Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Samehe Kutoka Katika Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Oktoba 15
    • 9, 10. Kwa nini hatupaswi kushangaa matatizo yakitokea kati ya akina ndugu?

      9 Katika Biblia, Mungu atuambia wazi kwamba tunaweza kutarajia hali ya kutokamilika katika kutaniko miongoni mwa ndugu na dada zetu. Kwa mfano, fikiria maneno ya Paulo yaliyorekodiwa kwenye Wakolosai 3:13: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia.”

      10 Jambo muhimu ni kwamba hapo Biblia inatukumbusha juu ya uhusiano uliopo baina ya msamaha wa Mungu na wajibu na uhitaji wetu wa kuwasamehe wengine. Kwa nini ni vigumu kusamehe? Kwa sababu Paulo alikiri kwamba mtu anaweza kuwa na “sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine.” Alitambua kwamba sababu kama hizo zingekuwapo. Ni lazima zilikuwapo katika karne ya kwanza, hata miongoni mwa Wakristo “watakatifu,” waliokuwa na ‘tumaini ambalo limewekwa akiba kwa ajili yao katika mbingu.’ (Wakolosai 1:2, 5) Basi, je, tuseme kwamba hali ingekuwa tofauti leo ambapo Wakristo wengi wa kweli hawana ushuhuda wa roho kwamba wao ni “wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa”? (Wakolosai 3:12) Kwa hiyo, hatupaswi kukata kauli ya kwamba kuna kasoro fulani mbaya sana ikiwa katika kutaniko letu kuna sababu za kulalamika—kuumizwa kwa sababu ya makosa ya kweli au yale yanayoonwa kuwa makosa.

      11. Mwanafunzi Yakobo alitutahadharisha juu ya nini?

      11 Maneno ya Yakobo ndugu-nusu ya Yesu pia yaonyesha kwamba ni lazima tutarajie kwamba angalau mara kwa mara tutapata hali ambazo tutahitaji kuwasamehe ndugu zetu. “Ni nani aliye mwenye hekima na mwenye kuelewa miongoni mwenu? Acheni aonyeshe kutokana na mwenendo wake bora kazi zake kwa upole ulio wa hekima. Lakini ikiwa nyinyi mna wivu wenye uchungu na ugomvi katika mioyo yenu, msiwe mkijigamba na kusema uwongo dhidi ya kweli.” (Yakobo 3:13, 14) “Wivu wenye uchungu na ugomvi” katika mioyo ya Wakristo wa kweli? Ndiyo, maneno ya Yakobo yaonyesha wazi kwamba mambo hayo yalikuwa yametokea katika kutaniko la karne ya kwanza nayo yatatokea leo.

      12. Kulitokea tatizo gani katika kutaniko la kale la Filipi?

      12 Mfano halisi ulihusu Wakristo wawili watiwa-mafuta ambao walikuwa na sifa nzuri ya kufanya kazi kwa bidii pamoja na Paulo. Huenda unakumbuka kusoma juu ya Euodia na Sintike, washiriki wa kutaniko la Filipi. Japo andiko la Wafilipi 4:2, 3 halifafanui kisa chao kindani, linaonyesha kwamba kulikuwa na tatizo kati yao. Je, tatizo hilo lilianza kwa maneno yasiyo yenye fadhili yaliyosemwa bila kufikiri, jambo lililoonwa kuwa madharau dhidi ya mtu wa ukoo, au uthibitisho fulani wa wivu wenye ushindani? Liwe lilikuwa nini, tatizo hilo lilipata kuwa baya sana hivi kwamba Paulo alilisikia akiwa mbali sana kule Roma. Huenda dada hao wawili wa kiroho walinyamaziana, na kufanya waepukane mikutanoni au kuambia rafiki zao maneno mabaya juu ya yule mwingine.

      13. Yaelekea Euodia na Sintike walitatuaje tatizo lao, tukipata somo gani?

      13 Je, umewahi kusikia jambo kama hilo, likifanana na jambo lililotokea katika kutaniko lenu au lililokuhusisha? Huenda tatizo kama hilo lipo sasa kwa kiasi fulani. Tunaweza kufanya nini? Katika kile kisa cha zamani, Paulo aliwahimiza dada hao wawili waliojiweka wakfu “wawe wenye akili ileile katika Bwana.” Huenda walikubali kuzungumzia jambo hilo, kusuluhisha tatizo hilo, kuonyesha utayari wa kusameheana, kisha kwa kweli kuiga mtazamo wa Yehova wa kusamehe. Hakuna sababu ya kufikiria vingine ila kwamba Euodia na Sintike walifaulu, nasi pia twaweza kufaulu. Mtazamo kama huo wa kusamehe waweza kutumika leo kwa mafanikio.

      Fanya Amani—Samehe

      14. Kwa nini mara nyingi inawezekana na ni bora kuziachilia tofauti za kibinafsi?

      14 Ni nini kinachohitajika kwa kweli ili usamehe kunapokuwa na tatizo kati yako na Mkristo mwingine? Kwa wazi, hakuna hata njia moja rahisi, lakini Biblia hutoa vielelezo vizuri na mashauri halisi. Pendekezo kuu—ingawa si rahisi kukubaliwa na kutumiwa—ni kusahau tu jambo hilo, kuliachilia tu. Mara nyingi tatizo linapozuka, kama ilivyokuwa kati ya Euodia na Sintike, kila mtu huhisi kwamba yule mwingine ndiye mwenye makosa au ndiye wa kulaumiwa zaidi. Basi katika hali kama hiyo, huenda ukafikiri kwamba yule Mkristo mwingine ndiye mwenye makosa au ndiye wa kulaumiwa zaidi. Lakini, je, huwezi kuliachilia tu jambo hilo kwa kusamehe? Tambua kwamba ikiwa yule Mkristo mwingine ndiye amechangia zaidi hali hiyo au ndiye pekee mwenye makosa, japo haielekei kuwa hivyo, wewe uko katika hali nzuri kabisa ya kuliachilia jambo hilo kwa kusamehe na kulimaliza.

      15, 16. (a) Mika alimfafanuaje Yehova? (b) Inamaanisha nini kwamba Mungu ‘anaachilia kosa’?

      15 Tusisahau kwamba Mungu ndiye kielelezo chetu katika kusamehe. (Waefeso 4:32–5:1) Kuhusu kielelezo cha Mungu cha kuachilia kosa, nabii Mika aliandika: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema.”—Mika 7:18.

      16 Kwa kumfafanua Yehova kuwa mwenye ‘kuachilia kosa,’ Biblia haisemi kwamba yeye hawezi kuyasahau makosa, kwa njia fulani akisahau makosa mengine. Fikiria visa vya Samsoni na Daudi, wote wawili walifanya makosa mazito. Mungu aliweza kuzikumbuka dhambi hizo muda mrefu baadaye; na hata sisi twajua baadhi ya dhambi zao kwa sababu Yehova alifanya ziandikwe katika Biblia. Na bado, Mungu wetu mwenye kusamehe aliwaonyesha rehema, akiwataja kuwa vielelezo vya imani tunaopaswa kuiga.—Waebrania 11:32; 12:1.

      17. (a) Ni hali gani iwezayo kutusaidia kuachilia makosa ya wengine? (b) Tukijaribu kufanya hivyo, tutakuwa tukimwigaje Yehova? (Ona kielezi-chini.)

      17 Naam, Yehova aliweza ‘kuyaachilia’a makosa, kama ambavyo Daudi alimwomba tena na tena ayaachilie. (2 Samweli 12:13; 24:10) Je, tunaweza kumwiga Mungu katika jambo hilo, kwa kuwa tayari kuachilia mambo yenye kuudhi na makosa ambayo watumishi wenzetu wanafanya wakiwa wanadamu wasiokamilika? Ebu wazia ukiwa katika ndege inayoondoka kwenye uwanja. Unapotazama nje, karibu na njia ya ndege unaona mtu unayemfahamu akitoa nje ulimi wake kwa njia ya kitoto yenye kuudhi. Unajua kwamba alikuwa amekasirika na huenda ni wewe anayekufanyia dhihaka hiyo. Au huenda hata si wewe anayekufikiria. Hata hivyo, ndege hiyo izungukapo ikipaa juu, unapita juu sana ya mwanamke yule, ambaye sasa anaonekana kama doa tu. Baada ya muda wa saa moja uko umbali wa mamia ya kilometa, na tayari umesahau kabisa dhihaka yake. Vivyo hivyo, mara nyingi tutasaidiwa kusamehe tukijaribu kuiga Yehova na kuliachilia kosa hilo kwa hekima. (Mithali 19:11) Je, kosa hilo halitaonekana kuwa jambo dogo sana miaka kumi ijayo au miaka mia mbili katika Milenia? Mbona usiliachilie tu?

      18. Tukiona kama hatuwezi kuachilia kosa, tunaweza kutumia shauri gani?

      18 Katika visa vichache, huenda umesali juu ya jambo hilo na kujaribu kusamehe, lakini unaona kwamba huwezi kusamehe? Ufanyeje sasa? Yesu alihimiza kwamba umwendee yule aliyekukosea na kujaribu kusuluhisha tofauti zenu kwa faragha ili mfanye amani. “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.”—Mathayo 5:23, 24.

      19. Twapaswa kuwa na mtazamo gani na twapaswa kuepuka mtazamo gani tunapofuatia amani na ndugu yetu?

      19 Jambo la maana ni kwamba Yesu hakusema umwendee ndugu yako ukamsadikishe kwamba wewe huna kosa na kwamba ni yeye aliyekosea. Labda alikosea. Lakini yaelekea sana kwamba kila mmoja wenu alikosea kwa njia fulani. Hata hivyo, lengo si kumlazimisha yule mwingine akubali kosa, au anyenyekee. Ikiwa hilo ndilo lengo lako la mazungumzo, haielekei utafaulu. Wala si lazima lengo liwe kupitia kila kijambo kidogo cha kosa lililofanywa au linalowaziwa tu. Wakati mazungumzo matulivu katika roho ya upendo wa Kikristo yafunuapo kwamba kwa kusikitisha ni kutoelewana ndiko kumesababisha tatizo, nyote wawili mwaweza kujaribu kusuluhisha tatizo hilo. Hata kama hamkubaliani kabisa kwenye mazungumzo hayo, je, ni lazima mkubaliane nyakati zote? Je, haingekuwa afadhali ikiwa angalau mwakubaliana kwamba nyote wawili mnataka kumtumikia kwa unyofu Mungu mwenye kusamehe? Ukabilipo hali hiyo, huenda ikawa rahisi kwa kila mmoja kusema kutoka moyoni, “Pole kwamba kwa sababu ya kutokamilika tumekuwa na tofauti hii. Tafadhali tuiachilie.”

      20. Twaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha mitume?

      20 Kumbuka kwamba mitume walikuwa na tofauti zao, kama wakati ambapo wengine wao walitaka utukufu zaidi. (Marko 10:35-39; Luka 9:46; 22:24-26) Jambo hilo lilisababisha uvutano, labda wengine wakaumizwa, au hata kuudhika sana. Lakini wao waliachilia tofauti hizo na kuendelea kufanya kazi pamoja. Baadaye mmoja wao aliandika: “Yeye ambaye angependa uhai na kuona siku zilizo njema, acheni azuie ulimi wake kutokana na lililo baya na midomo yake isiseme udanganyo, lakini acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia.”—1 Petro 3:10, 11.

      21. Yesu alitoa shauri gani muhimu juu ya kusamehe?

      21 Mwanzoni tulishughulikia sehemu moja ya mazungumzo yetu: Mungu alitusamehe dhambi nyingi tulizofanya wakati uliopita, basi tunapaswa kumwiga na kuwasamehe ndugu zetu. (Zaburi 103:12; Isaya 43:25) Lakini kuna sehemu nyingine ya mazungumzo hayo. Baada ya kuandaa ile sala ya kigezo, Yesu alisema: “Ikiwa mwasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa kimbingu atawasamehe nyinyi pia.” Zaidi ya mwaka mmoja baadaye, alirudia kutaja wazo kuu la jambo hilo, akiwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia husamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Mathayo 6:12, 14; Luka 11:4) Kisha, siku chache tu kabla ya kifo chake, Yesu aliongezea kusema: “Msimamapo mkisali, sameheni chochote kile mlicho nacho dhidi ya yeyote; ili Baba yenu aliye katika mbingu apate kuwasamehe makosa yenu nyinyi pia.”—Marko 11:25.

      22, 23. Utayari wetu wa kusamehe waweza kuathirije wakati wetu ujao?

      22 Naam, kuendelea kupokea msamaha wa Mungu kwategemea sana utayari wetu wa kuwasamehe wengine. Tatizo la kibinafsi likizuka kati ya Wakristo, jiulize, ‘Je, si ni muhimu zaidi kupata msamaha wa Mungu kuliko kuthibitisha kwamba ndugu au dada alikosea kidogo tu, au kukazia kutokamilika fulani kwa wanadamu?’ Unajua jibu.

      23 Lakini, namna gani ikiwa jambo hilo ni zito kuliko kosa au tatizo dogo tu la kibinafsi? Na shauri la Yesu linalopatikana kwenye Mathayo 18:15-18 latumika wakati gani? Ebu tuchunguze mambo hayo.

  • Unaweza Kumpata Ndugu Yako
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Oktoba 15
    • Unaweza Kumpata Ndugu Yako

      “Nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.”—MATHAYO 18:15.

      1, 2. Yesu alitoa shauri gani lenye kutumika kuhusu kushughulikia makosa?

      KUKIWA kumebaki muda unaopungua mwaka mmoja wa huduma yake, Yesu alifundisha wanafunzi wake masomo muhimu. Unaweza kuyasoma katika Mathayo sura ya 18. Mojawapo ya masomo hayo lilikuwa ni umuhimu wa kuwa wanyenyekevu kama watoto. Kisha akakazia kwamba ni lazima tuepuke kukwaza ‘mmoja wa wadogo hao’ na kwamba tunapaswa kujaribu kuwapata ‘wadogo hao’ ili kwamba wasiangamie. Kisha Yesu akaongezea shauri lenye kutumika na lenye manufaa sana juu ya namna ya kutatua matatizo kati ya Wakristo.

      2 Huenda unakumbuka maneno yake: “Ndugu yako akifanya dhambi, nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako. Lakini ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja nawe mmoja au wawili zaidi, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila jambo lipate kuthibitishwa. Ikiwa yeye hawasikilizi wao, liambie kutaniko. Ikiwa hasikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” (Mathayo 18:15-17) Tunapaswa kutumia shauri hilo wakati gani, na tunapaswa kuwa na mtazamo upi tunapofanya hivyo?

      3. Kwa ujumla twapaswa kuwa na mtazamo gani juu ya makosa ya wengine?

      3 Makala iliyotangulia ilikazia kwamba kwa kuwa sisi sote hatujakamilika na tuna mwelekeo wa kufanya makosa, tunahitaji kujitahidi kuwa wenye kusamehe. Hasa wakati ambapo tumeumizwa na jambo ambalo Mkristo mwenzetu alisema au kutenda. (1 Petro 4:8) Mara nyingi ni bora kuliachilia tu kosa hilo—kusamehe na kusahau. Tunaweza kuona kusamehe kuwa kuchangia amani katika kutaniko la Kikristo. (Zaburi 133:1; Mithali 19:11) Lakini, huenda kuna pindi ambapo huenda ukahisi kwamba ni lazima usuluhishe jambo fulani na ndugu au dada yako ambaye alikuumiza. Katika hali kama hiyo, maneno ya Yesu yaliyo juu yaandaa mwongozo.

      4. Kwa ujumla, tunaweza kutumiaje andiko la Mathayo 18:15 kuhusu makosa ya wengine?

      4 Yesu alishauri kwamba “ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake.” Hilo ni jambo la hekima. Tafsiri nyingine za Kijerumani zasema, uwasilishe kosa lake “mbele ya macho manne,” yaani macho yako na macho yake. Unapowasilisha tatizo kwa fadhili na kwa faragha, mara nyingi ni rahisi kutatuliwa. Ndugu ambaye alitenda au kusema jambo lenye kuudhi au lisilo la fadhili huenda akakiri mara moja kosa hilo ukiwa peke yako. Iwapo wengine wanasikiliza, asili ya wanadamu wasiokamilika huenda ikamfanya awe na mwelekeo wa kukana kuwa alitenda kosa au ajaribu kujitetea juu ya tendo lake. Lakini ukiwasilisha suala hilo “mbele ya macho manne,” unaweza kupata kwamba tatizo lilikuwa kutoelewana wala si dhambi au kosa la kimakusudi. Nyote mnapogundua kwamba kumbe ni kutoelewana, mnaweza kulisuluhisha, bila kuachilia jambo dogo liwe kubwa na kuharibu uhusiano wenu. Basi kanuni inayopatikana kwenye Mathayo 18:15 inaweza kutumiwa hata kusuluhisha makosa madogo-madogo katika maisha ya kila siku.

      Alimaanisha Nini?

      5, 6. Kulingana na muktadha, andiko la Mathayo 18:15 linarejezea dhambi za aina gani, na ni nini kinachoonyesha jambo hilo?

      5 Shauri la Yesu hasa lilihusu mambo mazito zaidi. Yesu alisema: “Ndugu yako akifanya dhambi.” Kwa ujumla, “dhambi” inaweza kuwa kosa lolote au kasoro yoyote. (Ayubu 2:10; Mithali 21:4; Yakobo 4:17) Lakini, muktadha wadokeza kwamba ni lazima Yesu alimaanisha dhambi nzito. Ilikuwa nzito kiasi cha kwamba ingeweza kufanya mkosaji aonwe “kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Maneno hayo yadokeza nini?

      6 Wanafunzi wa Yesu waliosikia maneno hayo walijua kwamba Wayahudi wenzao hawakuwa na shughuli na watu wasio Wayahudi. (Yohana 4:9; 18:28; Matendo 10:28) Nao bila shaka waliwaepuka wakusanya-kodi, wanaume Wayahudi ambao waligeuka wakawa wanawadhulumu watu. Basi andiko la Mathayo 18:15-17 lilikuwa likirejezea hasa dhambi nzito, si kuumizwa au makosa madogo-madogo ya kibinafsi ambayo unaweza kusamehe tu na kusahau.—Mathayo 18:21, 22.a

      7, 8. (a) Ni dhambi za aina gani zinazohitaji kushughulikiwa na wazee? (b) Ni dhambi za aina gani zingeweza kusuluhishwa kati ya Wakristo wawili, kwa kupatana na Mathayo 18:15-17?

      7 Katika Sheria, dhambi nyingine hazikuhitaji msamaha tu wa mtu aliyekosewa. Kukufuru, uasi, ibada ya sanamu, na dhambi za kingono za uasherati, uzinzi, na ugoni wa jinsia moja zilipasa kuripotiwa kwa wazee (au makuhani) wazishughulikie. Na ndivyo ilivyo katika kutaniko la Kikristo. (Mambo ya Walawi 5:1; 20:10-13; Hesabu 5:30; 35:12; Kumbukumbu la Torati 17:9; 19:16-19; Mithali 29:24) Lakini, ona kwamba aina za dhambi ambazo Yesu alirejezea zingeweza kusuluhishwa kati ya watu wawili. Kwa mfano: Kwa sababu ya hasira au wivu, mtu amchongea mwenzake. Mkristo achukua kandarasi ya kufanya kazi fulani akitumia vifaa fulani hususa na kumaliza kazi hiyo kufikia tarehe fulani. Mkristo mwingine akubali kwamba atalipa deni kufikia tarehe fulani. Mtu aahidi kwamba mwajiri wake akimzoeza kazi, hatashindana naye (hata kama anabadili kazi) wala hatajaribu kuchukua wateja wa mwajiri wake kwa muda fulani au katika eneo fulani.b Ikiwa ndugu hawezi kutimiza ahadi yake na haonyeshi toba kwa makosa kama hayo, kwa hakika hilo lingekuwa jambo zito. (Ufunuo 21:8) Lakini makosa kama hayo yanaweza kusuluhishwa kati ya watu hao wawili wanaohusika.

      8 Hata hivyo, wewe ungetatuaje jambo hilo? Mara nyingi maneno ya Yesu yameonwa kuwa yenye hatua tatu. Ebu tuchunguze kila hatua. Badala ya kuziona kama sheria kali zisizobadilikana, jaribu kupata maana ya maneno ya Yesu, bila kusahau lengo lako lenye upendo.

      Jitahidi Kumpata Ndugu Yako

      9. Tunapaswa kuzingatia nini tutumiapo Mathayo 18:15?

      9 Yesu alianza kwa kusema: “Ndugu yako akifanya dhambi, nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.” Kwa wazi, hii si hatua inayotegemea mambo ya kushuku tu. Unapaswa kuwa na uthibitisho au habari hususa uwezayo kutumia ili kusaidia ndugu yako aone kwamba alikosea na anahitaji kunyosha mambo. Ni vizuri kuchukua hatua haraka iwezekanavyo, bila kuachilia jambo hilo likue au mtazamo wake uzidi kuwa mbaya. Na usisahau kwamba kufikiria sana jambo hilo kwaweza kukuumiza pia. Na kwa kuwa mazungumzo yatakuwa kati yenu mkiwa wawili tu, epuka kuzungumza na wengine kabla ya kuongea naye ili uonewe huruma au ili ujionyeshe kuwa bora. (Mithali 12:25; 17:9) Kwa nini? Kwa sababu ya lengo lako.

      10. Ni nini kitakachotusaidia tumpate ndugu yetu?

      10 Lengo lako lapasa kuwa kumpata ndugu yako, wala si kumwadhibu, kumshushia heshima, au kumwumiza. Ikiwa kweli ametenda kosa, uhusiano wake na Yehova umo hatarini. Kwa kweli unataka abaki akiwa ndugu yako wa Kikristo. Uwezekano wa kufanikiwa utaongezeka ikiwa unabaki mtulivu, ukiepuka maneno makali au hali ya kushtaki-shtaki katika mazungumzo yenu ya faragha. Katika kikao hicho chenye upendo, kumbuka kwamba nyote wawili ni wanadamu wenye dhambi ambao hawajakamilika. (Waroma 3:23, 24) Atambuapo kwamba hujapiga porojo kumhusu na kwamba kwa kweli unataka kusaidia, huenda mkapata suluhisho haraka. Mfikio huo wa wazi na wenye fadhili hasa utakuwa njia ya hekima inapotokea kwamba kumbe nyote wawili mlikosea kwa kadiri fulani au kwamba tatizo kubwa lilikuwa ni kutoelewana.—Mithali 25:9, 10; 26:20; Yakobo 3:5, 6.

      11. Hata kama mkosaji hatusikilizi tunaweza kufanya nini?

      11 Ukimsaidia aone kwamba kosa lilifanyika na kwamba ni kosa zito, huenda akasukumwa kutubu. Lakini, kwa kweli kiburi chaweza kutatiza. (Mithali 16:18; 17:19) Kwa hiyo hata kama mwanzoni hakubali kosa alilofanya na kutubu, unaweza kungoja kidogo kabla ya kufuatilia jambo hilo tena. Yesu hakusema ‘nenda mara moja tu ufunue wazi kosa lake.’ Kwa sababu hiyo ni dhambi ambayo mnaweza kusuluhisha, fikiria kumwendea tena kwa roho ya Wagalatia 6:1 na “mbele ya macho manne.” Huenda ukafaulu. (Linganisha Yuda 22, 23.) Lakini, namna gani ikiwa una hakika kwamba dhambi imefanywa, naye amekataa kukubali?

      Kupata Msaada wa Watu Wakomavu

      12, 13. (a) Yesu alitaja hatua gani ya pili ya kushughulikia makosa? (b) Kuna tahadhari zipi zifaazo unapochukua hatua hiyo?

      12 Je, ungependa wengine wakuachilie kwa urahisi tu ikiwa una hatia ya kutenda kosa zito? La. Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba baada ya hatua ya kwanza, usiache kujaribu kumpata ndugu yako, ili kumfanya aendelee kuwa na umoja pamoja nawe na wengine katika kumwabudu Mungu ifaavyo. Yesu alitaja hatua ya pili: “Ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja nawe mmoja au wawili zaidi, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila jambo lipate kuthibitishwa.”

      13 Alisema chukua “mmoja au wawili zaidi.” Yeye hakusema kwamba baada ya kuchukua hatua ya kwanza, uko huru kuongea na wengine juu ya tatizo hilo, kuongea na mwangalizi asafiriye, au kuandikia akina ndugu juu ya tatizo hilo. Hata kama una hakika kabisa kwamba kosa hilo lilifanyika, bado halijathibitishwa kabisa. Haitafaa kueneza habari za uwongo ambazo zingeweza kugeuka kuwa uchongezi kwa upande wako. (Mithali 16:28; 18:8) Lakini Yesu alisema uchukue mmoja au wawili zaidi. Kwa nini? Nao wanaweza kuwa nani?

      14. Twaweza kuchukua nani katika hatua ya pili?

      14 Unajaribu kumpata ndugu yako kwa kumsadikisha kwamba amefanya dhambi na kwa kumfanya atubu ili awe na amani pamoja nawe na pamoja na Mungu. Ili kutimiza jambo hilo, ingekuwa afadhali kama huyo “mmoja au wawili” walishuhudia kosa likifanywa. Labda walikuwapo kosa lilipofanywa, au wana habari yenye msingi mzuri juu ya jambo lililofanywa (au halikufanywa) katika suala la kibiashara. Ikiwa hakuna mashahidi kama hao, wale unaowachukua huenda wakawa wenye ujuzi wa suala linalozungumziwa na basi wanaweza kuthibitisha kama jambo lililotendeka kwa kweli ni kosa. Isitoshe, ikihitajiwa baadaye, wao wanaweza kuwa mashahidi wa jambo lililosemwa, wakithibitisha mambo yaliyosemwa na jitihada iliyofanywa. (Hesabu 35:30; Kumbukumbu la Torati 17:6) Basi hao si watu wasiohusika tu, waamuzi; lakini, kuwapo kwao ni kusaidia kumpata ndugu yako na ndugu yao.

      15. Kwa nini wazee Wakristo wanaweza kusaidia ikiwa ni lazima tuchukue hatua ya pili?

      15 Usifikiri kwamba wale unaowachukua ni lazima wawe wazee kutanikoni. Lakini, wanaume wakomavu ambao ni wazee wanaweza kuchangia kwa sababu ya sifa zao za kiroho. Wazee kama hao ni “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:1, 2) Wao wana ujuzi wa kusababu na akina ndugu na dada na kuwarekebisha. Na mkosaji ana sababu nzuri ya kuonyesha uhakika katika “zawadi zikiwa wanadamu.” c (Waefeso 4:8, 11, 12) Kuzungumzia mambo mbele ya watu wakomavu kama hao na kusali pamoja nao kwaweza kuleta mazingira mapya na kutatua suala lililoonekana kama haliwezi kutatuliwa.—Linganisha Yakobo 5:14, 15.

      Jitihada ya Mwisho ya Kumpata Ndugu Yako

      16. Yesu alitaja hatua gani ya tatu?

      16 Hatua ya pili ikishindwa kusuluhisha suala hilo, bila shaka waangalizi wa kutaniko wanahusika katika hatua ya tatu. “Ikiwa yeye hawasikilizi wao [yule mmoja au wale wawili], liambie kutaniko. Ikiwa hasikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Hilo lahusisha nini?

      17, 18. (a) Ni kielelezo gani kinachotusaidia kuelewa kinachomaanishwa na ‘kuliambia kutaniko’? (b) Tunatumiaje hatua hii leo?

      17 Mwelekezo huo haumaanishi kuleta dhambi hiyo au kosa hilo kwenye mkutano wa kawaida au kwenye mkutano wa pekee wa kutaniko lote. Twaweza kujua utaratibu ufaao kutokana na Neno la Mungu. Ona jinsi mambo yalivyopasa kufanywa katika Israeli la kale kuhusu uasi, ulafi, na ulevi: “Mtu akiwa na mwana mkaidi, mshupavu, asiyetii sauti ya baba yake, wala sauti ya mama yake, nao wajapomwadhibu hawasikizi, ndipo babaye na mamaye na wamkamate, na kumpeleka kwa wazee wa mji wake, katika lango la mahali pake; wawaambie wazee wa mji wake, Huyu mwana wetu ni mkaidi, mshupavu, hasikizi sauti yetu; ni mwasherati, tena ni mlevi. Waume wote wa mji wake na wamtupie mawe.”—Kumbukumbu la Torati 21:18-21, italiki ni zetu.

      18 Dhambi za mtu huyo hazikusikilizwa na kuamuliwa na taifa lote wala na kabila lake lote. Badala yake, “wazee” waliotambuliwa walishughulikia dhambi hiyo wakiwa wawakilishi wa kutaniko. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 19:16, 17 kuhusu kesi iliyoshughulikiwa na ‘makuhani na waamuzi waliokuwapo siku hizo.’) Leo vilevile, inapokuwa lazima kuchukua hatua ya tatu, wazee, wanaowakilisha kutaniko, hushughulikia jambo hilo. Wana lengo lilelile, la kumpata ndugu Mkristo ikiwezekana. Wao huonyesha hilo kwa kuwa wasiopendelea, bila kuhukumu kesi kimbele au kubagua.

      19. Wazee wanaochaguliwa kusikiliza kesi hiyo watajitahidi kufanya nini?

      19 Wao watajitahidi kupima mambo na kusikiliza mashahidi wanaohitajiwa ili kuthibitisha kama kweli dhambi imefanywa (au inaendelea kufanywa). Wanataka kulinda kutaniko dhidi ya ufisadi na kuzuia roho ya ulimwengu. (1 Wakorintho 2:12; 5:7) Kwa kupatana na sifa zao za Kimaandiko, wao watajitahidi “kuhimiza kwa bidii kwa fundisho lililo lenye afya na pia kukaripia wale ambao hupinganisha.” (Tito 1:9) Tunatumaini kwamba mkosaji hatakuwa kama Waisraeli ambao nabii wa Yehova aliandika hivi kuwahusu: “Nilipoita hamkuitika; niliponena, hamkusikia; bali mlitenda yaliyo mabaya machoni pangu, mlichagua mambo nisiyoyafurahia.”—Isaya 65:12.

      20. Yesu alisema ni lazima nini litendeke ikiwa mtenda-dhambi anakataa kusikiliza na kutubu?

      20 Hata hivyo, katika visa vichache, mtenda-dhambi huonyesha mtazamo uleule. Ikiwa ndivyo ilivyo, mwelekezo wa Yesu ni wazi: “Mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Bwana hakupendekeza tuwe wakatili au kuwa na lengo lolote la kuumiza. Hata hivyo, hakuna utatanishi wowote kuhusu mwelekezo wa mtume Paulo wa kutenga watenda-dhambi wasiotubu kutoka kutanikoni. (1 Wakorintho 5:11-13) Hata hatua hiyo huenda hatimaye ikatimiza lengo la kumpata mtenda-dhambi.

      21. Kunabaki uwezekano gani kwa mtu ambaye ametengwa na kutaniko?

      21 Tunaweza kuona uwezekano wa kumpata tena kutokana na mfano wa Yesu wa mwana mpotevu. Kama ilivyoonyeshwa, baada ya kukaa kwa muda fulani mbali na ushirika wenye upendo katika nyumba ya babake, mtenda-dhambi huyo ‘alirudiwa na fahamu zake.’ (Luka 15:11-18) Paulo alimtajia Timotheo kwamba wakosaji wengine wangetubu hatimaye na “kurudiwa na fahamu zao nzuri kutoka katika mtego wa Ibilisi.” (2 Timotheo 2:24-26) Twatumaini kwamba watu wanaotenda dhambi bila kutubu na ambao ni lazima watengwe na kutaniko watahisi wamepoteza kitu—kibali cha Mungu na vilevile ushirika mchangamfu na mawasiliano na Wakristo waaminifu-washikamanifu—na kurudiwa na fahamu zao.

      22. Bado tunawezaje kumpata ndugu yetu?

      22 Yesu hakuwaona watu wa mataifa na wakusanya-kodi kuwa watu wasioweza kukombolewa. Mmojawapo wa wakusanya-kodi, Mathayo Lawi, alitubu, ‘akamfuata Yesu’ kwa moyo mweupe na hata akachaguliwa kuwa mtume. (Marko 2:15; Luka 15:1) Basi, leo mtenda-dhambi ‘asiposikiliza hata kutaniko’ na kutengwa, tunaweza kungoja na kuona ikiwa, baada ya muda fulani, atatubu na kunyosha njia zake. Anapofanya hivyo na kuwa mshiriki wa kutaniko tena, basi tutafurahi kwamba tumempata tena ndugu yetu katika ushirika wa ibada ya kweli.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki