Kutoa Habari Njema—Katika Eneo Lenye Kufanyiwa Kazi Mara Nyingi
1 Kuhubiri katika eneo lenye kufanyiwa kazi mara nyingi hutokeza matatizo ya pekee. Unaendelezaje ujumbe ukiwa mpya na wenye kuvutia? Ni njia ipi inayoweza kutumiwa kuelekea wengine ambao huonekana kama wameamua kwamba hawapendezwi kabisa? Unaweza kusema nini kwa wale wanaosema kwamba tunawatembelea mara nyingi mno?
UWE NA MWELEKEO UFAAO
2 Tofauti na vile wengine wangefikiri, eneo lenye kufanyiwa kazi mara nyingi na kikamili, kwa ujumla huwa na matokeo mazuri zaidi ya yale ambayo tunatembelea mara chache. Hivyo kizuizi cha kwanza cha kushinda ni fikira zozote zisizofaa juu ya kutembelea milango ile ile kwa kawaida. Watu wahitaji kupewa kila fursa kusikia ujumbe wa Ufalme. Lingekuwa kosa kwa upande wetu kukata maneno kwamba Yehova amehukumu kuwa wasiostahili wale ambao hawajaitikia vizuri ijapokuwa tumewatembelea mara nyingi.
3 Kuonyesha hisia za huruma ni jambo la maana hasa katika eneo lenye kufanyiwa kazi mara nyingi. Kuwa na ujumbe hususa ambao huzungumzia yale yanayowapata watu katika ujirani wao yaelekea utatokeza itikio lifaao katika wengine ambao kama sivyo hawangesikiliza. Je! wewe unaenda sambamba na matukio ya karibuni zaidi, na je! wewe uko tayari kuonyesha jinsi ujumbe wa Biblia unavyoweza kusaidia watu washughulikie matatizo wanayokabili?
TUMIA NJIA MBALIMBALI
4 Tumia njia mbalimbali za kufikia watu katika eneo linalofanyiwa kazi mara nyingi. Wakati mmoja waweza kutumia trakti ikiwa sehemu ya utangulizi wako. Katika pindi nyingine mojawapo matangulizi zaidi ya 40 yaliyodokezwa katika kitabu Kutoa Sababu katika kurasa 9-15 waweza kutumiwa ufaane na mambo fulani ambayo yanahangaikiwa na watu katika eneo lenu. Hata huenda ukataka kutaja ziara yako iliyopita katika ujirani huo, na hivyo kupunguza jambo hilo kuwa msingi wa kipingamizi. Ikiwa uliandika maelezo fulani yenye maana yaliyotolewa na mwenye nyumba wakati wa ziara yako iliyopita, hayo yaweza kutumiwa kuwa njia ya kuwa na mazungumzo zaidi yenye kuamsha kupendezwa.
5 Waone watu kama Yehova anavyowaona, nawe endelea kuonyesha hangaikio kwa wale ambao huenda wametuambia kwamba hawapendezwi kabisa. Yehova aliwasihi kwa kurudia-rudia watu wake wa kale ujapokuwa ubaridi wao kuelekea wajumbe wake. (2 Nya. 36:15; Yer. 7:13) Wengi ambao wakati mmoja walihisi kwamba hawakupendezwa ni ndugu na dada zetu leo. Hata wapinzani wakali wamevutwa kwenye kweli. Hao ni wenye shukrani sasa kwamba mtu fulani aliendelea kuwatembelea kwa subira akiwa na habari njema.
WEKA MAANDISHI MAZURI
6 Ni jambo la maana kabisa kuweka maandishi mazuri ya nyumba kwa nyumba. Kufuatia wale ambao hawakuwa nyumbani kutahakikisha mwenezo kamili wa eneo na kuongeza wakati wa katikati ya ziara zetu kwa wale waliomo nyumbani. Wengine wameliona kuwa jambo zuri pia kubadilishana maandishi ya wasiokuwa nyumbani wakati wa utendaji wa katikati ya juma na wale wanaofanyia kazi eneo wakati wa miisho ya juma. Jambo hilo hutofautisha kwa mafanikio nyakati ambazo wenye nyumba hutembelewa na kuongeza uwezekano wa kupata watu ambao daima hawamo nyumbani katika nyakati fulani za siku na katika siku fulani za juma. Madokezo zaidi yaweza kupatikana katika Mnara wa Mlinzi wa Julai 15, 1988, kurasa 15-20.
7 Yehova ajua wakati jitihada za kutosha zimefanya kufikia wote ambao watasikia. Chini ya uongozi wa Kristo, tutaendelea kumtii, tukiwa na hakika kwamba kazi yetu itamalizwa kwa wakati ambao imegawiwa.—Eze. 9:11.