Kutumia Trakti Ili Kuwa na Matokeo Yenye Manufaa
1 Tengenezo la Yehova la ki-siku-hizi lina historia ya kutumia trakti kwa mafanikio. Jina lenyewe la shirika letu halali, Watch Tower Bible and Tract Society, linadokeza kwamba trakti zina sehemu muhimu katika kueneza habari njema. Tangu 1881 hadi 1918, trakti zaidi ya milioni 300 ziligawanywa na watu wa Yehova. Wengi wa wale waliokuja kuwa sehemu ya mabaki ya ndugu za Kristo katika kipindi hicho walijulishwa kweli kwa mara ya kwanza kupitia trakti hizo za mapema.
2 Katika 1987 mkazo mpya uliwekwa juu ya utumizi wa trakti ndogo kwa kutokezwa kwa trakti nne za rangi-rangi ambazo zimepatikana tangu wakati huo. Je! wewe unatumia trakti zote nne ili kuwa na matokeo yenye manufaa katika huduma yako?
3 Matokeo mazuri hutokana na kutumia trakti kwa mafanikio. Twahitaji kupata kufahamu kila moja yazo. Bila shaka, umezisoma kwa uangalifu ili kupata kujua yale ambayo kila moja inazungumzia. Je! umefikiria ni mtu wa aina gani atakayevutiwa na kila trakti? Kupata kufahamu kila trakti kikamili kutajenga uhakika wako katika kuzitumia katika kazi ya nyumba kwa nyumba pamoja na hali nyinginezo nyingi ambamo waweza kutoa ushahidi wa vivi hivi.
4 Tumia Katika Huduma ya Nyumba kwa Nyumba: Mwangalizi mmoja wa mzunguko aandika hivi: “Ninapata mafanikio mazuri kwa kuanza mengi ya mazungumzo yangu kwa trakti.” Je! umejaribu mfikio huo? Kwa nini usitumie trakti zikiwa njia ya kutanguliza mazungumzo yako? Kukiwa na trakti mbalimbali, tuna matangulizi kadhaa yenye kuchochea ya kuchagua kutoka kwazo. Kila trakti latupa sisi nafasi ya kuanzisha funzo la Biblia ama kwenye ziara ya kwanza ama kwenye ziara ya kurudia.
5 Kuna nafasi nyinginezo za kutumia trakti. Wakati wa mazungumzo mlangoni, huenda ukapata kujua kwamba mtu huyo amefiwa na mpendwa hivi karibuni au kwamba mtu fulani katika familia ni mgonjwa. Watu wanaopatwa na huzuni nyingi sana au wanaojaribu kukabiliana na magumu yenye kudumu muda mrefu mara nyingi huanza kuwa na hisiamoyo zisizofaa na hushuka moyo. Waweza kupata kujua kwamba mtu huyo alitalikiwa hivi karibuni au kwamba amepoteza kazi yake ya kuajiriwa au ana matatizo ya nyumba au anatendwa vitendo vya jeuri au chuki. Lingekuwa jambo lenye upendo kama nini kushiriki ule ujumbe wenye kutia moyo unaopatikana katika zile trakti Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa? na Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani. Mawazo yenye kufariji kwenye kurasa 5 na 6 za trakti Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa? kwa kweli ni yenye kutumika sana pamoja na kuwa yenye kuchochea tumaini. Hata ingawa mtu huyo huenda asisome trakti hiyo mara hiyo inawezekana kwamba atafanya hivyo baadaye.—Mhu. 11:6.
6 Katika makundi mengine eneo limefanywa kazi mara nyingi, na watu wengi tayari wana baadhi ya fasihi yetu. Kwa kutumia trakti, tutakuwa na nafasi ya kuzungumza jambo fulani lenye kupendeza pamoja na mwenye nyumba, kuvuta maoni yao, na kuwafanya wafikiri juu ya tumaini la Ufalme. Panda swali akilini mwao liwezalo kuzungumziwa baadaye. Fanya ziara ya kurudia, na usitawishe zaidi kupendezwa huko. Baadaye huenda tukaweza kuanza kujifunza nao kwa kutumia broshua au kitabu walicho nacho tayari.
7 Tumia Trakti Vivi Hivi: Tukiweka trakti mahali tuwezapo kuzipata kwa urahisi—katika kifuko cha shati, kifuko cha koti, kibeti, au mfuko wetu wa kutoa ushahidi—twaweza kuzitumia katika pindi nyingi tofauti-tofauti, mahali popote ambapo watu waweza kupatikana. Zitumie unapofanya ununuzi, unaposafiri, au kuongoea na watu wa ukoo au wageni. Trakti zinatupatia nafasi ya kutoa ushahidi mfupi. Trakti si kitu chenye kumlemea mtu bali ni ya moja kwa moja na yenye busara. Inakubaliwa kwa utayari zaidi ya kitabu au magazeti, kwa kuwa hakuna mengi sana ya kusomwa.
8 Uwe chonjo kwa nafasi za kutoa trakti vivi hivi shuleni au kazini mwako, kwenye mikahawa, kwenye stesheni za petroli, na kadhalika. Alipokuwa akifanya mipango ya kumpeleka nyanya yake kwa daktari, dada moja alihakikisha kwamba alikuwa na trakti. Kwenye ofisi ya daktari, alianzisha mazungumzo pamoja na mama mmoja aliyekuwa mja mzito. Baada ya kumwonyesha mwanamke huyo ile trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani, dada huyo aliuliza hivi: “Je! ungependa kumlea mtoto wako katika ulimwengu ulioonyesha katika picha hii?” Aliweza kufuatia mazungumzo hayo kwa kutembelea nyumba ya mwanamke huyo. Hilo liliongoza kwenye ziara kadhaa za kurudia za kawaida.
9 Mafunzo ya Biblia Yanaweza Kuanzishwa kwa Trakti: Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliripoti kwamba kundi alilokuwa akizuru lilianzisha mafunzo ya Biblia nyumbani 64 katika juma hilo kwa kutumia trakti wakati wa kumsalimia mwenye nyumba mwanzoni.
10 Je! umejaribu kutoa funzo la Biblia kwenye ziara za kwanza za nyumba kwa nyumba? Kwa kutumia trakti, ungeweza kutoa wonyesho kifupi wa jinsi ambavyo funzo huongozwa. Dada mmoja alifanya hivyo kwa kutumia ile trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani. Akielekeza kwenye picha, alimwuliza mwenye nyumba ikiwa alifikiri dunia yetu ingepata kuwa hivyo wakati wowote. Baada ya mwenye nyumba kujibu, dada alimwalika asome 2 Petro 3:13 na Isaya 65:17, ambayo yamekaziwa katika trakti hiyo. Halafu dada wetu akasema hivi: “Ahadi hizo si ndoto wala fantasia bali zimefanywa kwa kweli katika Neno la Mungu, Biblia.” Kisha akapanga kuendelea na mazungumzo juma lifuatalo. Kwenye ziara ya kurudia, maswali kadhaa ya mwanamke huyo yalijibiwa na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani kikaachwa. Funzo la Biblia lakatokea.
11 Je! wewe ni mmoja aliyebatizwa hivi karibuni au labda ni mhubiri asiyebatizwa anayepata ujuzi katika huduma? Ikiwa ndivyo, huenda ukataka kuwatafuta wale wenye ujuzi zaidi na kuwaomba madokezo yao juu ya kutumia trakti katika eneo la kundi lenu. Tuna vielelezo vingi katika Biblia vya wale waliopokea kitia-moyo na mwelekezo kutoka kwa wale waliokuwa wakomavu katika imani.—Mdo. 18:24-27; 1 Kor. 4:17.
12 Kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kundi aweza hasa kuwa mwenye msaada katika kufanya mipango ili wengine wakupe wewe msaada katika kutumia trakti kwa matokeo. Wazazi wana daraka la kuwasaidia watoto wao wafanye maendeleo katika kazi ya kuhubiri. Shahidi mmoja mchanga alizoezwa na wazazi wake kutoa trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani. Alipokuwa pamoja na mama yake kwenye funzo la Biblia, alimtolea trakti mume wa mwanamke huyo mwenye kupendezwa. Mume huyo alivutiwa kwamba mtu mchanga angekuwa na usadikisho imara wa kidini. Alifurahia sana kusoma trakti hiyo. Kila wakati msichana huyo mchanga aliporudi pamoja na mama yake, alishiriki andiko au hadithi ya Biblia aliyokuwa ametayarisha hasa kwa ajili ya mume huyo. Sasa mtu huyo husoma magazeti kwa kawaida, ameonyesha kupendezwa katika kitabu Upeo wa Ufunuo, na amehudhuria mikutano michache. Yote hayo yalitokea kwa sababu wazazi walichukua wakati kutunza madaraka yao katika kufundisha binti yao kutumia trakti vizuri.
13 Tumia Trakti Zetu kwa Matokeo: Katika kutumia trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani, ungeweza kujijulisha mwenyewe na kuanza mazungumzo yako kwa kusema hivi: “Habari. Sisi tunaongea na watu juu ya hali ya maisha leo. Je! unafikiri hali ya maisha itakuwa bora zaidi, au itaendelea kudhoofika kukiwa na ongezeko la uhalifu, njaa, na ugonjwa? [Ruhusu jibu.] Wengine hufikiri kwamba hakuna masuluhisho yoyote kwa hayo matatizo mengi tunayokabili. Wewe unaonaje?” Baada ya mwenye nyumba kuitikia, toa trakti na uelekeze fikira kwenye sehemu ya juu ya ukurasa 2 na kwenye Sala ya Bwana na kwenye uhakika wa kwamba Ufalme wa Mungu utasuluhisha matatizo na taabu zetu zote. Halafu endelea kwa kutumia jambo moja au mawili chini ya kichwa kidogo “Uzima Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu” kuanzia ukurasa 3. Ziara inapofikia mwisho, pangia ziara nyingine ili kuzungumzia mambo yanayobaki chini ya kichwa kidogo kilichotajwa juu au chini ya kichwa kidogo cha mwisho kitakachoonyesha jinsi mwenye nyumba awezavyo kufurahia uzima katika ulimwengu mpya wenye amani.
14 Nyakati nyingi sisi hujipata wenyewe katika hali ya kuweza kushiriki ujumbe wa Ufalme pamoja na wengine kifupi tu, kama vile kazini au shuleni. Kazini mwako, huenda mazungumzo yakatokea kuhusu kama Biblia hujipinga yenyewe. Waweza kukubali kwamba kuna madai mengi ya jinsi hiyo lakini yanapochunguzwa kwa uangalifu hakuna uthibitisho wowote wa kutegemeza madai hayo. Halafu ungeweza kurejezea fungo la mwisho la ukurasa 2 la trakti Sababu Kwa Nini Wewe Unaweza Kuitumaini Biblia na kusoma na kuzungumzia kile kielelezo kuhusu ni wapi Kaini alikopata mke wake. Ikiwa hakuna wakati wa kufuatia jambo hilo basi jaribu kufanya mipango ya kuzungumzia sehemu nyingine ya trakti hiyo, labda ile inayoshughulikia usahihi wa Biblia katika kutabiri matukio ya wakati ujao.
15 Mkiwa watu mmoja mmoja au familia, chukueni wakati wa kufikiria namna ya kutoa kila moja ya trakti hizo tofauti-tofauti. Mwe na vipindi vya kujizoeza. Unaweza kutumiaje trakti hizo pamoja na fasihi nyingine inayotokezwa katika huduma ya shambani mwezi huo? Una miadi zipi zinazokaribia ambako ungeweza kuchukua trakti chache na wewe? Je! utakutana na mtu fulani juma hili ambaye aweza kunufaishwa na ule ujumbe unaofaana na wakati unaotolewa na trakti hizo?
16 Upendo mwingi kwa Yehova na ufikirio kwa watu utatusukuma tufanye yote tuwezavyo katika kujulisha habari njema. Kutumia trakti kwa ukawaida kutatusaidia tufanye hivyo. Mvulana mmoja mchanga, mwenye miaka saba, alitaka kumsaidia jirani yake aweze kuingia mfumo mpya, kwa hiyo alimpa trakti, na funzo la Biblia likaanzishwa. Linasikika kuwa jambo rahisi sana! Lakini je, sisi huthamini mfikio huo rahisi katika huduma yetu? Mara nyingine tunapomwachia mtu trakti, huenda ikaongoza kwenye funzo la Biblia pia. Tukitumia trakti kwa hekima katika kuhubiri habari njema za Ufalme, kwa hakika tutapata matokeo yenye manufaa.