Tumia Lile Neno la Kweli kwa Ustadi
1 Ustadi wetu katika kutumia Neno la Mungu waweza kuathiri jinsi watu wanavyoitikia habari njema. Hivyo, Paulo alitia moyo kukuza ufundi katika utumishi, akisema: “Fanya yote yote uwezayo kujiweka mwenyewe mbele za Mungu katika hali ya kukubaliwa, mfanyi kazi asiye na lo lote la kuaibikia, ukitumia lile neno la ile kweli sawasawa.”—2 Tim. 2:15, NW.
2 Ustadi katika kutumia Biblia lazima ukuzwe. Kuweka kando wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni kwa lazima. Hata hivyo, ni lazima tujizoeze mambo tunayojifunza kwa kutumia Biblia kwa ukawaida katika utumishi. Hilo lataka bidii nyendelevu tukitafuta msaada na mwongozo wa Mungu.—1 Yn. 3:22.
3 Kazia Neno la Mungu: Ni jambo la maana watu waelewe kwamba ujumbe wetu hautokani na sisi wenyewe bali watokana na Neno la Mungu lililoandikwa. (Yn. 7:18) Kuonyesha mtu lile Mungu asemalo kuhusu jambo fulani katika Biblia kwaweza kuwa na tokeo kubwa. Watu wenye mioyo ya haki huvutwa kwenye ujumbe wenye nguvu wa Biblia. Tutumiapo zaidi na zaidi Maandiko, tunakuwa wenye ufundi zaidi na tutaweza kuwafahamisha wengine wazi zaidi Neno la Mungu, jambo ambalo litakuwa lenye faida kwao.
4 Watu walio wengi hawaifahamu Biblia. Tunapoitumia, ni lazima tufanye zaidi ya kusoma tu maandiko. Kujitayarisha kwa makini ni kwa lazima ili kujua jinsi ya kutanguliza andiko. Maswali au tatizo lililotajwa yaweza kutumiwa ili kuamsha kupendezwa. Pia, uangalifu lazima utolewe kwa yale tunayosema baada ya andiko kusomwa. Mtu huenda asiweze kuelewa jambo kuu katika usomaji mmoja tu. Kukazia tena maneno makuu na kuyatolea utumizi wayo kutafanya mawazo hayo yaeleweke.—Ona Kiongozi cha Shule, masomo 24 na 25.
5 Toleo: Tunapowapata watu wakati wa Novemba ambao wanapendezwa kikweli, tutawatolea New World Translation of the Holy Scriptures pamoja na The Bible—God’s Word or Man’s? Tunawezaje kuwafikia watu na toleo hilo? Bado tunatumia Kichwa cha Mazungumzo, “Dini Inayompendeza Mungu,” na waweza kutumia mfikio ulioonyeshwa katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Julai 1991 au dokezo katika fungu la 6 la makala “Kufahamu Umaana wa Matukio ya Wakati Huu” kama linavyopatikana katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Oktoba 1991. Ikiwa unapenda, ungeweza hata kusema: “Watu wengi wanapenda kujua jinsi ya kumwabudu Mungu katika njia inayokubalika Kwake. Je! umeshapata kujiuliza ni nini hufanya dini kuwa yenye kumpendeza Mungu? Kuna maoni mengi yanayotofautiana kuhusu hilo lakini Yesu alionyesha kwamba si dini zote zinazompendeza Mungu. Angalia maneno yake hapa katika Mathayo 7:13, 14.” Halafu ungeweza kuendelea na Kichwa cha Mazungumzo.
6 Baada ya kutumia Tito 1:16 kuonyesha umaana wa kuishi kulingana na viwango vya juu vya adili za Biblia ungeweza kuonyesha New World Translation na kueleza kwamba maelezo yake ya kisasa yamekusaidia kukua katika heshima na uthamini wa Biblia. Kazia kwamba mafundisho ya Biblia yatahakikisha kwamba anaabudu katika njia inayofaa, yakiandaa faida sasa, na pia tumaini thabiti kwa wakati ujao. Labda mazungumzo hayo yatatoa fursa ya kumtolea mwenye nyumba funzo la Biblia nyumbani bila malipo.
7 Nyakati zote Yesu alielekeza kwenye Maandiko ili kusaidia wenye kufuata haki na kukanusha wapinzani wake. Ilikuwa desturi ya Paulo ‘kueleza na kuthibitisha kwa marejezo’ mambo aliyofunza. (Mdo. 17:2, 3, NW) Uhakika na shangwe yetu katika utumishi itaongezeka tukijitahidi kwa bidii kuwa wastadi hata zaidi katika kulitumia Neno la kweli.