Kueneza Kifo Kimakusudi
KABLA UKIMWI haujaua mihanga wao, huwakabidhi daraka la kutetemesha: nguvu ya kuleta uhai au kifo juu ya wengine. Watu wengi wenye UKIMWI hutenda kwa kujali daraka lao, wakijinyima kitendo chochote ambacho kingeweza kuathiri mwingine. Lakini wachache fulani walio hatari huamua tofauti.
Daktari wa akili katika Washington, D.C., aliandika juu ya kielelezo cha kuogopesha—mmoja wa wagonjwa wa daktari huyo wa kike: “Mimi nahofu kwamba mtu fulani mwenye kufanya ngono na jinsia zote mbili aliye mhanga mwenye kuhangaishwa sana na UKIMWI anajaribu kuambukiza watu wengine ugonjwa wake. Yeye ajua ungeweza kuwaua.” Mgonjwa huyo alimwambia daktari huyo hivi: “Kwanza nilipojua nina UKIMWI niliamua kutofanya ngono na yeyote, halafu nikakasirika mara na kusema: Acheni tuushinde ulimwengu.” Alimaanisha nini?
Daktari huyo wa akili aeleza hivi: “Aliniambia kwamba nyakati fulani alipokasirikia mtu fulani, sauti fulani ya ndani ilimwambia, ‘Acheni tumnase jamaa huyu’ na hapo mwanamume huyo angejaribu kufanya ngono na mtu huyo. Pia mwanamume huyo alisema kwamba alikuwa akiishi na mwanamume mwenye kufanya ngono na jinsia zote mbili ambaye aliishi ovyo na wanawake.” Daktari huyo wa akili alijaribu kusadikisha maofisa wamtie kizuizini mwanamume huyo hatari lakini wapi. “Nilipomwona mara ya mwisho,” aandika daktari huyo wa kike, “mwenendo wake ulikuwa haujabadilika, nami sina sababu ya kutia shaka kwamba kuna badiliko lolote leo.”
Je! ni kisa cha pekee? Kwa kuhuzunisha, sivyo. Mwanamume mmoja alibandikwa jina na Vitovu vya Kudhibiti Magonjwa kwa kuitwa Mgonjwa Namba Sifuri kwa sababu ya ushiriki wake mkuu katika mweneo wa mapema wa UKIMWI katika United States. Hata baada ya yeye kujua kwamba alikuwa akihatarisha uhai wa wengine, aliendelea kufanya ugoni-jinsia-moja pamoja na wenzi wapatao 250 kwa mwaka. Wanawake wamelalamika juu ya wenzi wa ndoa walioficha siri ya kufanya ngono na jinsia zote mbili. Watumizi wa dawa za kulevya huendelea kushirikiana sindano zao zilizotumika na kuchafuka na kwa hiyo wamekuwa ndicho kikundi kikubwa zaidi cha mihanga wa UKIMWI katika nchi kadhaa.
Ijapokuwa yote haya ni yenye kufadhaisha, hayawashangazi wanafunzi wa Biblia. Kitabu hicho cha kale kilitabiri hapo kale kwamba watu wa kizazi hiki chenye mfadhaiko wangekuwa “wenye kujipenda . . . wasiowapenda wa kwao.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa uhakika wakati huo umekuja. Wale wanaopuuza sheria za Mungu juu ya maadili wamemwudhi sikuzote Mtungaji wa sheria hizo, Muumba wetu. Hiyo ndiyo hatari mbaya kabisa ambayo mtu aweza kujasiria maishani. Lakini leo kutotii kule kule huleta hatari ya ziada mara nyingi: kukabidhi uhai wenyewe wa mtu kwa watu wasiothamini chochote isipokuwa raha yao wenyewe.