Kutoka Kwenye Barabara ya Kifo Kuja Kwenye Barabara ya Uhai
KWA miaka mingi maisha yangu yalitiwa makovu na uzoelevu wa dawa za kulevya. Nilianza na dawa zisizo kali sana nikaishia kuzitumia zilizo kali, kama vile LSD. Dawa za kulevya zikaja kufananisha ukombozi kutoka namna zote za matatizo ya kibinafsi na kijamii. La kuhuzunisha ni kwamba, niliwatia moyo vijana wengine waandamane nami katika barabara hiyo ya kifo.
Kwa kuwa nilijulikana kuwa mchuuzi wa dawa za kulevya, macho ya polisi yalikuwa kwangu. Ni lazima nikubali kwamba niliogopa, kwa maana nilijua kwamba nikikamatwa ningefungwa gerezani miaka mingi. Ingawa niliishi katika mtaabiko mkubwa wa fikira, hiyo haikutosha kunifanya nibadili njia zangu.
Wazazi wangu walijaribu kunisaidia kwa kunipeleka makao ya wagonjwa wa akili ili nikatibiwe. Ilitumainiwa kwamba dawa na matibabu ambayo ningepokea huko zingetatua tatizo langu, lakini mara tu nilipotoka huko, wazazi wangu waling’amua kwamba wala hata matibabu hayangeweza kunibadili mimi. Walijaribu kunisaidia kwa kunifanya niongee na padri. Hata hiyo ikawa kazi bure. Mimi nilivuta bangi na kunywa pombe mbele yake, kana kwamba yeye hakuwa pale. Sikutaka kubadilika kamwe kamwe!
Mchumba wangu, Oriana, alipinga sana njia yangu ya maisha, nami sikutaka msichana huyo aniache. Kijuu-juu, hicho kilionekana kama kichocheo chema cha kunifanya nibadilike. Lakini, badala ya kufanya hivyo, niliendelea na zoea langu la kutumia dawa za kulevya kwa siri. Nilimfanya Oriana aamini nilikuwa mgonjwa. Muda si muda nikawa binadamu hohehahe. Niliendelea kujiahidi mwenyewe kwamba ningeacha, kwamba ningeweza kufaulu, lakini wapi. Nilikuwa nikizidi tu kusonga mbele katika barabara ya kifo.
Kwa kuwa nilitaka kumwoa Oriana mara tu iwezekanapo, tulipashana habari na fundi wa kupamba nyumba ndani ili atufanyie kazi katika kijumba chetu. Mke wake alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na mke huyo aliongea nasi kuhusu imani yake. Kwanza maongezi tuliyokuwa nayo yalimvutia Oriana kwa kina kirefu kuliko vile yalivyonivuta mimi, lakini yalipoendelea, mimi niling’amua kwamba Mashahidi wa Yehova huamini kwa uthabiti kwamba muda si muda Mungu atafanya dunia hii iwe paradiso na kwamba watu wataishi hapa hapa katika amani milele.
Nilitaka kuchunguza mwenyewe nione kama ilikuwa kweli kwamba “hata sasa Mashahidi wa Yehova huonyeshana upendo na staha mmoja na mwenzake,” kama alivyosema bibi huyo. Kwa hiyo Oriana na mimi tukaenda kwenye Jumba la Ufalme. Mimi niliona aibu kwa sababu ya kuwa na nywele ndefu na nguo ovyo-ovyo, lakini ukaribishi ambao Mashahidi walitutolea sisi ulinifanya nihisi nikiwa nimestareheka mara hiyo. Nilihisi kwamba ningeweza kuwaamini wao. Ilikuwa wazi kwamba tayari wao wamekwisha kuwa wakipendana na kuonyeshana staha kwa moyo mweupe.
Tangu siku hiyo, nilianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, nami nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilinyoa nywele zangu na kubadili njia yangu ya kuvaa, na kwa jitihada kubwa, nikaweza kuacha kabisa kuvuta sigareti na kutumia dawa za kulevya. (2 Wakorintho 7:1) Hata hivyo, lilikuwamo tatizo jingine zito maishani mwangu. Nilikuwa nimekuwa mzoelevu wa kileo bila kung’amua hivyo. Nilipokunywa pombe, niliingia matatani. Nilibishana na watu na kuona wivu sana kuhusu Oriana. Nilitumbukia katika hali ya kina kirefu ya kukosa furaha. (Mithali 23:29-35) Nikafanya jitihada ya kuvunja zoea hilo, na kwa msaada wa Yehova, nguvu ya sala, na msaada wa ndugu Wakristo, niliweza kuung’oa mzizi wa zoea baya hili kutoka maishani mwangu.
Mke wangu na mimi tulibatizwa siku ya Agosti 23, 1974. Nautolea ukweli shukrani, maisha zetu sasa zina maana. Kwa maana nilikuwa nimerudiwa na uhakika wa kujiamini, nilistahiwa kazini. Sote wawili, mke wangu na mimi, tulichuma donge kubwa la pesa, lakini ndipo tukang’amua kwamba tulibaki na wakati mchache kwa ajili ya utumishi mtakatifu. Ikiwa tulitaka kuona shangwe ya kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova, tungelazimika kufanya mabadiliko katika maisha zetu. Ama sivyo, ilikuwako hatari ya kwamba upendo wetu wa kwanza kwa ajili ya ukweli ungepoa. Kwa hiyo katika 1979 tukaanza kupainia, tukijitoa kwa ukamili zaidi tuwe kwenye kazi ya kuhubiri.
Kwa nini mimi nilifanya uamuzi huu? Ala, kwani mimi ningekuwa wapi leo bila nuru ya ukweli? Wale waliokuwa pamoja nami katika barabara ya kifo ni wazoelevu wa kileo sasa au hawana tena jamaa au wamo gerezani—au wamekufa. Na hata hivyo, ujumbe wa Biblia ndio ulionipa uhuru. Kupata matibabu na kuwa na uthabiti wa nia hakukutosha kamwe. Kichocheo imara kilihitajiwa. Kutafuta kusitawisha urafiki wa kweli pamoja na Yehova, Muumba, ndiko kulikoandaa kichocheo hicho. Sasa, tamaa yangu ya moyo mweupe ni kwamba nifanye yote niwezayo kuwasaidia wale walio watumwa wa zoea la kutumia dawa za kulevya, na pia wale wanaoteseka au wanaotafuta njia ya kutoka katika matatizo yao. Kwa kushiriki kwa utendaji mwingi katika huduma ya Kikristo, mke wangu na mimi tumekuwa tukifanya hivyo hasa. Tumekuwa na pendeleo la kusaidia watu wengi waifuate barabara ya uhai. Miongoni mwa hawa wamo watu watatu ambao mimi binafsi nilikuwa nimewaanzisha kutumia dawa za kulevya. Kwa sasa mimi natumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko kaskazini mwa Italia.
Ni kweli kwamba: Utumizi mbaya wa dawa za kulevya ni kama barabara ambayo muda fulani itakuongoza tu kwenye kifo au angalau kwenye maisha matupu yasiyo na wakati ujao. Mimi nashindwa kupata maneno ya kueleza shukrani zangu kwa Yehova Mungu! Yeye alinionyesha mimi njia ya kutoka katika giza nilimokuwa nikiishi na kunionyesha wazi barabara ya uhai, yenye kujaa nuru, ambayo yaongoza kwenye wakati ujao wa milele.—Kama ilivyosimuliwa na Ruggero Polotti.