Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mfanye Yehova Kuwa Tumaini Lako
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
    • Maana ya Kumtumaini Yehova

      18, 19. Biblia inatumia maneno gani kututia moyo tumtumaini Yehova, lakini watu fulani wana maoni gani yasiyofaa kuhusiana na hilo?

      18 Neno la Mungu linatuhimiza hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Maneno hayo mazuri yanatupa uhakika kama nini! Kwa kweli, hakuna mwingine katika ulimwengu wote ambaye anatumainika zaidi kuliko Baba yetu mpendwa wa mbinguni. Hata hivyo, ingawa ni rahisi kusoma maneno haya katika kitabu cha Mithali, huenda isiwe rahisi kuyatenda.

      19 Wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu maana ya kumtumaini Yehova. Wengine hufikiri kwamba kumtumaini Yehova kunamaanisha kuwa na hisia fulani yenye kufurahisha ambayo huchemka moyoni mwao. Huenda wengine wakafikiri kumtumaini Mungu humaanisha kwamba tunaweza kutarajia atukinge na taabu zote, atatue matatizo yetu yote, na atuondolee majaribu yetu mara moja kama tunavyotaka! Lakini maoni hayo hayana msingi. Kuwa na tumaini kunahusisha mengi zaidi kuliko kuwa na hisia fulani, na si jambo la kuwaziwa tu. Kwa watu wazima, kuwa na tumaini kunahusisha kufanya maamuzi baada ya kuyafikiria kwa makini.

      20, 21. Kumtumaini Yehova kunahusisha nini? Toa mfano.

      20 Ona tena jinsi Mithali 3:5 inavyosema. Inatofautisha kumtumaini Yehova na kutegemea akili zetu wenyewe, ikionyesha kwamba hatuwezi kufanya yote mawili. Je, hiyo inamaanisha kwamba haturuhusiwi kutumia nguvu zetu za uelewevu? La, kwa kuwa Yehova ndiye aliyetupa nguvu hizo na anatarajia tuzitumie kumtumikia. (Waroma 12:1) Lakini sisi hutegemea nini? Ikiwa kufikiri kwetu hakupatani na kwa Yehova, je, sisi tunakubali kwamba hekima yake ni ya juu sana kuliko yetu? (Isaya 55:8, 9) Kumtumaini Yehova humaanisha kuacha kufikiri kwake kuongoze kufikiri kwetu.

      21 Kwa mfano: Wazia mtoto mdogo akiwa ameketi kwenye kiti cha nyuma cha gari huku wazazi wake wakiwa mbele. Baba yake ndiye anayeendesha gari hilo. Matatizo yakitokea wakati wa safari, labda kuhusu barabara inayofaa au hali ya hewa au hali ya barabara, mtoto mtiifu na mwenye kutumaini wazazi atatendaje? Je, atawaamuru la kufanya, akimwambia baba yake jinsi ya kuendesha gari? Je, atatilia shaka uamuzi wa wazazi wake au akatae kusikiliza anapoambiwa aendelee kuketi akiwa amejifunga mkanda wa usalama? La, kwa kawaida yeye atawatumaini wazazi wake washughulikie mambo hayo hata ingawa wao si wakamilifu. Yehova ni Baba yetu mkamilifu. Je, hatupaswi kumtumaini kabisa, hasa tunapokabili hali ngumu?—Isaya 30:21.

      22, 23. (a) Kwa nini tunapaswa kumtumaini Yehova tunapokabili matatizo, na tunawezaje kufanya hivyo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      22 Hata hivyo, andiko la Mithali 3:6 linaonyesha kwamba tunapaswa ‘kumkiri Yehova katika njia zetu zote,’ si wakati tu tunapokabili hali ngumu. Kwa hiyo maamuzi tunayofanya kila siku yanapaswa kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova. Matatizo yanapotokea, hatupaswi kuvunjika moyo, kushtuka, au kukataa mwongozo wa Yehova kuhusu jinsi ya kushughulikia mambo kwa njia bora zaidi. Tunapaswa kuona matatizo kuwa nafasi ya kutetea enzi kuu ya Yehova, kuchangia kumthibitisha Shetani kuwa mwongo, na kusitawisha utii na sifa nyingine zinazompendeza Yehova.—Waebrania 5:7, 8.

      23 Tunaweza kuonyesha tumaini letu kwa Yehova hata tukitishwa na vizuizi vyovyote vile. Tunaonyesha hivyo kwa sala zetu na jinsi tunavyotegemea mwongozo wa Neno la Yehova na tengenezo lake. Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova hasa tunapokabili matatizo ya ulimwengu huu? Habari hii itazungumziwa katika makala yetu inayofuata.

  • Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za Taabu
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
    • Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za Taabu

      “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.”—ZABURI 46:1, Biblia Habari Njema.

      1, 2. (a) Ni mfano gani unaoonyesha haitoshi tu kudai kwamba tunamtumaini Mungu? (b) Kwa nini tunapaswa kufanya mengi zaidi kuliko kusema tu kwamba tunamtumaini Yehova?

      NI RAHISI mtu kudai kwamba anamtumaini Mungu, lakini ni vigumu kuonyesha hivyo kwa matendo. Kwa mfano, usemi, “In God We Trust” (yaani, Tunamtumaini Mungu) umeonekana kwa muda mrefu kwenye noti na sarafu za Marekani.a Katika mwaka wa 1956, Bunge la Marekani lilipitisha sheria iliyotangaza usemi huo kuwa wito wa taifa la Marekani. Jambo la kushangaza ni kwamba watu wengi, si katika nchi hiyo tu bali ulimwenguni kote, hutumaini zaidi pesa na mali kuliko wanavyomtumaini Mungu.—Luka 12:16-21.

      2 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunapaswa kufanya mengi zaidi kuliko kusema tu kwamba tunamtumaini Yehova. Kama vile “imani bila kuwa na kazi imekufa,” ndivyo pia ilivyo ubatili kudai kwamba tunamtumaini Mungu tusipoonyesha hivyo kwa matendo yetu. (Yakobo 2:26) Katika makala iliyotangulia, tulijifunza kwamba tunaweza kuonyesha tunamtumaini Yehova tunaposali kwake, tunapotafuta mwongozo kutoka katika Neno lake, na kutegemea mwongozo wa tengenezo lake. Hebu sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kuchukua hatua hizo tatu wakati wa taabu.

      Unapopoteza Kazi au Mapato Yanapokuwa Kidogo

      3. Watumishi wa Yehova wanaoishi katika ‘nyakati hizi za hatari’ wanakabili hali gani ngumu za kiuchumi, na tunajuaje kwamba Mungu yuko tayari kutusaidia?

      3 Katika ‘nyakati hizi za hatari,’ sisi Wakristo hukabiliana na hali ngumu za kiuchumi kama watu wengine. (2 Timotheo 3:1) Kwa hiyo, huenda kwa ghafula tukajikuta tumepoteza kazi. Au huenda tukalazimika kufanya kazi kwa saa nyingi na kupata mshahara kidogo. Chini ya hali hizo, huenda tukaona ni vigumu ‘kuwaandalia kitu wale walio wetu wenyewe.’ (1 Timotheo 5:8) Je, Mungu Aliye Juu Zaidi yuko tayari kutusaidia nyakati hizo? Ndiyo kabisa! Kwa kweli, Yehova hatukingi na magumu yote ya maisha ya mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, tukimtumaini, maneno ya Zaburi 46:1, BHN, yatatuhusu: “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu.” Lakini tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamtumaini Yehova kikamili kunapokuwa na taabu za kiuchumi?

      4. Tunapokabili matatizo ya kiuchumi, tunaweza kusali juu ya nini, na Yehova huonaje sala hizo?

      4 Njia moja ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova, ni kusali kwake. Lakini tunaweza kusali juu ya nini? Tunapokabili matatizo ya kiuchumi, huenda tukahitaji hekima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Bila shaka tunapaswa kusali tupewe hekima! Neno la Yehova linatuhakikishia hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yakobo 1:5) Naam, mwombe Yehova akupe hekima—uwezo wa kutumia vizuri ujuzi, uelewevu, na utambuzi—ili ufanye maamuzi ya busara na machaguo mazuri. Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anatuhakikishia kwamba atasikiliza sala hizo. Yeye yuko tayari daima kunyoosha mapito ya wale wanaomtumaini kwa moyo wao wote.—Zaburi 65:2; Mithali 3:5, 6.

      5, 6. (a) Kwa nini tunaweza kutegemea Neno la Mungu ili litusaidie kukabiliana na hali ngumu za kiuchumi? (b) Tunaweza kufanya nini ili kupunguza wasiwasi tunapopoteza kazi?

      5 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova ni kutegemea mwongozo kutoka katika Neno lake. Vikumbusho vyake vyenye hekima vinavyopatikana katika Biblia vimekuwa “vyenye kutegemeka sana.” (Zaburi 93:5, NW) Ingawa kitabu hicho kilichoongozwa kwa roho ya Mungu kilikamilishwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, kina mashauri yenye kutegemeka na ufahamu wenye kina unaoweza kutusaidia kukabiliana vizuri na hali ngumu za kiuchumi. Fikiria mifano fulani inayoonyesha hekima ya Biblia.

      6 Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi zamani: “Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.” (Mhubiri 5:12) Wakati na pesa zinahitajika ili kurekebisha, kusafisha, kudumisha, na kulinda vitu vyetu vya kimwili. Hivyo tukipoteza kazi, huenda tukatumia nafasi hiyo kuchunguza tena mtindo wetu wa maisha na kujaribu kuamua vitu tunavyohitaji na vitu tusivyohitaji. Ili kupunguza wasiwasi, lingekuwa jambo la hekima kufanya mabadiliko fulani. Kwa mfano, je, inawezekana kufanya maisha yetu yawe sahili, labda kuhamia nyumba ndogo zaidi au kuondoa vitu vya kimwili tusivyohitaji?—Mathayo 6:22.

      7, 8. (a) Yesu alionyeshaje kwamba anajua wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kuhangaikia vitu vya kimwili kupita kiasi? (Ona pia kielezi-chini.) (b) Yesu alitoa shauri gani lenye hekima kuhusu jinsi ya kuepuka kuwa na mahangaiko isivyofaa?

      7 Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alishauri hivi: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa.”b (Mathayo 6:25) Yesu alijua kwamba kwa kawaida wanadamu wasio wakamilifu huhangaika kupata mahitaji ya lazima. Lakini tunawezaje ‘kukoma kuhangaikia’ vitu hivyo? Yesu alisema: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme.” Hata tuwe tunakabili matatizo gani, tunapaswa kuendelea kutanguliza ibada ya Yehova maishani. Tukifanya hivyo, Baba yetu wa mbinguni ‘atatuongezea’ mahitaji yetu yote ya kila siku. Kwa njia fulani, atatuandalia tunayohitaji.—Mathayo 6:33.

      8 Yesu alitoa shauri hili lingine: “Msihangaike kamwe juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe.” (Mathayo 6:34) Si jambo la hekima kuhangaikia isivyofaa mambo ambayo huenda yakatokea kesho. Msomi mmoja alisema hivi: “Wakati ujao si mbaya sana kama tunavyohofia.” Kutii kwa unyenyekevu shauri la Biblia kuhusu kuzingatia mambo muhimu na kutatua matatizo wakati yanapotokea kutatusaidia kuepuka kuwa na mahangaiko isivyofaa.—1 Petro 5:6, 7.

      9. Tunapokabili taabu za kiuchumi, tunaweza kupata msaada gani katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”?

      9 Tunapokabili taabu za kiuchumi, tunaweza pia kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kutafuta msaada kutoka katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Mara kwa mara, gazeti la Amkeni! limechapisha makala zilizo na mashauri na madokezo mazuri kuhusu jinsi ya kushughulika na magumu ya kiuchumi. Makala “Ukipoteza Kazi—Suluhisho Ni Nini?” katika toleo la Juni 8, 1992, iliorodhesha miongozo minane ambayo imewasaidia watu wengi kudumisha usawaziko wa kifedha na kihisia-moyo wanapopoteza kazi.c Bila shaka, pamoja na miongozo hiyo, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu umuhimu wa pesa. Jambo hilo lilizungumziwa katika makala “Kitu Kingine cha Maana Sana Kuliko Pesa” iliyochapishwa katika toleo hilohilo.—Mhubiri 7:12.

      Tunapotaabishwa na Matatizo ya Afya

      10. Mfano wa Mfalme Daudi unaonyeshaje kwamba ni jambo la busara kumtumaini Yehova tunapougua ugonjwa mbaya?

      10 Je, ni jambo la busara kumtumaini Yehova tunapougua ugonjwa mbaya? Ndiyo kabisa! Yehova huwahurumia wagonjwa miongoni mwa watu wake. Zaidi ya hayo, yeye yuko tayari kuwasaidia. Kwa mfano, mfikirie Mfalme Daudi. Huenda yeye mwenyewe alikuwa mgonjwa mahututi alipoandika jinsi Mungu anavyomtendea mwadilifu anayeugua. Alisema: “BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia.” (Zaburi 41:1, 3, 7, 8) Mfalme Daudi aliendelea kumtumaini Mungu kabisa na hatimaye mfalme huyo akapona ugonjwa wake. Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunamtumaini Mungu tunapotaabishwa na matatizo ya afya?

      11. Tunapougua ugonjwa, tunaweza kumwomba nini Baba yetu wa mbinguni?

      11 Tunapougua ugonjwa, njia moja ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova ni kwa kumsihi katika sala atusaidie kuvumilia. Tunaweza kumwomba atusaidie tutumie “hekima kamili” ili tuweze kutafuta matibabu kulingana na hali zetu. (Mithali 3:21) Tunaweza pia kumwomba atusaidie kuwa na uvumilivu na subira ili tukabiliane na ugonjwa huo. Zaidi ya yote, tungependa kumwomba Yehova atutegemeze na kutupa nguvu za kuendelea kuwa waaminifu kwake bila kupoteza usawaziko hata jambo gani litokee. (Wafilipi 4:13) Kudumisha uaminifu wetu kwa Mungu ni muhimu zaidi hata kuliko kulinda uhai wetu wa sasa. Tukiendelea kuwa waaminifu, Mthawabishaji Mkuu atatupa afya na uhai mkamilifu milele.—Waebrania 11:6.

      12. Ni kanuni gani za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima kuhusiana na matibabu?

      12 Kumtumaini Yehova pia hutuchochea tutegemee mwongozo kutoka katika Neno lake Biblia. Kanuni zinazopatikana katika Maandiko zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima kuhusu matibabu. Kwa mfano, tukijua kwamba Biblia inashutumu “zoea la uwasiliani-roho,” tutaepuka njia yoyote ya kupima magonjwa au matibabu yanayohusisha uwasiliani-roho. (Wagalatia 5:19-21; Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Mfano mwingine wa hekima ya Biblia yenye kutegemeka ni huu: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15) Hivyo, tunapofikiria matibabu fulani, litakuwa jambo la hekima kutafuta habari zenye kutegemeka badala ya ‘kuamini kila neno.’ ‘Utimamu huo wa akili’ unaweza kutusaidia kufikiria kwa makini machaguo yetu na kufanya uamuzi unaotegemea habari kamili.—Tito 2:12.

      13, 14. (a) Ni makala gani zenye kuarifu kuhusu afya ambazo zimechapishwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.) (b) Ni shauri gani kuhusu jinsi ya kushughulika na magonjwa yanayodumu lililotolewa katika Amkeni! la Januari 22, 2001?

      13 Tunaweza pia kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kuchunguza vichapo vya mtumwa mwaminifu. Mara kwa mara, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamechapisha makala zenye kuwaarifu wasomaji kuhusu matatizo hususa ya afya na magonjwa.d Nyakati nyingine, magazeti hayo yamechapisha makala za watu ambao wamekabiliana kwa mafanikio na magonjwa na ulemavu mbalimbali. Zaidi ya hayo, makala fulani zimetoa madokezo ya Kimaandiko na vilevile mashauri kuhusu jinsi ya kuishi na matatizo ya kiafya yanayodumu.

      14 Kwa mfano, gazeti la Amkeni! la Januari 22, 2001, lilichapisha mfululizo wa makala zenye kichwa “Faraja kwa Wagonjwa.” Makala hizo zilitaja kanuni nzuri za Biblia na pia habari kutoka kwa watu waliohojiwa ambao wana ujuzi kuhusu magonjwa yenye kudhoofisha mwili ambayo wameugua kwa miaka mingi. Makala “Kuishi kwa Mafanikio na Ugonjwa Wako—Jinsi Gani?” ilitoa shauri linalofuata: Jifunze mengi kadiri uwezavyo kuhusu ugonjwa wako. (Mithali 24:5) Weka miradi unayoweza kutimiza, kutia ndani miradi ya kuwasaidia wengine, lakini kumbuka kwamba huenda usiweze kutimiza miradi ambayo wengine wanatimiza. (Matendo 20:35; Wagalatia 6:4) Epuka kujitenga na wengine. (Mithali 18:1) Wafanye wengine wafurahie kukutembelea. (Mithali 17:22) Zaidi ya yote, dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kutaniko. (Nahumu 1:7; Waroma 1:11, 12) Je, hatushukuru kwa mwongozo wenye kutegemeka ambao Yehova hutupa kupitia tengenezo lake?

      Udhaifu wa Kimwili Unapoendelea kwa Muda Mrefu

      15. Mtume Paulo alifanikiwaje kupambana na udhaifu wa mwili wenye dhambi, nasi tunaweza kuwa na uhakika gani?

      15 Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema.” (Waroma 7:18) Paulo alijionea mwenyewe jinsi ilivyo vigumu kupambana na tamaa na udhaifu wa mwili wenye dhambi. Hata hivyo, Paulo pia alikuwa na uhakika kwamba anaweza kushinda. (1 Wakorintho 9:26, 27) Jinsi gani? Kwa kumtumaini Yehova kabisa. Ndiyo sababu Paulo alisema: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki? Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:24, 25) Namna gani sisi? Sisi pia tunapigana vita na udhaifu wa kimwili. Tunapoendelea kupambana na udhaifu huo, ni rahisi kupoteza tumaini, na kusadiki kwamba hatuwezi kufanikiwa kamwe. Lakini Yehova atatusaidia ikiwa sisi, kama Paulo, tutamtegemea Yeye bila kutegemea nguvu zetu wenyewe.

      16. Udhaifu wa kimwili unapoendelea kwa muda mrefu, tunapaswa kusali juu ya nini, na tunapaswa kufanya nini ikiwa tutarudia tena udhaifu huo?

      16 Udhaifu wa kimwili unapoendelea kwa muda mrefu, tunaweza kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kumwomba kwa bidii. Tunahitaji kumwomba Yehova msaada wa roho yake takatifu. (Luka 11:9-13) Tunaweza kumwomba hasa atupe sifa ya kujidhibiti, ambayo ni moja ya matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Tutafanya nini tukirudia tena udhaifu huo? Hatupaswi kuvunjika moyo hata kidogo. Na tusichoke kamwe kusali kwa unyenyekevu kwa Mungu wetu mwenye rehema, huku tukimwomba msamaha na msaada. Yehova hatakataa wala kutupilia mbali kamwe moyo “uliovunjika na kupondeka” kwa sababu ya dhamiri yenye hatia. (Zaburi 51:17) Tukimwomba Yehova tukiwa na moyo mnyofu na wenye toba, atatusaidia tupigane na vishawishi.—Wafilipi 4:6, 7.

      17. (a) Kwa nini inafaa kutafakari maoni ya Yehova kuhusu udhaifu fulani ambao huenda tunapambana nao? (b) Tunaweza kukariri maandiko gani ikiwa tunajaribu kudhibiti hasira ya ghafula? tunashindwa kulinda ulimi wetu? tuna mwelekeo wa kujihusisha katika vitumbuizo visivyofaa?

      17 Tunaweza kuonyesha pia kwamba tunamtumaini Yehova kwa kuchunguza Neno lake ili kupata msaada. Tukitumia konkodansi ya Biblia au kitabu Watch Tower Publications Index, tunaweza kutafuta jibu kwa swali hili, ‘Yehova anaonaje udhaifu ambao ninapambana nao?’ Kutafakari maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo kunaweza kuimarisha tamaa yetu ya kutaka kumpendeza. Kwa hiyo, tunaweza kuanza kuwa na maoni kama yake, na kuchukia mambo anayochukia. (Zaburi 97:10) Wengine wameona kwamba inafaa kukariri maandiko ya Biblia yanayohusu udhaifu hususa wanaopambana nao. Je, tunajaribu kudhibiti hasira yetu ya ghafula? Ikiwa ndivyo, basi tunaweza kukariri maandiko kama vile Mithali 14:17 na Waefeso 4:31. Je, tunashindwa kulinda ulimi wetu? Tunaweza kukariri maandiko kama vile Mithali 12:18 na Waefeso 4:29. Je, tuna mwelekeo wa kujihusisha katika vitumbuizo visivyofaa? Tunaweza kujaribu kukumbuka mistari kama vile Waefeso 5:3 na Wakolosai 3:5.

      18. Kwa nini hatupaswi kuona haya kuwaomba wazee watusaidie kushinda udhaifu wetu?

      18 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunamtegemea Yehova ni kutafuta msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko ambao wamewekwa rasmi na roho. (Matendo 20:28) Kwa kweli, wazee hao ni “zawadi zikiwa wanadamu” kutoka kwa Yehova kupitia Kristo ili kuwalinda na kuwatunza kondoo zake. (Waefeso 4:7, 8, 11-14) Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kuomba msaada ili kukabiliana na udhaifu fulani. Huenda tukaona haya, tukiogopa kwamba wazee watatudharau. Lakini bila shaka wanaume hawa waliokomaa kiroho watatuheshimu kwa sababu tulikuwa na ujasiri wa kuomba msaada. Zaidi ya hayo, wazee hujitahidi kuonyesha sifa za Yehova mwenyewe wanaposhughulika na kundi. Huenda mashauri na maagizo yao yanayofaa na yenye kufariji ambayo yanatoka kwenye Neno la Mungu, ndiyo tunayohitaji ili kuimarisha azimio letu la kushinda udhaifu wetu.—Yakobo 5:14-16.

      19. (a) Shetani anajaribu kutumiaje ubatili wa maisha katika mfumo huu? (b) Tumaini linahusisha nini, na tunapaswa kuazimia kabisa kufanya nini?

      19 Usisahau kamwe kwamba Shetani anajua wakati wake ni mfupi. (Ufunuo 12:12) Yeye anataka kutumia ubatili wa maisha katika ulimwengu huu ili kutuvunja moyo na kutukatisha tamaa. Basi na tuyatumaini kabisa maneno haya kwenye Waroma 8:35-39: “Nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je, ni dhiki au taabu au mnyanyaso au njaa au uchi au hatari au upanga? . . . Kinyume chake, katika mambo yote haya tunatokea tukiwa wenye kushinda kabisa kupitia yeye aliyetupenda. Kwa maana nasadiki kwamba wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Mistari hiyo inatutia moyo kama nini tumtumaini Yehova! Hata hivyo, tumaini la aina hiyo si hisia tu. Bali ni tumaini linalohusisha maamuzi tunayofanya kila siku ambayo yanategemea habari kamili. Basi na tuazimie kabisa kumtumaini Yehova kikamili nyakati za taabu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika barua yake ya Novemba 20, 1861, aliyoandikia kiwanda cha kutengeneza pesa cha Marekani, Waziri wa Fedha, Salmon P. Chase alisema: “Hakuna taifa linaloweza kuwa na nguvu bila kutegemea nguvu za Mungu, au kuwa salama pasipo ulinzi Wake. Tunapaswa kuonyesha kwenye sarafu za taifa letu kwamba raia zetu wanamtumaini Mungu.” Kwa hiyo, ule wito “In God We Trust” ulionekana mara ya kwanza katika sarafu ya Marekani mwaka wa 1864.

      b Hangaiko linalotajwa hapa linasemekana kuwa ni “hofu inayosababisha wasiwasi ambao huondoa furaha yote maishani.” Tafsiri fulani zinasema “msisumbuke” au “msiwe na wasiwasi.” Lakini tafsiri hizo zinadokeza kwamba hatupaswi kuanza kuwa na wasiwasi au kusumbuka. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema: “Njeo ya kitenzi cha Kigiriki iko katika hali ya kuamrisha sasa, ikionyesha amri ya kuacha kufanya jambo fulani ambalo tayari linaendelea.”

      c Miongozo hiyo minane ni: (1) Usiwe na hofu kuu; (2) fikiria kwa mwelekeo mzuri; (3) fungulia akili yako aina mpya za kazi; (4) ishi kwa mapato yako mwenyewe—si ya mwingine; (5) uwe mwangalifu na mkopo; (6) endeleza umoja katika familia; (7) endelea kujistahi; na (8) panga bajeti.

      d Magazeti hayo yanayozungumzia Biblia hayapendekezi matibabu fulani hususa, kwa kuwa yanatambua kwamba huo ni uamuzi wa mtu binafsi. Badala yake, makala zinazozungumzia magonjwa hususa zimekusudiwa kuwaarifu wasomaji habari zinazojulikana kwa sasa kuhusu magonjwa hayo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki