Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ kwa sababu gani Daudi, hali akijua alimtia hatarini Ahimeleki kuhani mkuu na jambo hilo likaongoza kwenye kifo cha kuhani huyo, kama vile Daudi alivyoungama katika 1 Samweli 22:22?
Kwa kweli, andiko la 1 Samweli 22:22 halionyeshi kwamba Daudi alijua mapema kwamba mwendo wake ungeongoza kwenye kifo cha Ahimeleki. Mstari huo unasema hivi: “Daudi akamwambia Abiathari [mwana wa Ahimeleki] Siku ile alipokuwako Doegi, Mwedomi, nalijua yakini ya kuwa [yeye Doegi] atamwambia Sauli; mimi nimewapatia watu wote wa jamaa ya baba yako [Ahimeleki] kifo.”
Alipokuwa akimkimbia Mfalme Sauli mwenye hasira kali, Daudi alienda Nobu ambako Ahimeleki kuhani mkuu alikuwa. Labda kwa sababu ya kuhangaika ya kwamba kuhani mkuu hangehisi akiwa na wajibu wa kumweleza mfalme mahali ambako Daudi alikuwa, Daudi hakumfunulia sababu hasa iliyomfanya awe nje ya Yerusalemu. Hata hivyo kuwapo kwake katika Nobu kulionekana. Mwedomi jina lake Doegi alimwona Daudi na baadaye akamweleza jambo hilo Sauli mwenye hasira.
Ingawa hivyo, hakuna lo lote katika masimulizi hayo linalothibitisha kwamba Daudi alijua mapema juu ya kuwapo kwa Doegi. Doegi ‘siku ile alikuwa amezuiwa hapo mbele za Yehova.’ (1 Samweli 21:7) Inaelekea kwamba Daudi alishangaa, hata akashtuka, kwamba Doegi asiyefuata kanuni alimwona akiwa pamoja na Ahimeleki. Hata hivyo, ilipokwisha fanywa, ikawa imefanya. Daudi hangeweza kubadili jambo hilo wala kuyazuia matokeo mabaya sana ambayo hasira kali ya Sauli ilileta juu ya huyo kuhani mkuu na hesabu kubwa ya makuhani wengine, vilevile wanawake, watoto, na wanyama katika Nobu.—1 Samweli 22:9-19.
Akiwa na hilo akilini, angalia tena maneno yenye masikitiko ambayo Daudi alimwambia Abiathari, aliyekuwa ameyaokoka mauaji hayo: “Siku ile alipokuwako Doegi, Mwedomi, nalijua yakini . . .” Tunaweza kuelewa kwamba jambo alilomaanisha Daudi ni kwamba, ‘Mimi nilijua siku hiyo, mara tu nilipoona kwamba Doegi alikuwa ameniona nikiwa pamoja na Ahimeleki . . . ’ Lakini ilikuwa ni kuchelewa mno. Doegi alikuwa pale bila kutazamiwa naye akaona Daudi akiwa pamoja na kuhani mkuu. Kwa hiyo Daudi alikata shauri papo hapo kwamba Doegi angemweleza Sauli jambo hili. Ndiyo sababu Daudi alikiri baadaye mbele ya Abiathari kwamba alihisi kwa kiasi fulani akiwa na hatia, hata ikiwa Daudi alikuwa ameshiriki tu kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika mauaji yaliyofuata. Yeye alihimiza Abiathari abaki pamoja naye, kwa maana Daudi alitumaini kupata mwongozo na ulinzi wa Yehova.—1 Samweli 22:22,23.
■ Je! inafaa ndugu wawili au watatu washiriki kuzamisha mtu wakati wa ubatizo wa Kikristo?
Kwa kawaida ni mhudumu mmoja tu wa kiume anayehitajiwa kubatiza mtu.
Ingawa Biblia haitoi mpangilio wa kanuni za kufuata kuhusu ubatizo wa Kikristo, tunaweza kujifunza kutokana na kumbukumbu la Biblia. Hasa ubatizo wa Yesu katika maji una mafundisho mengi.
Biblia inaripoti hivi: “Ndipo Yesu akatoka Galilaya kuja Yordani kwa Yohana [Mbatizaji]ili abatizwe na yeye.” (Mathayo 3:13, NW) Angalia kwamba hapo panasema “na yeye,” si na wao. Masimulizi ya Injili hayatoi dalili ya kuonyesha kwamba mtu ye yote alishirikiana na Yohana katika kubatiza Yesu. Kwa kweli, inaonekana wazi kwamba hakukuwa na watazamaji wo wote kwenye ubatizo huo, kwa maana Yohana peke yake ndiye pale mwanzoni-mwanzoni aliyemtambulisha Yesu kuwa “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:33, 34) Basi, ubatizo wa Yesu unaweka kielelezo cha kuzamishwa kabisa katika maji, lakini pia unadokeza kwamba mtumishi mmoja wa kiume wa Mungu ndiye anayepaswa kufanya ubatizo huo.
Huenda ikawa kulikuwa na shahidi mmoja au zaidi wakati Filipo alipobatiza towashi Mwethiopia “mahali penye maji [mengi],” lakini Filipo alikuwa peke yake katika kuufanya ubatizo wenyewe. (Matendo 8:36-39) Wala maandishi ya Biblia juu ya mabatizo mengine hayaonyeshi kwamba ndugu wawili au watatu walishiriki katika kumshusha mtu chini ya maji kisha kumwinua ndugu au dada huyo mpya atoke ndani ya maji hayo. Ingawa hivyo, inaonekana katika visa vingi walikuwako watazamaji au mashahidi wenye kuona mabatizo hayo.
Bila shaka, katika muda wa miaka iliyopita zimekuwako hali fulani za pekee ambazo zimehitaji mambo yarekebishwe yalingane na hali hizo wakati wa kufanya mabatizo fulani. Kwa mfano, wakati mahali pa pekee penye maji mengi panapoweza kupatikana ni kijito chenye maji yanayopita kasi na kinachoweza kuwa hatari, kuheshimu usalama kunaweza kupendekeza kwamba ndugu wawili wafanye kazi pamoja. Au hali ya kimwili ya mtaka-ubatizo, kama vile kupooza mwili au kuwa na udhaifu wa kimwili unaopita kiasi, inaweza kutaka kwamba ndugu zaidi ya mmoja wafanye ubatizo ule. Ingawa hivyo, hivyo ni visa visivyo vya kawaida vinavyopaswa kushughulikiwa kulingana na inavyoonekana ni hekima kufanya. Kawaida kati ya Mashahidi wa Yehova ni mwanamume mmoja tu kumzamisha mtaka-ubatizo.