Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 5/8 kur. 17-19
  • Nawezaje Kuwa na Furaha Nikiishi na Mzazi Mmoja Tu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nawezaje Kuwa na Furaha Nikiishi na Mzazi Mmoja Tu?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ubora—Sio Wingi
  • Kutosheka na Vichache
  • Jinsi ya Kushughulikia Kazi Nyingi Mno
  • Ninaweza Kuwa na Furaha Katika Familia ya Mzazi Mmoja?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Je! Nitakuwa Mtu wa Kawaida Nikiwa na Mzazi Mmoja Tu?
    Amkeni!—1991
  • Naweza Kumsaidiaje Mzazi Wangu Aliye Peke Yake?
    Amkeni!—1992
  • Nishughulikeje na Mzazi Wangu Aliyeondoka Nyumbani?
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 5/8 kur. 17-19

Vijana Wanauliza. . .

Nawezaje Kuwa na Furaha Nikiishi na Mzazi Mmoja Tu?

“Watoto wenye wazazi wawili waweza kuwa na vyumba vyao wenyewe na kununua nguo mpya. Lakini mimi napaswa kushiriki chumba; mara nyingi sipati aina ya nguo nipendazo. Mama husema ni za bei ghali sana kwake. Kukiwa na zile kazi nyingi za nyumbani ambazo napaswa nifanye anapofanya kazi, najiona kuwa kama yaya—ni kama ninazuiliwa nisifurahie sehemu ya utoto wangu.”—Shalonda, umri wa miaka 13.

NYUMBA yenye wazazi wawili ni bora kabisa. Wazazi wawili wenye upendo waweza kwa kawaida kutoa mwongozo, himaya, na utegemezo zaidi ya vile mmoja awezavyo. “Wawili ni bora kuliko mmoja,” yasema Biblia, “kwa sababu wakiwa pamoja waweza kufanya kazi kwa matokeo zaidi.”—Mhubiri 4:9, Today’s English Version.

Si ajabu basi, kwamba ijapokuwa ongezeko lenye kuendelea la nyumba zenye mzazi mmoja, vijana wengi huona aibu kuishi katika familia kama hizo. Huenda wakahisi kwamba hawako tayari kukabiliana na mibano na matatizo ambayo maisha kama hayo huwaletea. Vipi, basi, ikiwa hali usizoweza kudhibiti zakunyima upendo na utunzaji wa mmoja wa wazazi wako? Je! ni lazima uishi maisha yasiyo na furaha? Sivyo.

Mengi yanategemea maoni yako juu ya hali hiyo. Mithali 15:15 husema hivi: “Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.” Kulingana na kanuni hiyo, Dakt. Helen Mendes asema hivi: “Familia zenye mzazi mmoja zapasa zijione kuwa timu na kujikubali zenyewe kuwa familia kamili,” si jamaa zilizovunjika. Yeye aongeza hivi: “Familia kama hizo zina mwelekeo na maoni tofauti kabisa kuhusu maisha zinapoanza kujiona kuwa vikundi vya watu vinavyokubalika kijamii.” Lakini je, ni jambo la uhalisi kuwa na maoni chanya (mazuri) kama hayo?

Ubora—Sio Wingi

Watafiti wa jarida Family Relations watukumbusha hivi: “Kuwepo kwa wazazi wawili katika nyumba si uhakikisho kwamba upendo, malezi yanayofaa, na mwongozo wenye hekima unaandaliwa.” Wao husema pia: “Mzazi aliye nyumbani kimwili huenda wakati mwingi asiwepo kisaikolojia [kiakili].” Hivyo, furaha yako yategemea, si wingi wa wazazi unaoishi nao, bali aina ya mzazi au wazazi ulio nao nyumbani na upendezi na hangaiko wanaloonyesha kwa hali njema yako. Kama vile mwanasaikolojia Richard A. Gardner alivyoonelea: “Wazazi wabaya, wawe mmoja au wawili, hufanya watoto wasiwe na furaha; na wazazi wazuri, wawe mmoja au wawili, husaidia watoto wakue wenye afya njema zaidi na wenye furaha zaidi.” Na wazazi walio peke yao mara nyingi hufanya jitihada zenye kusifiwa kuwapa watoto wao ufikirio unaohitajiwa.

Melanie mwenye umri wa miaka kumi na saba asema hivi: “Haijawa rahisi tangu baba yetu alipotuacha. Imekuwa vigumu sana kwa mama yangu kwa sababu yeye hufanya kazi sasa. Lakini sisi huweza kwenda kwenye mikutano yetu ya Kikristo na kuwa na mafunzo ya Biblia ya kawaida, jambo ambalo hatukufanya mara nyingi wakati baba yetu alipokuwa akiishi nasi.” Yeye aongeza hivi: “Sisi hufanya mambo mengi zaidi tukiwa familia, na tumekaribiana sana. Bila shaka, namwonea hamu baba yangu, lakini nafurahia sana kuishi pamoja na mama yangu.” Ikiwa mzazi wako mmoja anafanya bidii kama hiyo ili kukulea katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova,” wewe waweza kufanikiwa na kusitawi hata ikiwa muundo wa familia yako si ule uliotamanika sana.—Waefeso 6:4, NW.

Kutosheka na Vichache

Hata hivyo, kuna mahangaiko halisi ambayo huenda yakatokea. Utafiti mmoja ulionyesha kwamba mara tu baada ya talaka, nyumba yenye mzazi mmoja huenda ikapatwa na upungufu wa asilimia 73 katika kiwango chayo cha maisha. Ni jambo lenye kueleweka, basi, kwamba pesa ni mojawapo kati ya mahangaiko makubwa katika familia nyingi zenye mzazi mmoja.a

Wewe waweza kufanya nini? Labda huna uwezo mwingi wa kudhibiti hali ya kifedha ya familia yenu. Lakini waweza kusaidia kuokoa na kutumia kwa muda mrefu vitu mlivyo navyo kwa kuepuka matumizi ya kupita kiasi. (Linganisha Yohana 6:12.) Kijana Rodney asema hivi: “Nyumbani, mimi hujaribu kuwa mwangalifu nisivunje au kupoteza vitu, kwa kuwa kutengeneza au kuweka vitu vipya mahali pa vya zamani kunagharimisha. Huwa najaribu kuzima vifaa vinavyotumia umeme au kuzima taa ambazo hazitumiwi. Hilo lasaidia kupunguza gharama zetu za umeme.”

Tony mwenye umri wa miaka kumi na minne hujaribu njia tofauti. Asema hivi: “Watoto katika shule yangu hudai kwamba wazazi wao wawanunulie viatu vya kuchezea na nguo zenye kubuniwa na watu mashuhuri. Wao hukataa kwenda shuleni bila hizo.” Tony aongeza hivi: “Mimi sina nguo za kisasa zilizobuniwa na watu mashuhuri, lakini mimi ni nadhifu na safi, nami hutunza zile nilizo nazo. Mama yangu anajaribu sana awezavyo; nami sitaki kufanya mambo yawe magumu zaidi kwake.” Hisia-mwenzi kama hiyo haiokoi tu machumo madogo bali pia ni chanzo halisi cha kitia-moyo kwa mzazi.—1 Petro 3:8.

Kupunguza au kuacha kabisa kuuma-uma makumbwe ya kuburudisha mdomo na vyakula visivyofaa afya huenda kukasaidia pia. Kijana Rita aonelea hivi: “Kula nyumbani huenda kusiwe kwenye kuvutia kama kula kwenye mikahawa yenye vyakula vinavyotayarishwa kwa haraka, lakini huokoa pesa.” Ni kadirio la hekima kweli kweli! Vijana wengine huchangia akiba ya familia sehemu ya machumo yao kutokana na kazi zao za nusu-wakati. Danny mwenye umri wa miaka kumi na mitatu humpa mama yake pesa ambazo yeye huchuma kutoka kwa kazi yake ya kupelekea watu magazeti. Mama yake aeleza hivi: “Baada ya kulipia rehani, gesi, simu, chakula, na kununua nguo, hizo ndizo pesa tuzitegemeazo kwa riziki. Na Danny ni mtoto mzuri kweli kweli; yeye haoni vibaya.” Kushirikiana katika jambo hilo ni njia moja ya ‘kumheshimu mzazi wako.’—Mathayo 15:4.

Ingawaje, kabla ya kutafuta kazi isiyo ya wakati wote, zungumza jambo hilo pamoja na mzazi wako.b Kazi isiyo ya wakati wote huenda ikaingilia kazi yako ya shule, wajibu wako mbalimbali wa nyumbani, na mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Kwa kawaida wazazi huweza kutafuta njia fulani ya kuwatunza watoto wao bila watoto wao kuhitaji kuchukua sehemu kubwa ya daraka hilo. Hata hivyo, huenda ukapaswa kuishi kwa machumo madogo. Lakini kumbuka kwamba ingawa vitu vya kimwili na pesa ni zenye manufaa, Wakristo wanahimizwa waridhike na “chakula na nguo.”—1 Timotheo 6:8-10; Luka 12:15.

Kwa mfano, huenda familia yako ikapaswa ihame nyumba kubwa zaidi kwenda kwenye ndogo zaidi; au kwenye kijumba cha sehemu ya jengo kubwa, sasa hiyo ikitaka ukae chumba kimoja na mshiriki wa familia. Lakini bado waweza kuridhika. Na kwa kutumia akili kidogo, huenda ukaweza kudumisha kadiri fulani ya faragha. Kwa mfano, familia fulani wamejenga katika sebule mahali pa kulala juu karibu na dari, panapofichwa na makabati ya kuwekea vitabu. Kupanga vizuri nafasi iliyopo au kutumia kitu kigawanyo cha vyumba huenda vilevile kukatosha kukufanya uhisi angalau faragha fulani.

Kwa vyovyote vile, msaikolojia Richard A. Gardner akumbusha vijana wenye mzazi mmoja hivi: “Ni jambo la maana kukumbuka kwamba pesa—na vitu ambavyo pesa zaweza kununua—siyo mambo yenye umaana zaidi maishani. Ni . . . mambo kama namna ya mtu uliye na jinsi unavyotendea watu wengine ambayo yataamua jinsi utakavyofurahia maisha.” (Linganisha Matendo 20:35.) Kulingana na hayo, mtume Paulo alisema hivi: “Nimejifunza kutosheka na kile ninacho . . . ili kwamba popote, kwa wakati wowote, ninaridhika.”—Wafilipi 4:11, 12, TEV.

Huenda pia ukahitaji kuchukua sehemu kubwa zaidi ya daraka la kufanya nyumba yenu iendelee vizuri kuliko kama ungekuwa ukiishi katika nyumba yenye wazazi wawili. Lakini badala ya kuwa na maoni mabaya kuhusu hali hiyo, jaribu kuiona kuwa nafasi ya kusaidia mzazi wako na pia kujizoeza kwa ajili ya madaraka ya wakati ujao.

Jinsi ya Kushughulikia Kazi Nyingi Mno

Hata hivyo, nyakati nyingine kijana hupata kwamba ana madaraka mengi kuliko yale awezayo kushughulikia. Hilo ni yamkini kutukia hasa kama wewe ni mtoto wa kwanza. Wewe waweza kufanya nini? Jaribu kuongea na mzazi wako na kumweleza jinsi tatizo hilo linavyokuathiri. Labda waweza kudokeza kwamba kazi zigawanywe kwa usawa zaidi. Kwa mfano, familia fulani huweka orodha ya kazi ambazo kila mshiriki wa familia apaswa afanye. Ili yeyote asilazimike kufanya kazi zile zisizopendeza wakati wote, familia nyingine hubadilishana zamu za kazi kwa ukawaida miongoni mwa washirika wa familia wenye uwezo.

Madokezo yaliyotangulia huenda yakawa yenye msaada katika kukabiliana na hali yako kwa kadiri uwezavyo. Hata hivyo, hiyo si kusema kwamba mara kwa mara hutaona ni laiti ungekuwa na mzazi wa pili nyumbani. Lakina kijana aitwaye Carrie aeleza jambo hilo hivi: “Huponi uchungu huo kamwe, lakini unapungua. Ni kama doa kubwa mkononi mwako. Lipo sikuzote, lakini nyakati nyingine hulioni.”

Hata hivyo, mengi yategemea kadiri unavyojitahidi kukabiliana na hali yako. Kwa kuwa yajapokuwa matatizo ya kuishi katika nyumba yenye mzazi mmoja, wewe waweza kusaidia kufanya maisha yako huko yawe yenye mafanikio na yenye shangwe!

[Maelezo ya Chini]

a Nyumba zenye mzazi mmoja ziongozwazo na baba huwa na hali bora kiuchumi kuliko zile ziongozwazo na mama kwa sababu (1) wanaume huchuma zaidi ya wanawake na (2) baba wasiopewa utunzaji wa watoto mara nyingi hukosa kulipa wake zao pesa walizoamriwa na mahakama kulipa au hukosa kulipa pesa za utunzaji wa watoto.

b Matoleo ya Amkeni! ya Julai 8, 1992 na Agosti 8, 1992, yatazungumzia kikamili zaidi habari ya kuajiriwa kazi ya kufanya ya baada ya shule.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kujitayarishia mwenyewe vyakula vyako vya mchana ni njia moja ya kuokoa wakati na pesa za mzazi wako

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki