Mtoto wa Chura
“Mtoto wa chura ni chura.”
Methali hii ya Kijapani humaanisha kwamba mtoto hukua na kuwa tu kama mzazi wake. Mama yangu alikuwa geisha.
NILIKUA katika nyumba ya geisha iliyosimamiwa na mama yangu. Kwa hiyo, kuanzia nilipokuwa mdogo, nilizungukwa na mabibi wenye kupendeza waliovalia kimono ghali sana. Nilijua kwamba nikiwa mkubwa, ningejiunga na maisha yao. Mazoezi yangu yalianza 1928 siku ya sita ya mwezi wa sita nilipokuwa na umri wa miaka sita. Tarakimu 666 ilisemekana kuhakikisha mafanikio.
Nilijifunza sanaa za kitamaduni za Japani—kucheza dansi, kuimba, kucheza vyombo vya muziki, kutumbuiza katika sherehe za chai, na kadhalika. Kila siku baada ya shule nilikimbia nyumbani, nikabadilisha mavazi yangu, na kwenda kwenye masomo yangu. Ningekuwa huko tena na rafiki zangu wa shuleni kwa sababu sisi sote tulikuwa watoto wa geisha. Ulikuwa wakati wenye shughuli nyingi, nami niliufurahia.
Siku hizo kabla ya Vita ya Ulimwengu ya 2, ilikuwa lazima kwenda shule hadi umri wa miaka 12, kwa hiyo ndipo nilipoanza kufanya kazi. Nikiwa geisha kijana, nilivalia kimono nzuri ajabu zilizokuwa na mikono iliyokuwa ikining’inia hadi karibu kwenye nyayo zangu. Nilihisi furaha sana nilipoenda kwenye mgawo wangu wa kwanza.
Kazi Yangu Nikiwa Geisha
Kazi yangu hasa ilitia ndani kutumbuiza na kutumikia nikiwa mtumishi wa kike. Matajiri walipopanga karamu za mlo kwenye mikahawa ya hali ya juu, wangepigia simu nyumba ya geisha na kuomba watumikiwe na geisha wachache. Geisha walipaswa kufanya jioni iwe yenye uchangamfu na kuhakikisha kila mgeni alienda nyumbani akiwa ameridhika, akihisi kwamba alikuwa na wakati mzuri.
Ili kufanya hivi, ilitubidi tuone kimbele mahitaji ya kila mgeni na kuyaandaa—hata kabla ya mgeni kutambua alikuwa na uhitaji. Nafikiri, jambo lililokuwa gumu zaidi, lilikuwa ni kubadilikana kwa muda mfupi sana. Ikiwa kwa ghafula wageni walitaka kuona dansi, basi tulicheza dansi. Ikiwa muziki ulitakikana, tulitoa vifaa vyetu na kucheza muziki uliotakikana au kuimba wimbo wowote ulioombwa.
Kueleweka vibaya kawaida ni kwamba geisha wote ni makahaba wa hali ya juu, ambao miadi yao yaweza kufanywa kwa simu. Sivyo ilivyo. Ijapokuwa kuna geisha ambao hujitafutia riziki kwa kujiuza, hakuna haja ya geisha kujishusha kiadili kwa jambo hilo. Najua kwa sababu sikufanya hivyo kamwe. Geisha ni mtumbuizaji, na akiwa mtumbuizaji mzuri, stadi zake humletea kazi, zawadi ghali, na bakshishi za ukarimu kutoka kwa wateja.
Ni kweli kwamba si wengi wawezao kuwa geisha bora kabisa. Geisha walio wengi huwa na ustadi wa mojawapo sanaa za utamaduni wa Japani tu. Lakini nilipata diploma katika sanaa saba kama hizo, kutia ndani dansi ya Kijapani, mpangilio wa maua, sherehe za chai, ngoma ya Kijapani iitwayo taiko, na mitindo mitatu ya muziki uchezwao kwenye shamisen yenye kamba tatu. Bila uwezo huo mbalimbali, ili kujitafutia riziki, labda ningehisi uhitaji wa kufanya lolote ambalo wateja waliniomba nifanye.
Wakati Japani haikuwa imara kiuchumi, nyakati nyingine wasichana walichagua kuwa geisha ili kutegemeza familia zao. Walikopa pesa ili kulipia mazoezi na kimono zao. Wengine waliuzwa na familia zao kwa nyumba za geisha. Wamiliki wao, wakiwa wamelipa pesa nyingi sana, walitaka warudishiwe malipo kutoka kwa wasichana hao. Katika hali hizi geisha walikuwa katika hali mbaya sana, kwa sababu mazoezi yao yalianza kuchelewa nao walianza kazi yao wakiwa na deni kubwa sana. Wengi wa geisha hao waligeukia au wakalazimika kuingia kwenye ukosefu wa adili ili kutimiza madaraka yao ya kifedha.
Utumishi wangu ukaja kutakikana sana na watu mashuhuri sana upande wa michezo, vitumbuizo, biashara, na siasa. Miongoni mwa wateja wangu walikuwa mawaziri na mawaziri wakuu. Wanaume hawa walikuwa wakinitendea kwa heshima na kunishukuru kwa kazi yangu. Ijapokuwa sikujiunga na mazungumzo yao isipokuwa niwe nimealikwa, mara nyingine niliombwa maoni. Kwa hiyo nilisoma magazeti na kusikiliza redio kila siku ili nijue habari za karibuni. Karamu nilizotumikia mara nyingi zilikuwa za kusudi la mashauri, kwa hiyo nilipaswa kuwa mwenye busara ili nisiseme mambo niliyosikia.
Mama Yangu Ni Nani?
Siku moja mnamo 1941, nilipokuwa mwenye umri wa miaka 19, niliitwa kwenye mkahawa mmoja na kupata wanawake wawili wakiningoja. Mmoja wao alitangaza kuwa alikuwa mama yangu mzazi na kwamba alikuja kunichukua anipeleke nyumbani. Yule mwanamke mwingine aliwaajiri geisha na akajitolea kunipa kazi. Alifikiri nilipaswa kufanya kazi ili kutegemeza mama yangu mzazi badala ya mama mlezi. Sikuwa nimewazia kamwe kwamba mwanamke aliyenilea hakuwa mama yangu halisi.
Nikiwa nimevurugika, nilikimbia nyumbani na kumwambia mama yangu mlezi lililotokea. Sikuzote alikuwa mwenye kudhibiti hisia zake, lakini sasa machozi yaliyajaza macho yake. Aliniambia yeye alitaka kuwa yule atakayeniambia kwamba nilipokuwa na umri wa mwaka mmoja, nilipelekwa kwenye nyumba ya geisha. Niliposikia kweli hiyo, nilipoteza tumaini katika watu na nikawa mwenye kujitenga na kimya.
Nilikataa kumkubali mama yangu mzazi. Bila shaka kutokana na mkutano wetu mfupi alijua kuhusu mafanikio yangu naye alitaka nifanye kazi ili nimtegemeze. Kulingana na mahali pa biashara ya rafiki yake, nilijua kwamba kufanya kazi huko kungetia ndani ukosefu wa adili. Nilitaka kuuza vipawa vyangu vya kisanaa, si mwili wangu. Ndivyo nilivyowaza, na bado nawaza, kwamba nilifanya uamuzi mzuri.
Ijapokuwa nilikasirishwa na mama yangu aliyenilea, ilinipasa kukubali kwamba alinizoeza ili niweze kujiruzuku sikuzote. Kadiri nilivyowaza jambo hilo, ndivyo nilivyohisi kuwiwa shukrani naye. Yeye alichagua kwa uangalifu na uthabiti mahali pangu pa kazi, akinilinda na wanaume waliotaka utumishi wa geisha kwa sababu tu ya makusudi ya ukosefu wa adili. Hadi leo, mimi humshukuru kwa jambo hilo.
Yeye alinifundisha kanuni. Aliyokazia ilikuwa ile ya ndiyo yangu iwe ndiyo na la yangu iwe la. Pia alinifundisha kukubali daraka na kuwa mwenye kujitia nidhamu kwa uzito. Kwa kufuata kanuni alizonifundisha, nilikuwa mwenye mafanikio katika kazi yangu. Nina shaka kama ningalipata msaada kama huo kutoka kwa mama yangu mzazi. Kulelewa kwangu na mama mwingine huenda kuliniokoa na maisha magumu, nami nikaamua kwamba nilifurahi jambo hilo lilitokea.
Mwana Katikati ya Vita
Nilizaa mwana mnamo 1943. Kulingana na desturi ya mapokeo ya Kijapani, ambayo haitambui “dhambi,” sikufikiri nimefanya kosa lolote au jambo la aibu. Nilipendezwa sana na mwana wangu. Alikuwa kitu chenye thamani zaidi nilichokuwa nacho—mtu wa kuishi kwa ajili yake na kumfanyia kazi.
Katika 1945 Tokyo ilikuwa ikipigwa mabomu vibaya sana, na ikanibidi kutoroka jiji pamoja na mwana wangu. Chakula kilikuwa haba, naye alikuwa mgonjwa sana. Watu waliijaa stesheni wakiwa wamevurugika sana, lakini hata hivyo tuliweza kupanda gari-moshi iliyokuwa ikienda kaskazini hadi Fukushima. Tulikaa huko kwenye hoteli usiku huo, lakini kabla sijampeleka mvulana wangu mdogo hospitalini, alikufa kutokana na utapia-mlo na upungufu wa maji mwilini. Alikuwa na umri wa miaka miwili tu. Nilivunjika moyo sana. Mchemsha-maji kwenye hoteli alichoma mwili wa mwana wangu kwa moto aliotumia kupasha joto maji ya kuogea.
Upesi baada ya hapo vita iliisha, nikarudi Tokyo. Jiji hilo lilikuwa limeharibiwa kabisa kwa mabomu. Nyumba yangu na kila kitu nilichokuwa nacho havikuwepo. Nilienda kwa nyumba ya rafiki yangu. Aliniazima kimono zake, nikaanza kufanya kazi tena. Mama yangu mlezi, ambaye alikuwa amekimbilia mahali nje ya Tokyo, alidai kwamba nimpelekee pesa na kumjengea nyumba Tokyo. Madai hayo yalinifanya nihisi mpweke zaidi kuliko wakati wowote ule. Bado nilikuwa namwomboleza mwana wangu na nilitamani liwazo, lakini hata hakutaja mtoto wangu. Alikuwa akijifikiria tu.
Wajibu wa Familia
Mapokeo yalifundisha kwamba vyote tulivyo navyo twadaiwa na wazazi na vilevile wazazi wetu wa kale na kwamba ni wajibu wa watoto kuwalipa wazazi wao kwa kuwatii bila ya shaka na kuwatunza mpaka wafe. Kwa hiyo nilifanya wajibu wangu, lakini madai ya mama yangu mlezi yalipita kiasi. Pia alitazamia nitegemeze watoto wawili wa ndugu yake aliowachukua awalee. Nilikuwa nikifikiria ni ndugu na dada yangu, hadi nilipofika umri wa miaka 19.
Geisha wengi hawakuolewa kamwe, nao waliepuka kuwa na watoto wao wenyewe. Mara nyingi walilea watoto wasichana kutoka familia maskini na kuwazoeza wawe geisha kwa kusudi tu la kupata tegemezo la kifedha ili kufurahia maisha yenye ustarehe uzeeni. Kwa huzuni, nilianza kuona kwa nini nilikuwa nimepokea utunzaji wote na mazoezi niliyokuwa nayo. Ulikuwa kwa sababu ya ulinzi wa kifedha tu.
Nilikubali yote haya, ijapokuwa nilijiuliza ni kwa nini, kuongezea mama yangu aliyenilea, nilipaswa kutegemeza “ndugu” na “dada” yangu, ambao wote walikuwa na afya nzuri na waliweza kufanya kazi. Hata hivyo, niliwategemeza wote watatu, nikifanya kila kitu walichoniomba. Hatimaye, siku kabla hajafa mnamo 1954, mama yangu alipiga magoti kitandani mwake, akainama, na kunishukuru kirasmi. Alisema kwamba nilikuwa nimefanya ya kutosha. Kukubali huku na wonyesho wa shukrani ulilipia miaka mingi ya kazi yangu. Uradhi wa kujua kwamba nilitimiza madaraka yangu bado hunifanya nilie machozi.
Kumwandalia Binti Yangu
Katika 1947, nilipata kuwa mama ya msichana mdogo, nami nikaamua kufanya kazi kwa bidii ili kupata utajiri kwa ajili yake. Kila usiku nilienda kufanya kazi. Pia nilianza kucheza katika majumba makuu ya Japani, kama vile Kabukiza katika Ginza. Hiyo pia ilitoa malipo mazuri.
Iwe ni kucheza dansi au kucheza shamisen, sikuzote nilipokea sehemu za uongozi. Lakini, mbali na kuwa na mafanikio ambayo geisha wengine waliyawazia tu, sikuwa mwenye furaha. Labda singalikuwa mpweke kama ningaliolewa, lakini maisha ya geisha na ndoa hayapatani. Liwazo langu pekee lilikuwa Aiko, msichana wangu mdogo, naye alikuwa jambo kuu katika maisha yangu.
Kwa kawaida, geisha huzoeza binti zao wafanye kazi hiyohiyo, wawe ni watoto halisi au wa kulelewa. Nilifuata desturi hiyohiyo, lakini baadaye nilianza kufikiri kuhusu aina ya maisha niliyokuwa nikimtayarishia. Ikiendelezwa, ingemaanisha kizazi baada ya kizazi hakingejua umaana wa kuwa na familia halisi. Nilitaka kuvunja mnyororo huo. Nilitaka Aiko, na watoto wake, wafurahie ndoa na maisha ya kawaida ya familia. Sikutaka mtoto wa huyu chura kuwa chura!
Aiko alipoingia miaka yake ya utineja, akawa hawezi kudhibitiwa. Tangu kifo cha mama yangu mlezi miaka michache iliyopita, washiriki wa Aiko nyumbani walikuwa wafanyikazi niliowaajiri. Alihitaji sana wakati na uangalifu wangu. Kwa hiyo hata ingawa nilikuwa na umri wa miaka ya katikati ya 30 na kwenye kilele cha kazi-maisha yangu, niliamua kuacha kazi ya geisha na kukubali kucheza kazini na kucheza shamisen tu. Niliacha kwa sababu ya Aiko. Tulianza kuwa na milo ya jioni pamoja, na mara akaanza kuwa mwenye kupendeza na kukubalika. Kumpa wakati wangu kulikuwa na matokeo mazuri ajabu.
Baada ya muda tukahamia mahali penye utulivu ambapo nilifungua mkahawa. Aiko akawa mkubwa, nikapumzishwa kuona akiolewa na Kimihiro, mwanamume mpole ambaye alielewa maisha niliyoishi.
Dini Yawa Suala
Katika 1968, Aiko akazaa mjukuu wangu wa kwanza. Muda mfupi baadaye akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hilo lilinishangaza kwa sababu tayari tulikuwa na dini. Nilikuwa nimeweka madhabahu kubwa sana ya Buddha nyumbani kwetu baada ya mama—mama yangu mlezi—kufa, nami nilipiga magoti mbele yayo kwa ukawaida nikimwabudu. Pia, nilikuwa nikizuru kaburi la familia kila mwezi ili kumpelekea ripoti ya yote yaliyotendeka.
Ibada ya wazazi wa kale iliniridhisha. Nilihisi kwamba nilikuwa nikifanya yale niliyopaswa kwa kutunza wazazi wangu wa kale na kuwaonyesha shukrani, na nilimzoeza Aiko kufanya hayohayo. Kwa hiyo nilighadhibika sana aliponiambia kwamba hangeshiriki tena katika ibada ya wazazi wa kale, wala hangeniabudu nitakapokufa. ‘Ni jinsi gani,’ nikajiuliza, ‘ningeweza kulea mtoto kama huyo, na angewezaje kujiunga na dini inayofundisha watu kutokuwa na shukrani hivyo kwa mababu wao?’ Kwa miaka mitatu iliyofuata, ilikuwa kana kwamba wingu jeusi lilikuwa likining’inia juu yangu.
Badiliko lilikuja wakati Aiko alipobatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Rafiki Shahidi wa Aiko, aliyeshangaa kwamba sikuwepo wakati wa ubatizo wa binti yangu, alimwambia Aiko kwamba atanitembelea. Nilighadhibika, lakini alipokuja nilimkaribisha tu kwa sababu ya uungwana wangu. Kwa sababu hiyohiyo, sikusema la aliposema kwamba angerudi juma lifuatalo. Ziara hizi ziliendelea kwa majuma, zikinighadhibisha sana hivi kwamba mwanzoni sikujifunza kitu kutokana na yale aliyosema. Ingawa hivyo, polepole mazungumzo yakanifanya nifikiri.
Nilianza kukumbuka mambo ambayo mama alikuwa akisema. Ijapokuwa alitaka kuabudiwa baada ya kifo, hakuwa na uhakika kuhusu maisha ya baada ya kifo. Jambo ambalo wazazi hutaka zaidi, yeye angesema, ni watoto wawe wenye fadhili kwao na kuwazungumzia kwa uchangamfu wakiwa wangali hai. Niliposoma maandiko kama vile Mhubiri 9:5, 10, na Waefeso 6:1, 2, na kuona kwamba Biblia hutia moyo jambo hilohilo, nilihisi kana kwamba sikuwa nimepofushwa tena kuelekea kweli. Mambo mengine ambayo mama alikuwa amenifundisha pia yalikuwa katika Biblia, kama vile ndiyo yangu iwe ndiyo na la yangu iwe la. (Mathayo 5:37) Nikijiuliza ni nini kingine ambacho Biblia hufundisha, nilikubali funzo la kawaida la Biblia.
Huzuni na mvurugo niliokuwa nimehisi maishani mwangu mwote ulianza kupotea kadiri nilipofanya maendeleo katika ujuzi wa Biblia. Nilipoanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, nilivutiwa sana. Huu ulikuwa ulimwengu mwingine. Watu walikuwa wa kweli, fadhili, na wenye urafiki, nao moyo wangu ukaitikia. Hasa nilisukumwa kujifunza juu ya rehema ya Yehova. Yeye husamehe kwa upendo watenda dhambi wote wenye kutubu. Naam, angesamehe makosa yangu yote ya zamani na kunisaidia kufurahia uhai mpya!
Mabadiliko Katika Maisha Yangu
Ingawa nilitaka kumtumikia Yehova, nilikuwa na ushirikiano mkubwa sana na ulimwengu wa vitumbuizo. Wakati huo nilikuwa katika miaka yangu ya 50, lakini bado nilikuwa nikicheza jukwaani. Pia nilikuwa kiongozi na mmoja wa wasimamizi wawili wa wanamuziki wa shamisen wakati Danjuro Ichikawa alipocheza Sukeroku kwenye Kabukiza. Kwa kuwa ni wachezaji wachache tu wa shamisen wawezao kuandaa mtindo unaoandamana na katoubushi unaohitajiwa kwa ajili ya Sukeroku, hakungekuwa na mtu wa kutwaa mahali pangu ikiwa ningeacha. Hivyo nilihisi nimetegwa.
Hata hivyo, Shahidi mmoja mzee-mzee, ambaye pia alihusika katika namna moja ya vitumbuizo vya kitamaduni vya Kijapani, aliniuliza ni kwa nini nilifikiri ilinipasa kuacha. “Lazima watu wafanye kazi ili wajitegemeze,” yeye akaeleza. Alinisaidia nione kwamba sikuwa nafanya lolote kinyume cha Maandiko na kwamba ningeweza kumtumikia Yehova na niendelee na michezo yangu.
Kwa muda fulani niliendelea kwenye Kabukiza, jumba kuu la michezo la Japani. Kisha maonyesho yakaanza kuwa katika usiku wa mikutano, kwa hiyo nikaomba nibadilishwe katika usiku mwingine. Hata hivyo, baada ya muda mfupi nyakati zetu za mikutano zikabadilika, na ningeweza kufaa kote kazini na mikutanoni. Lakini, ili nifike mikutanoni kwa wakati, mara nyingi ilinilazimu kuingia teksi upesi baada ya wonyesho kuisha badala ya kupumzika pamoja na wachezaji wengine kama ilivyokuwa desturi. Hatimaye, nikaamua kuacha.
Wakati huo tulikuwa tumefanya sana mazoezi kwa muda mrefu kwa ajili ya mfululizo wa michezo wa miezi sita katika majiji makubwa ya Japani. Kusema juu ya kuacha kungeleta matatizo mengi. Kwa hiyo, bila kutaja makusudio yangu, nilianza kumzoeza mtu fulani ili awe mwandamizi wangu. Ziara hiyo ya majiji ilipokamilika, nilimwelezea kila mtu aliyehusika kwamba nimetimiza madaraka yangu na kwamba nilikuwa naacha. Wengine walikasirika. Wengine walinilaumu kwa kuwa mwenye ujanja na kusababisha matatizo kimakusudi. Ulikuwa wakati mgumu kwangu, bali nilishikilia uamuzi wangu na nikaacha baada ya miaka 40 ya kucheza. Tangu wakati huo, nimefunza shamisen, na kufanya hivi huandaa mapato kidogo.
Kuishi Kupatana na Wakfu Wangu
Miaka michache mapema, nilikuwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Yehova Mungu. Nilibatizwa mnamo Agosti 16, 1980. Hisia inayonijaa sasa ni ile ya shukrani nyingi kwa Yehova. Najifikiria kuwa kama yule mwanamke Msamaria anayetajwa katika Biblia kwenye Yohana 4:7-42. Yesu aliongea naye kwa fadhili, naye akatubu. Vivyohivyo, Yehova, ambaye “huutazama moyo,” kwa fadhili alinionyesha njia, na kwa sababu ya rehema yake, nimeweza kuanza maisha mapya.—1 Samweli 16:7.
Katika Machi 1990, nilipokuwa na umri uliokaribia miaka 68, nikawa painia, kama vile wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova waitwavyo. Aiko pia ni painia, na watoto wake watatu vilevile. Walikua wakawa kama mama yao kupatana na ile methali ya Kijapani: “Mtoto wa chura ni chura.” Mume wa Aiko ni mzee Mkristo katika kutaniko. Mimi ni mwenye baraka kama nini kuzingirwa na familia yangu, wote wakitembea katika kweli, na kuwa na ndugu na dada wenye upendo katika kutaniko!
Nikiwa na shukrani kwa wazazi wangu wa kale, shukrani zangu nyingi zaidi zamwendea Yehova, ambaye amenifanyia mengi zaidi kuliko vile mwanadamu yeyote angeweza kunifanyia. Hasa, ni shukrani kwa rehema na faraja nyingi zake ambazo hunichochea kutaka kumsifu yeye kwa umilele wote.—Kama ilivyosimuliwa na Sawako Takahashi.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Nikifanya mazoezi, nilipokuwa na umri wa miaka minane
[Picha katika ukurasa wa 20]
Nikiwa na mama yangu mlezi
[Picha katika ukurasa wa 21]
Binti yangu alikuwa fahari ya maisha yangu
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nilimwabudu mama yangu mbele ya madhabahu hii ya familia
[Picha katika ukurasa wa 24]
Nikiwa na binti yangu, mume wake, na wajukuu wangu