisi kama mtume Paulo ambaye ‘alimshukuru Mungu na kujipa moyo’ akina ndugu walipokuja kumpokea.​—Matendo 28:15.

Elfriede na wanafunzi wenzake wakitazama ramani ya tufe wakiwa Gileadi.

Tukiwa Shule ya Gileadi (nipo kushoto), pamoja na wanafunzi wenzangu Francis na Margaret Shipley

Nilipewa mgawo wa kuhubiri katika mji mtulivu wa León na nikaazimia kujifunza Kihispania haraka iwezekanavyo. Haikuwa rahisi kwangu kuifahamu lugha hiyo, licha ya kwamba nilijifunza kwa saa 11 kila siku, kwa miezi miwili!

Ninakumbuka siku moja, mwenye nyumba alitaka kunipa fresco. Hiyo ni juisi ya matunda katika Kinikaragua. Nilifikiri kwamba nimemwambia mimi hunywa tu “maji yaliyochujwa.” Lakini mwanamke huyo alinitazama kwa mshangao. Siku chache baadaye niligundua nilikuwa nimemwambia mimi hunywa tu “maji matakatifu”! Nashukuru kwamba kadiri muda ulivyosonga nilifahamu Kihispania vizuri zaidi.

Elfriede na Marguerite wakiwa juu ya farasi.

Nikiwa na Marguerite, mmishonari aliyekuwa mwandamani wangu kwa miaka 17

Mara nyingi nilijifunza Biblia na familia nzima nzima. Kwa kuwa nilihisi nikiwa salama katika mji wa León, nilipenda kuongoza mafunzo ya Biblia jioni, nyakati nyingine mpaka saa nne usiku. Nilijua karibu kila mtu kwa jina katika mji huo. Nilipokuwa nikirudi nyumbani, niliwasalimu majirani wenye urafiki na kuwajulia hali. Walipenda kuketi nje ya nyumba zao jioni na kufurahia upepo huku wakistarehe kwenye viti vinavyobembea.

Niliwasaidia watu kadhaa kujifunza kweli huko León. Mmoja wao alikuwa Nubia ambaye alikuwa na wavulana wanane wadogo. Tuliendelea kujifunza lakini katika mwaka wa 1976 nilipewa mgawo wa kwenda Managua. Sikuweza kuwasiliana na Nubia na watoto wake kwa miaka 18, hadi niliporudi León kuhudhuria kusanyiko. Wakati wa mapumziko, nilizungukwa na kundi la wanaume vijana. Walikuwa watoto wa Nubia! Nilisisimka sana nilipoona kwamba Nubia alikuwa amefaulu kuwalea wana wake katika kweli.

Umishonari Katika Nyakati za Taabu

Mwishoni mwa miaka ya 1970, kulianza kuwa na misukosuko ya kijamii na ya kisiasa nchini Nikaragua. Tuliendelea kuhubiri kadiri tulivyoweza. Eneo nililogawiwa la Masaya lilikuwa kusini mwa jiji kuu na mara nyingi kulikuwa na maandamano yenye kelele na fujo za wafanya-ghasia waliokuwa wamebeba silaha. Usiku mmoja mikutano ilipokuwa ikiendelea kwenye Jumba la Ufalme, tulilazimika kulala sakafuni kwa sababu wapiganaji wa kikundi cha Sandinista walikuwa wakifyatuliana risasi na wanajeshi wa serikali.a

Siku nyingine nilipokuwa katika huduma, nilifika mahali ambapo mpiganaji wa Sandinista aliyekuwa amejifunika uso alikuwa akimpiga risasi mwanajeshi. Nilijaribu kutoroka, lakini wanaume wengine waliokuwa wamejifunika uso wakatokea. Nilipiga kona na kukimbia lakini hakukuwa na mahali pa kutorokea. Kisha helikopta za serikali zikaanza kumimina risasi. Ghafla, mwanamume fulani akafungua mlango wa nyumba yake na kunivuta ndani. Nilihisi Yehova alikuwa ameniokoa!

Kufukuzwa!

Nilitumikia katika eneo la Masaya hadi Machi 20, 1982, siku ambayo sitawahi kusahau. Mapema asubuhi mimi na wamishonari wengine watano tulikuwa tukijiandaa kupata kiamsha kinywa tulipoona kikundi cha wanajeshi wa Sandinista waliobeba bunduki wakiingia upande wa nyuma wa makao ya wamishonari. Waliingia kwenye chumba cha kulia chakula na mmoja wao akatoa agizo kwa ukali: “Kila mmoja wenu ana saa moja ya kuweka vitu vyake kwenye begi moja kisha mwandamane nasi.”

Wanajeshi hao walitupeleka kwenye shamba moja ambapo tulizuiliwa kwa saa kadhaa. Kisha wakatupeleka sote wanne kwa basi dogo hadi kwenye mpaka wa Kosta Rika, na hivyo tukawa tumefukuzwa nchini. Kwa ujumla, wamishonari 21 walifukuzwa.

Akina ndugu nchini Kosta Rika walitukaribisha, na siku iliyofuata tukawasili katika ofisi ya tawi jijini San José. Hata hivyo, hatukukaa hapo muda mrefu. Siku kumi hivi baadaye, wanane kati yetu walipewa mgawo mpya wa umishonari nchini Honduras.

Kutumikia Nchini Honduras

Nchini Honduras, nilipewa mgawo wa kwenda jiji la Tegucigalpa. Katika miaka 33 ambayo nilitumikia katika jiji hilo, kutaniko moja tulilokuta liliongezeka na kuwa manane. Kwa kusikitisha, kadiri miaka ilivyozidi kusonga, uhalifu pia uliongezeka jijini Tegucigalpa. Kulikuwa na wezi wengi na walinipora mara kadhaa. Isitoshe kulikuwa na magenge ya uhalifu na washiriki wa magenge hayo walidai niwape pesa, au “kodi ya vita” kama walivyoiita. Niliwaambia, “Nina kitu chenye thamani zaidi kuliko pesa,” kisha niliwapa trakti au gazeti. Sikuzote waliniachilia!

Watu wengi katika jiji la Tegucigalpa walipenda amani na walikuwa wenye fadhili. Nilisaidia baadhi yao kujifunza kweli. Kwa mfano, ninamkumbuka Betty ambaye alikuwa mwanafunzi wa Biblia. Alikuwa anafanya maendeleo lakini siku moja aliniambia kwamba anataka kujiunga na kanisa la kiinjilisti. Nilivunjika moyo lakini miaka miwili baadaye Betty aliacha kwenda kanisani na akaanza tena kujifunza Biblia nami. Ni nini kilichomfanya arudi? Betty alikosa sana upendo wa kweli ambao alionyeshwa kutanikoni. (Yohana 13:34, 35) Aliniambia: “Ninyi huwakaribisha kwa uchangamfu wote wanaohudhuria mikutanoni yenu, iwe ni matajiri au maskani. Ninyi ni tofauti.” Baada ya muda, Betty alibatizwa.

Makao ya wamishonari jijini Tegucigalpa yalifungwa mwaka wa 2014, na baada ya hapo nilipata mgawo mpya wa kwenda nchi ya Panama. Sasa ninaishi kwenye makao ya wamishonari pamoja na wamishonari wengine wanne ambao wametumikia kwa muda mrefu.

Ramani ya Amerika ya Kati inayoonyesha maeneo ambayo Elfriede aliishi na kuhubiri: Tegucigalpa, Honduras; León na Masaya, Nikaragua; Kosta Rika; na Panama.

Kufikia Miradi ya Kiroho Huleta Furaha ya Kweli

Kufikia sasa, nimekuwa mmishonari kwa miaka 55. Sasa siwezi kufanya mengi kama nilivyofanya zamani kwa sababu ya matatizo ya afya ninayokabili. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova ninaendelea kuwafundisha wengine kumhusu.

Je, ningeweza kutumia maisha yangu kufuatilia jambo tofauti? Bila shaka. Hata hivyo, nisingekosa baraka nyingi ambazo nimepata maishani! Nimesaidia zaidi ya watu 50 kujifunza kweli nao ni kama wana na mabinti wa kiroho kwangu. Isitoshe, nina marafiki wengi. Kwa kweli hiyo ni “familia kubwa,” bila kusahau upendo na utegemezo ninaopata kutoka kwa dada ya mama yangu anayeitwa Steffi, ambaye anaishi Ujerumani.

Ingawa sikuwahi kufunga ndoa, sijawa mpweke. Yehova amekuwa pamoja nami. Isitoshe, nimepata marafiki wazuri kama vile Marguerite Foster, mmishonari ambaye alikuwa mwandamani wangu kwa miaka 17. Tulifurahia mambo mengi pamoja, na mpaka leo sisi ni marafiki wa karibu.​—Methali 18:24.

Jambo linaloniridhisha kabisa maishani ni kujua kwamba nimetumia maisha yangu kwa njia bora kabisa, yaani, kumtumikia Yehova kikamili. Nimetimiza ndoto yangu ya utotoni, na wakati uleule nimejionea mambo mengi yenye kusisimua. Nimefurahia maisha yangu na ninatazamia kwa hamu kumtumikia Yehova kwa umilele wote.

a Chama cha Sandinista National Liberation Front kilipata umaarufu nchini Nicaragua katika mwishoni mwa miaka ya 1970 na hatimaye kikaondoa mamlakani familia ambayo ilikuwa imetawala nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 40.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki