Vitolewaji Vipya Vyatusaidia Sisi Kujizoeza Ujitoaji Kimungu
1 Tukiwa tumekwisha kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya, tunatambua zaidi uhitaji wa kuwa tukijizoeza ujitoaji kimungu ukiwa lengo letu. (1 Tim. 4:7, NW) Tunapotafakari juu ya habari yote iliyotolewa kwenye programu na kujitahidi kuifuata katika maisha yetu ya kila siku, tunasaidiwa kumkaribia zaidi Yehova katika ibada ya kweli.
2 Hata hivyo, kujizoeza kwetu katika ujitoaji kimungu kutaongezwa hasa tunapochanganua hatua kwa hatua utajiri wa habari iliyoandikwa katika vitolewaji vipya tulivyopokea kwenye Ujitoaji Kimungu “Mkusanyiko wa Wilaya.” Je! tayari umekwisha kusoma vitolewaji hivyo vipya?
BROSHUA MPYA
3 Hoja za Kimaandiko zenye kusadikisha zilizotumiwa katika broshua Should You Believe in the Trinity? zinatusaidia si kuthibitisha tu kwamba Utatu ni fundisho bandia linalopasa kukataliwa bali pia kueleza wengine ukweli juu ya Mungu, Mwanaye, na roho takatifu.
4 Msimamo wetu wenye kutegemea Biblia ni kwamba “kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba.” (1 Kor. 8:6) Broshua mpya hiyo itatusaidia kufichua ubandia wa fundisho la kipagani la Utatu tunapowatia moyo wapole wote waache “Mungu aonekane kuwa amini [kweli] na kila mtu mwongo.”—Rum. 3:4.
MAJIBU KWA AJILI YA VIJANA
5 Hatutasahau upesi hotuba ya mkusanyiko ya moja kwa moja na mpango wa pekee wa kutoa kitabu Questions Young People Ask—Answers That Work. Ingawa kilitolewa kwa manufaa ya vijana, wazazi, hasa akina baba, walisihiwa waongoze katika kukitumia kitabu hicho kuwazoeza watoto wao na ‘kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4, NW.
6 Wazazi na watoto pia wapaswa kuzoeleana kabisa na habari hii ya muhimu iliyoandaliwa na tengenezo la Yehova ili kuwasaidia vijana waendelee kujizoeza katika ujitoaji kimungu. Kama ilivyodokezwa katika hotuba hiyo ya mkusanyiko, hilo laweza kufanywa katika mazungumzo ya jamaa.
NENO LA MUNGU—SI LA MWANADAMU
7 The Bible—God’s Word or Man’s? kitabu kipya kilichotolewa mnamo Jumamosi, kimekusudiwa kisaidie watu wenye mioyo minyofu kuelewa kwamba Biblia imevuviwa na kwamba ina “kweli ile iletayo utauwa [ujitoaji kimungu].” (Tito 1:1) Jinsi kitabu hiki kipya chapasa kuwa motisha kwa kazi yetu! Lakini ili kukitumia kwa njia yenye matokeo shambani, ni lazima sisi binafsi tuzoeleane na sehemu zacho zenye kuagiza na kuweza kuvuta fikira kwenye mambo fulani hususa katika kitabu hicho tunapokitumia katika utumishi wa shambani.
8 Jinsi tulivyo na shukrani kwa Yehova sisi sote kwa ajili ya utele wa chakula cha kiroho cha wakati wake kilichopokewa kwenye “Ujitoaji Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya! Na tuazimie kudhihirisha uthamini wetu wa moyoni kupitia matumizi ya juhudi ya maandalizi hayo katika kufuatia kwetu ujitoaji kimungu. Hiyo itatia ndani kutumia maandalizi hayo katika kuwasaidia wengine wawe waabudu wa Mungu wetu mmoja na Baba, Yehova.