Sura ya 20
Ni Maisha ya Namna Gani Unayotaka?
KAMA mtu angekuuliza, ‘’Nawezaje kupata furaha leo?’ ungempa jibu gani? Unaweza kumwambia hivi bila shaka lo lote: ‘Ili upate maisha kamili, yenye furaha na ya kudumu, fanya mambo kwa njia ya Mungu!’
2 Katika sura zilizotangulia tumezungumza kwamba Muumba yuko kweli kweli, kwamba anaitumia Biblia kutupa habari na mwongozo tunaohitaji sote, na kwamba kufuata Neno lake ni jambo lenye mafaa leo. Kuishi tukiwa Wakristo wa kweli kunaweza kutusaidia tushindane na matatizo kama mikazo na upweke. Kuitegemea Biblia ituongoze kunaweza kutulinda na matatizo yenye maumivu yanayosababishwa na ulevi, uasherati, udanganyifu na maovu mengine. (Mithali 4:11-13) Kukubali maoni ya Biblia juu ya fedha kunatuwezesha turidhike zaidi na ‘kushika sana uzima ulio kweli kweli’—1 Timotheo 6:19.
3 Tunapotii anayosema Muumba, maisha yetu yanapata maana na mwelekezo. Tunafahamu sababu gani Mungu ameruhusu uovu na taabu ziwepo. Na tunapouona utimizo wa unabii mbalimbali katika matukio ya siku zetu, tunajua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” wa taratibu (mfumo) mbovu ya mambo ya sasa. (2 Timotheo 3:1-5) Ndiyo kusema kwamba karibuni Mungu ataziondoa kabisa falme zote za kibinadamu pamoja na historia yazo ya ufisadi wa kisiasa na majeshi yanayoendelezwa kwa kulemea watu na mizigo mizito sana ya kodi. (Danieli 2:44; Ufunuo 16:14, 16) Hivyo Mungu ataukomesha mfuatano wa jitihada za kibinadamu za kuitawala dunia kisha awaelekeze wanadamu watakaookoka kwa kuutumia ufalme wake wa kimbingu.—Ufunuo 11:17, 18; 21:1-4.
JE! HIVYO NDIVYO WEWE UNAVYOTAKA?
4 Walio wengi kati yetu wangesema: ‘Ingekuwa vizuri sana kuishi kati ya watu wenye upendo, wenye kumwogopa Mungu katika paradiso.’ (Isaya 11:9) Lakini ili tuishi hivyo ni lazima kupenda kwetu uadilifu na kutamani kujipatanisha na viwango vya Mungu kuwe na nguvu za kutosha ili kutuamulia sasa kielelezo cha maisha yetu. (Mathayo 12:34; 15:19) Je! kweli hivyo ndivyo wewe unavyotaka? Katika habari hii, mwanafunzi Yakobo aliongozwa na Mungu awaandikie Wakristo hivi:
“Je, hamjui kwamba kuwa rafiki wa ulimwengu ni kuwa adui wa Mungu? Ye yote ANAYETAKA kuwa rafiki wa ulimwengu anajifanya adui wa Mungu.”—Yakobo 4:4, HNWW.
5 Yakobo alikazia pia kwamba “dini iliyo safi na isiyo na hitilafu mbele ya Mungu Baba” inahusu ‘mtu kujilinda mwenyewe asichafuliwe na ulimwengu huu.’ (Yakobo 1:27, HNWW) Inatupasa tujitahidi kufanya hivyo. Bila shaka, si vyepesi kukaa bila kugusika kabisa kabisa kwa kuwa Wakristo wanaishi kati ya jeuri na mafamba (ufisadi) ya ulimwengu, mipango yenye uasherati, siasa na utukuzo wa taifa. Hata Mkristo mwenye kujitoa sana huenda akateleza au akafanya makosa asiyotazamia anapojaribu kuepuka asichafuliwe na njia ya ulimwengu. Ndiyo sababu Wakristo wanahitaji wazidi kujikaza wafanye maendeleo. (Wakolosai 3:5-10) Lakini maana ni hii, sisi tunataka nini?
6 Kwa mfano, tuwazie wanaume wawili wanakula chakula cha mchana. Mwanamume mmoja anajitupia doa la mchuzi kwenye tai yake bila kutaka. Yule mwingine anaichukua tai yake mwenyewe na kuichovya kwa makusudi ndani ya ule mchuzi; anataka mambo yawe hivyo. Kati ya hao wawili, sisi tuko kama yupi? Je! tunaonyesha kwa mambo tunayoruhusu yatuvute na kwa yale tunayochagua kufanya kwamba sisi tunataka kuwa rafiki za ulimwengu? au rafiki za Mungu?
7 Urafiki na ulimwengu unaweza kuonyeshwa kwa njia nyingi. Watu wengine wanafungamana sana na jamaa au jirani zao mpaka wanakubaliana au wanashiriki mambo wanayojua Mungu hayapendi, kama vile sherehe za siku zisizo za Kimaandiko, unywaji mwingi mno wa pombe, mizaha (utani) ya matusi au kubagua watu kwa sababu ya rangi ya mwili wao. (1 Petro 4:3, 4; Waefeso 5:3-5; Matendo 10:34, 35) Ikiwa tunataka kumpendeza Mungu, basi tutakuwa na maoni ya kwamba kupata kibali yake ni bora kuliko kupata ya watu wa ukoo wetu.—Luka 14:26, 27; 11:23.
8 Vivyo hivyo, uchaguzi wetu wa tafrija huenda ukaonyesha kama tunataka au hatutaki kuwa rafiki za ulimwengu. Wakristo wa kwanza walikataa kabisa kuhudhuria mapigano yenye ukatili mwingi katika wanja za michezo. Hata walikataa kutazama michezo yenye kukazia uasherati. Namna gani sisi leo? Inatupasa tufikirie tunatanguliza nini kuhusiana na michezo, vipindi vya televisheni, sinema au vitabu vya kusoma. Tukiona tunazoelea sana kutaka mambo anayotukataza Mungu, tunahitaji kutia bidii tubadili mapendezi yetu. Vivuta-macho vya ulimwengu vinaweza kunasa hata vijana ambao wamekulia katika jamaa za Kikristo na vilevile Wakristo ambao wamejifunza Biblia kwa muda mrefu.
9 Shauri hili la kuwa rafiki za Mungu au rafiki za ulimwengu, linahusu uzima au kifo. (1 Yohana 2:15-17) Hatuwezi kuweka mguu mmoja upande huu na mwingine upande ule mwingine. Hakuna mtu aliye penye njia panda anayeweza kutembea katika njia mbili zilizo tofauti.
10 Wakati wa siku za Eliya, Waebrania wengine walivutwa na ibada ya Baali ya mataifa yenye kuwazunguka. Ingawa Waebrania hao walikuwa na uhusiano fulani na yule Mungu wa kweli, Yehova, hawakushikamana kabisa naye. Eliya alisema walikuwa ‘wakisita-sita katikati ya mawazo mawili.’ Ilikuwa lazima waamue kama wangeshikamana au hawangeshikamana na Yehova na njia zake. Uchaguzi uliokuwapo ulikuwa wa uzima au kifo.—1 Wafalme 18:21-40; Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.
11 Hatuwezi kuahirisha uamuzi wa kuonyesha tunachotaka hasa. Katika karne ya kwanza W.K., mtume Petro alihimiza Wakristo ‘wakukaribishe akilini kuwapo kwa siku ya Yehova’ ambayo katika hiyo uovu utaondolewa duniani. Walipaswa waonyeshe kwa “vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa” kwamba wanajua kuna uharaka. Na hiyo ingetia ndani kuutangaza ule ujumbe wa Kikristo kwa shauku. (2 Petro 3:11, 12, NW) Ingawa Wakristo wengine walikuwa na maisha za ndoa zilizo mfano mwema, wengine walichagua kukaa bila kuoa au kuolewa ili waweze “kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine.”—1 Wakorintho 7:29-35.
12 Ikiwa namna ya maisha ambayo Wakristo walitaka kuwa nayo ilikuwa ya maana katika karne ya kwanza, ni ya maana zaidi sana sasa! Tunaweza kuona kwamba ufalme wa Mungu tayari unatawala katika mbingu na kwamba umebaki ‘wakati mfupi tu’ kabla Mungu hajamtumia Kristo kuyaponda mataifa na kumfunga Shetani yule Ibilisi. (Ufunuo 12:12; 19: 11-20:2) Kwa hiyo sasa ndio wakati wa kuamua tunataka kuwa na maisha ya namna gani.
NAMNA YA MAISHA AMBAYO MUNGU ATAWAPA WATU
13 Namna ya maisha tunayochagua sasa ndiyo itakayoamua kama tutaruhusiwa tufurahie namna ya maisha ambayo Mungu atawapa watu katika taratibu mpya inayokuja.
14 Ni jambo jepesi kuzifikiria kwanza baraka nyingi za kimwili zitakazokuwa katika paradiso itakayorudishwa. Katika ile paradiso ya kwanza, Adamu na Hawa walikuwa na chakula cha kutosha chenye kujenga mwili. (Mwanzo 2:9, 16) Hivyo, katika taratibu mpya kutakuwako chakula kizuri chenye kuleta afya, tena kwa wingi.—Zaburi 72:16; 67:6.
15 Adamu na Hawa walikuwa na afya nzuri, kwa maana Mungu aliwaumba wakiwa wakamilifu. Jambo hilo linakazia uhakikisho wa Biblia kwamba katika taratibu mpya magonjwa, maumivu yenye kuletwa na maradhi na machozi ya huzuni yatakuwa mambo ya zamani. (Ufunuo 21:1-4) Wanadamu wataendelea mbele mpaka wafikie ukamilifu wa kimwili.
16 Wanaume na wanawake watapata msisimko mzuri wa kuweza kuzichunguza pande nyingi za elimu na maarifa, kwa maana hawatazuiwa tena na matatizo wala kifo hakitawakomesha wakiwa na umri wa miaka 70. Wewe utaweza kufurahia kuonyesha kwa ukamili majaliwa yako, hata kusitawisha mengine ambayo hukudhani ulikuwa nayo. Upishi, ujenzi wa nyumba, kutengeneza makabati, kupamba-pamba vitu, kulima bustani nzuri, kupiga vyombo vya muziki, kushona mavazi kwa cherehani, kuchunguza pande nyingi sana za maarifa ya namna namna—Huwezi kufikia mwisho wa mambo yenye kudai uwezo wako, na yenye faida, utakayoweza kuyafanya. Wakati mmoja Yehova alisema: “Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:22.
17 Pia, Biblia inasema kwamba katika ile bustani ya Edeni chakula cha wanyama kilikuwa majani, miche na mboga. (Mwanzo 1:30) Kwa hiyo, unaweza kumtazamia Mungu apange mipango ya kuzuia wanyama wasiwe tena wakali sana na wenye hatari; watakaa kwa amani wao kwa wao na pamoja na wanadamu. Watoto hata watu wazima watafurahia kabisa urafiki wao pamoja na wanyama.—Linganisha Isaya 11:6-8; 65:25; Hosea 2:18.
18 Lakini Biblia haianzi kueleza mapana na marefu yote ya baraka za kimwili zitakazoletwa na taratibu mpya. Yehova, Muumba wetu, anajua mahitaji yetu. Biblia inatuhakikishia hivi juu ya Mungu: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.
19 Kwa kufaa Maandiko hayakazii ufanisi wala baraka za kimwili, bali yanakazia mambo ya kiroho na ya kiakili yatakayowezesha furaha iwe katika paradiso itakayorudishwa. Kwa mfano, tunaweza kuzitazamia hali zinazoelezwa kuwa hivi:
“Kazi ya uadilifu wa kweli lazima iwe amani; na utumishi wa uadilifu wa kweli, utulivu na usalama kwa wakati usiojulikana. Na watu wangu lazima wakae katika mahali pa amani penye kudumu na katika makao ya uhakika kamili na katika mahali pa kupumzikia pasiposumbuliwa.”—Isaya 32:17, 18, NW.
20 Tunaweza kufahamu kwamba hata tukiwa na afya njema, makao mazuri na chakula kingi, hatuwezi kuridhika kweli kweli ikiwa tumezungukwa na mapigano, wasiwasi, wivu na hasira kali. (Mithali 15:17; 21:9) Walakini, watu ambao Mungu ataruhusu waishi katika paradiso inayokuja watakuwa ni wale ambao wamejibidiisha sana kuyashinda makosa hayo ya kibinadamu. Wao ndio watakaokuwa jamaa ya Wakristo ya dunia nzima. Watakuwa watu wenye kusitawisha matunda ya roho ya Mungu, kutia na upendo, amani, fadhili na kujiweza. (Wagalatia 5:19-23, NW) Kwa unyofu wa moyo watajitahidi kuwa na nyutu zinazopatana na utu wa Yehova.—Waefeso 4:22-24.
KUISHI ILI KUMPENDEZA NA KUMSIFU YEHOVA
21 Baraka za kimwili na za kiroho zilizoahidiwa zinatupa sababu ya kuitazamia ile taratibu mpya. Walakini, tukiziacha hizo ziwe ndizo sababu za kwanza zinazotufanya tumwabudu Mungu na kuwa na maisha ya Kikristo, kwa kadiri fulani tutakuwa sawa na kizazi cha watu wenye maoni ya mimi kwanza, kinachotanguliza vitu ambavyo wao wanataka na wanavyoweza kuvipata.
22 Badala ya kuwa hivyo, inatupasa tusitawishe tamaa ya kuwa na maisha ya Kikristo—sasa na wakati ujao—kwa sababu Mungu anatutaka tufanye hivyo. Yeye ndiye anayepaswa kuwekwa mbele, si sisi. Yesu alionyesha maoni tunayoyahitaji, akisema: “Nimekuja . . . niyafanye mapenzi yako, Mungu,” na, “Chakula changu ni kufanya anachotaka yule aliyenituma na kuitimiza kazi yake.” (Waebrania 10:7, UV; Yohana 4:34, HNWW) Kuthamini mambo ambayo Mungu ametufanyia kunapasa kutuongoze tumweke yeye mbele.—Warumi 5:8.
23 Kwa kufaa, Biblia haikazii wokovu wetu na baraka tunazoweza kupokea kuwa zenye maana ya kwanza. Bali, inatilia nguvu kutetewa kwa jina la Mungu na kufaa kwetu kumsifu Mungu kwa namna alivyo na yale ambayo amefanya. Daudi aliandika, akasema:
“Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza, nitalihimidi jina lako milele na milele. [Yehova] ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana, wala ukuu wake hautambulikani. Nitaifikiri fahari ya utukufu wa adhama yako, na matendo yako yote ya ajabu.”—Zaburi 145:1, 3, 5.
24 Kumweka Mungu kwanza maishani na kumsifu yeye kwa bidii kuliwafaa Yesu na Daudi. Kunatufaa sana sisi vilevile. Tunapounganisha jambo hilo na ile njia yenye mafaa ya maisha ya Kikristo, hapo tutakuwa tumekwisha kuipata furaha—sasa na mpaka wakati ujao utakaoendelea daima dawamu.
[Mambo ya Kuzungumziwa]
Sababu gani kutenda kwa njia ya Mungu ndiyo njia bora zaidi ya kupata furaha? (1-3)
Kwa sababu gani ni lazima tuamue kama tunataka kuwa rafiki za ulimwengu au za Mungu? (4-6)
Ni kwa njia gani nyingi mtu anaweza kuonyesha kama anataka au hataki urafiki na ulimwengu? (7, 8)
Ni jambo la maana namna gani tuamue kile tunachokitaka hasa? (9-12)
Ni maisha ya namna gani ambayo Mungu atawapa watu katika taratibu mpya? (13-18)
Ni baraka gani zilizo za maana zaidi kutokana na paradiso itakayorudishwa? (19, 20)
Tunaweza kupataje furaha ya kweli? (21-24)
[Picha katika ukurasa wa 189]
Wakati wa kusitawisha majaliwa yako na kuyatumia kwa ukamili